Historia ya Moroko

Historia ya Moroko inahusu eneo ambalo leo ni nchi ya Afrika kaskazini-magharibi.

Moroko ya Kale hariri

Habari za kimaandishi za kwanza ni kutoka karne za kwanza KK. Wafinisia walijenga miji yao pwani lakini eneo la ndani lilibaki nchi ya Waberber waliounda ufalme wa Mauretania ya Kale (usiuchanganye na nchi ya kisasa Mauretania) uliounganisha sehemu kubwa ya Moroko ya kaskazini.

Wamauretania wa kale walishirikiana na Dola la Roma hadi kuwa jimbo la dola hili kwa jina la "Mauretania Tingitana".

Wakati wa kudhoofika kwa Dola la Roma kuanzia mwaka 400 BK kukawa na uvamizi wa Wavandali.

Uvamizi wa Kiarabu hariri

Karne ya 7 BK ilileta uvamizi wa Waarabu walioteka nchi na kusababisha polepole Waberber (waliokuwa Wayahudi, Wakristo au wafuasi wa dini za jadi) kuwa Waislamu.

Mwanzoni Moroko ilikuwa sehemu ya milki ya khalifa ya Waomawiyya waliotawala Dameski (Siria). Baada ya kupinduliwa kwa Waomawiyya na Waabasiya wa Baghdad (Iraq) mkimbizi Mwarabu Idris ibn Abdallah (788-791) alikusanya makabila ya Waberber na kuunda milki ya kujitegemea. Hii ilikuwa mwanzo wa Moroko kuwa milki ya Kiislamu inayojitawala.

Watawala wa kienyeji hariri

Vipindi vya historia husebabiwa kufuatana na familia zilizofuatana za wafalme Waarabu au Waberber.

 
Eneo la utawala wa Wamurabitun

Moroko ilitawaliwa na familia za (miaka BK)

Murabitun na Muwahidun hariri

Wafalme wa Wamurabitun (Almoravi) (1073-1147) na wa Wamuwahidun (Almohad) (1147-1269) walieneza utawala wao hadi Afrika ya Magharibi (Mauretania, Senegal na Mali ya leo) na sehemu kubwa ya Andalusia (Hispania ya Kiislamu), tena hadi mipaka ya Misri.

Wamuwahidun waliendelea kupanuka kuelekea Misri lakini baadaye walidhoofika wakapaswa kuwaachia Wahispania Wakristo sehemu za Andalusia. Athira ya milki ya Moroko ilipungua baadaye hadi Hispania yote ikarudishwa kwa watawala Wakristo mwaka 1492; pia utawala kusini kwa Sahara haukuendelea.

Wareno wa Wahispania waliendelea kuteka miji kwenye pwani za Moroko. Utawala wa Hispania juu ya Ceuta na Melilla leo ni mabaki ya nyakati zile.

Sehemu za nchi zilianza kujitawala bila kukubali tena mamlaka wa juu, kwa mfano makabila ya Waberber milimani au miji ya Rabat na Sale iliyounda dola dogo la Jamhuri ya Bou Regreg katika karne ya 17 na kujishughulisha na uharamia.

Waalawi (1666 hadi leo) hariri

Katika karne ya 17 familia ya Waalawi walishika mamlaka wakaendelea nayo hadi leo. Waliweza kutunza uhuru wa nchi hadi mwanzo wa karne ya 20. Lakini mwanzo wa karne ya 20 Ufaransa na Hispania walimlazimisha mfalme Mulay Abdelaziz kukubali mkataba uliofanya Moroko kuwa kama koloni chini ya nchi hizo mbili.

Vita Kuu ya Pili ya Dunia ilidhoofisha Ufaransa pamoja na kuingia kwa wanajeshi Waamerika na Waingereza na ahadi zao za kuleta uhuru tokeo lililohamasisha wazalendo wa Maroko kupigania upya uhuru wa nchi.

Baada ya vita Wafaransa walijaribu kukandamiza mwendo huo wakamwondoa Sultani Mohammed V nchini 1953. Ghasia zikaongezeka, Sultani akarudi na nchi ikapewa uhuru mwaka 1956.

Utawala wa mwanae Hassan II kuanzia mwaka 1961 uliitwa "miaka ya risasi" kwa sababu mfalme alikataa kukubali utaratibu wa kidemokrasia. Chaguzi zilikuwa za uwongo, wapinzani wakatupwa jela au kuuawa. Hassan II alishinda majaribio mbalimbali ya kumpindua. Siasa ya kushikamana na Marekani ilimsaidia mfalme kimataifa lakini baada ya mwisho wa "vita baridi" alilazimishwa na Wamarekani kulegeza utawala wake.

Mtoto wake Muhamad VI akawa mfalme kijana mwaka 1999 akaanza mageuzi ya kisiasa ya wazi zaidi.

  Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Historia ya Moroko kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.