Ferdinand Magellan

Ferdinand Magellan (148027 Aprili 1521; Kireno: Fernão de Magalhães; Kihispania: Fernando de Magallanes) alikuwa baharia na mpelelezi kutoka Ureno katika utumishi wa mfalme wa Hispania aliyekuwa mtu wa kwanza wa kuwa na safari iliyozunguka dunia yote.

Ferdinand Magellan

Baharia wa Ureno hariri

Magellan alizaliwa katika familia ya makabaila wadogo wa Ureno akaingia katika huduma ya mfalme wa Ureno akiwa kijana mdogo. Alipata mafunzo ya misingi ya ubaharia na kutumwa kwa jahazi hadi koloni za Ureno kule Uhindi. Hapa alipanda ngazi hadi kuwa nahodha akarudi Ureno. Alipokuwa na umri wa miaka 24 alipoteza kazi yake baada ya kupatikana kuwa na biashara na Waarabu isiyoruhusiwa.

 
Safari ya Magellan na jahazi zake

Kuhamia katika utumishi wa Hispania hariri

1517 aliomba ajira kwa mfalme wa Hispania aliyemtafuta nahodha hodari wa kujua siri za Wareno. Hispania ililenga kufika kwenye "visiwa vya India" vinavyoitwa leo Indonesia na Ufilipino kwa sababu utajiri uliodhaniwa kupatikana kule. Utajiri huu ulikuwa hasa pilipili na viungo vya chakula vilivyotafutwa sana Ulaya vikawa na bei kali kwa sababu biashara yote ilipitia mikono mingi hasa ya Waislamz mbalimbali wenye uhusiano wa kivita na nchi za Ulaya.

Mfalme kijana Carlos I wa Hispania aliyechaguliwa 1519 kuwa Kaisari Karolo V wa Dola Takatifu la Roma alimpokea Magellan akapatana naye kumpa jahazi 5. Agizo lake lilikuwa kukuta njia ya mpito upande wa magharibi kufika kwenye visiwa vya viungo vya India.

Mipango ya Hispania ya kuelekea Uhindini hariri

Wakati ule Wareno walifaulu tayari kufika Uhindi kwa kuzunguka bara la Afrika na kuelekea mashariki. Mkataba wa Tordesillas yaliwapa haki ya pekee ya kutumia njia hiyo. Hispania ilijaribu kufika Uhindi kwa njia ya magharibi. Kolumbus aliwahi kufika Amerika alichoita "India" lakini hadi 1520 ilionekana tayari ya kwamba Uhindi iliyotafutwa kwa utajiri wake ilikuwa tofauti na nchi na visiwa vilivyopelelezwa na Kolumbus. Bahari kuwbwa iligunduliwa ng'ambo ya Amerika ya Kati ikaaminiwa ya kwamba Uhindi yenyewe ulikuwa nyuma ya bahari ile ya magharibi.

Wahispania waliona haja ya kukuta nafasi iliyoruhusu mpito kutoka Atlantiki kwenda bahari ile upande wa magharibi wa Amerika. Wakati ule umbo la mabara ya Amerika ya Kaskazini na Amerika ya Kusini halijulikani bado.

Safari kubwa ya Magellan hariri

Tar 10 Agosti 1519 kundi la jahazi 5 liliondoka mjini Sevilla. Magellan alikuwa na watu 234, kati yao Wahispania 170, Wareno 40, Waitalia 20 halafu Waafrika na Waasia 4 kama wafasiri.

Kupitia visiwa vya Kabo Verde alielekea Brazil akafika tar. 6 Desemba 1519. Tar 13 Desemba alipumzika katika hori aliyoita kwa heshima ya Mtakatifu Januari na jina limekaa leo hii panaitwa "Rio de Janeiro". Walipokelewa vizuri na Maindio wenyeji walioamini ni miungu kwa sababu walileta mvua baada ya ukame.

 
Jahazi kuu ya Magellan ilikuwa Victoria

Wakaendelea kuelekea kusini wakitafuta mpito wa kwenda magharibi. Walipofika kwenye mdomo wa Rio de la Plata walitumaini kwa muda ya kwamba hapa palikuwa mpito wakatumia mwezi mmoja kupeleleza hori.

Uasi katika Patagonia hariri

Mwisho wa Machi 1520 walikuwa kweye pwani la Patagonia katika kusini ya Argentina ya leo. Waliona majira ya baridi ilianza wakaamua kukaa pwani hadi mwisho wa baridi wakajenga vibanda. Chakula kilikuwa haba na Magellan aliamua kupunguza chakula cha kila siku. Nahodha 2 pamoja na sehemu ya watu waliasi dhidi yake na mapigano yalitokea. Magellan aliweza kushinda nahodha waasi walinyongwa na viongozi wengine kufukuzwa porini.

Jahazi moja ilitumwa kupeleleza mazingira ikaharibika ikazama. Jahazi nne zilizobaki ziliendela baada ya miezi saba wakati wa Oktoba 1520. Magellan aliendelea kuchunguza kila horina kila mdomo wa mto akitafuta njia ya mpito.

 
Mlangobahari wa Magellan kwenye kusini ya Amerika

Mpito kwa Pasifiki hariri

21 Oktoba 1520 jahazi nne zilifika kwenye rasi moja waliyoita Cabo Vírgenes "rasi ya bikira" na Magellan alituma jahazi mbili kupeleleza hori nyuma ya rasi. Ikaonekana ya kwamba hori lilingia sana ndani ya nchi na kuelekea magharibi wakaona labda ni mlango bahari. Hapa Magellan aliitisha mkutano wa nahodha wa jahazi zote. Waendelee au wasiendelee? Mmoja tu alipendelea kurudi nyuma wengine wakanyamaza au kusema sawa. Wakaendelea pamoja.

Njia waliyofuata inaitwa leo hii mlango bahari ya Magellan. Mpito mara nyini ni nyembamba kuna visiwa vingi na kuna nafasi mbalimbali za kuendelea. Hapa Magellan aliamua kugawa kundi tena. Akisubiri mwenyewe alituma jahazi mbili na boti moja kupeleleza njia tatu. Boti ilirudi mapema ikaleta taarifa ya kwamba njia yake iliishia baharini. Lakini jahazi moja tu kati ya mbili ilirudi. Kwenye jahazi nyingine palitokea uasi waasi wakashinda wakarudi Hispania.

Kwenye Pasifiki hariri

Tar 28 Novemba 1520 jahazi 3 ziliingia katika bahari upande wa magharibi ya Amerika. Magellan aliita "Bahari Pasifiki" kwa sababu kinyume cha Atlantiki ya kusini walipotoka bahari hii ilionekana kitulivu sana.

Magellan alikadiria ya kwamba wangehitaji bado mwezi mmoja hadi visiwa vya India. Hali halisi ilichukua miezi 3 na siku 20 bila kukuta nchi kavu. Chakula hakikutosha watu wakaanza kupika ngozi na supu ya unga wa ubao. Aliyefaulu kukamata panya kwenye tumbo la jahazi alibahatika sana kuonja nyama. Mabaharia 19 angalau walikufa katika kipindi hiki.

6 Machi 1521 Wahiapania walifika kwenye visiwa vya Mariana. Hapa waliweza kupata chakula na kuweka akiba mpya kwenye jahazi.

Ufilipino hariri

Wakaendelea hadi visiwa vya Ufilipino walipofika 16 Machi. Wakati ule Magellan alikuwa bado na mabaharia 150. Waliweza kuwasiliana na wenyeji kwa sababu mfasiri Enrique Melaka alielewa lugha. Yeye alikuwa mmoja wa wafasiri 4 kutoka Afrika na Asia kundini na yeye alikuwa mweyeji wa visiwa vile. Aliwahi kusafiri Ulaya pamoja na Magellan alipofika hapa kama nahodha Mreno mara ya kwanza. Sasa Enrique alikuwa mtu wa kwanza katika historia aliyekamilisha safari ya kuzunguka dunia. Alikuwa ameondoka kuelekea magharibi na sasa alirudi kutoka upanda wa mashariki.

Kwa msaada wa Enrique Magellan alikutana na mfalme wa kisiwa cha Limasawa aliyeitwa Raja Kolambu. Aliwasindikiza Wahispania kwenda kisiwa cha Cebu walipokaa kwa mfalme Raja Humabon. Huyu mfalme pamoja na sehemu ya raia zake walikubali kubatizwa na kuwa Wakristo.

Kifo cha Magellan hariri

Mfalme yeye yule alikuwa na fitina na jirani yake kwenye kisiwa cha Mactan. Magellan aliamua kumsaidia rafiki mpya kwa silaha zake. Tar. 27 Aprili 1521 Wahispania walifika Mactan lakini walishindwa na wenyeji walipaswa kukimbia. Magellan alikaa nyuma alijaribu kuwalinda watu wake kando la bahari walipopanda boti. Magellan alisimama tayari kwenye maji alipopigwa na mshale kwenye mguu. Alipoanguka chini alitobolewa na mikuki miwili akafa.


Kurudi baada ya kifo cha Magellan hariri

Wahispania waliobaki waliamua kurudi haraka. Baada ya kupotea watu wengi katika mapigano walikuwa na mabaharia kwa jahazi mbili tu. Jahazi ya tatu walibomoa.

Waliondoka Ufilipino wakaendelea kupitia Borneo na visiwa vya Indonesia ya leo. Hapa waliweza kunuua walichotafuta yaani pilipili na viungo vya chakula vya India. Katika sehemu hizi wenyeji walijua tayari watu wa Ulaya kwa sababu Wareno waliwahi kufika mara kadhaa.

Tar. 21 Desemba jahazi ya kwanza iliondoka kwenda Ulaya ilikuwa na Wazungu 47 na Wasia 13. Jahazi ya pili ilibaki kwa matengenezo ikafuata lakini ilikamatwa baadaye na Wareno wasiofurahia kuona Wahispania katika maeneo waliyosikia ilikuwa bahari na biashara yao. Mabaharia 5 tu wa jahazi ya pili waliweza kurudi Hispania baada ya kukamatwa na ufungoni.

Jahazi ya kwanza iliyoitwa "Victoria" ilivuka Bahari Hindi kwa matatizo kutokana na hali ya hewa na dhoruba. Waliendelea katika Atlantiki wakafika kwenye visiwa vya Kabo Verde vilivyokuwa chini ya Ureno. Hadi kufika hapa mabaharia 21 walikufa tayari baharini kutokana na magonjwa. Baada ya kuingia bandarini Wareno walikamata mabaharia 13. Nahodha ya Victoria aliamua kuondoka mara moja kabla ya Wareno hawakushambulia jahazi bado. Wakaelekea Hispania moja kwa moja.

Tar. 6 Septemba 1522 Victoria iliingia katika bandari ya Sanlucar nchini Hispania. Watu 18 pekee kati ya 256 walioondoka pamoja walikuwa wakikamilisha safari ya kwanza ya kuzunguka dunia baada ya miaka 2, miezi 11 na wiki 2.

Jahazi Victoria ilibeba mzigo wa tani 25 za viungo na thamani yake ilitosha kulipia gharama zote za kifedha za msafara huu pamoja na upotevu wa jahazi nyingine.