Izazi ni kata ya Wilaya ya Iringa Vijijini katika Mkoa wa Iringa, Tanzania, yenye Postikodi namba 51217.

Inaundwa na vijiji vitatu tu, yaani Izazi, Makuka na Mnadani, vyote vikiwa katika Bonde la Ufa kwenye bwawa la Mtera (ambalo likijaa kabisa liko mita 698.5 juu ya usawa wa bahari). Ndiyo sehemu ya chini zaidi katika Nyanda za Juu za Kusini Tanzania.

Siku hizi barabara inayopita kijijini ikiunganisha Iringa na Dodoma, hivyo pia Cape Town na Kairo, imetiwa lami.

Wakazi hariri

Katika sensa iliyofanyika mwaka 2022 wakazi walihesabika kuwa 8,764 [1]. Kwa mujibu wa sensa iliyofanyika mwaka wa 2012, kata ilikuwa na wakazi wapatao 5,281 waishio humo.[2]

Upande wa dini, baada ya ile ya jadi, Waarabu waliohamia kutoka Yemen kwa ajili ya biashara na uwindaji wakati wa ukoloni wa Waingereza walileta Uislamu. Kuanzia mwaka 1953 Ukristo ulienea zaidi kwa juhudi za Wakatoliki, halafu za Waanglikana. Siku hizi mchanganyiko wa watu umezidisha pia wingi wa madhehebu.

Uchumi hariri

Eneo ni kubwa sana na lenye rutuba lakini watu ni wachache hasa kutokana na uhaba wa mvua ambayo kwa kawaida inaishia milimita 300 kwa mwaka. Kwa sababu hiyohiyo kilimo kikuu ni cha mtama.

Muhimu zaidi kiuchumi ni ufugaji: utovu wa ndorobo ulivutia kwanza Wasagara kutoka wilaya ya Kilosa (mwisho wa karne XIX), halafu Wamasai kutoka Mkoa wa Arusha (mwanzo wa karne XX). Ni vigumu kusema kama Wahehe, watawala wa eneo hilo, walikuwa wanaishi huko kabla ya wote, au walihamia pamoja na Wasagara. Baada yao Wagogo wengi walihamia kutoka Mkoa wa Dodoma. Ndiyo makabila manne yaliyochangia zaidi mwanzo wa makazi.

Baada ya bwawa la Mtera kupatikana, uvuvi umekuwa kivutio kipya kwa watu kutoka Tanzania nzima, ingawa uwezekano wake unategemea wingi wa maji.

Marejeo hariri

  Kata za Wilaya ya Iringa Vijijini - Tanzania  

Idodi | Ifunda | Ilolompya | Itunundu | Izazi | Kalenga | Kihanga | Kihorogota | Kising'a | Kiwere | Luhota | Lumuli | Lyamgungwe | Maboga | Magulilwa | Mahuninga | Malengamakali | Masaka | Mboliboli | Mgama | Migoli | Mlenge | Mlowa | Mseke | Nyang'oro | Nzihi | Ulanda | Wasa


  Makala hii kuhusu maeneo ya Mkoa wa Iringa bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Izazi kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.