Chuo Kikuu cha Al-Azhar

Chuo Kikuu cha Al-Azhar (kwa Kiarabu: جامعة الأزهر, jamiʿat al-azhar kwa heshima ya Fatima Zahra, binti wa Mtume Muhammad) katika Kairo (Misri) ni chuo kinachoheshimiwa kati ya Waislamu wa madhehebu ya Sunni kama kitovu cha elimu ya dini yao.

Al-Azhar.
Msikiti wa Al-Azhar mwanzoni mwa karne ya 20.

Baada ya chuo cha Al-Qairawin mjini Fez (Moroko) ni chuo kikuu cha kale kuliko vyote duniani kinachoendelea hadi leo hii.

Al-Azhar imejulikana hasa kama chuo cha Kiislamu, lakini leo hii kuna idara nyingi kama vile madhab (Sheria ya Kiislamu), lugha ya Kiarabu, tiba, ualimu, uhandisi na fani nyingine.

Historia hariri

Al-Azhar kilianzishwa wakati wa makhalifa Wafatima (wa Shia) kama chuo cha sharia kando ya msikiti wa Al-Azhar iliyojengwa mwaka 969 BK. Mwaka 975 mafundisho ya sheria ya Kiislamu yalianzishwa. Madrasa ya kufundisha kalam (teolojia ya Kiislamu) ilianzishwa mwaka 988.

Baada ya mwisho wa utawala wa Wafatima mwelekeo wa chuo ulikuwa wa Kisunni.

Baada ya anguko la Waabbasi kutokana na Baghdad kutwaliwa na Wamongolia mwaka 1258, Al-Azhar ilikuwa kitovu cha elimu ya Kisunni katika dunia ya Kiislamu ikabaki hivyo hadi leo.

Katika karne ya 20 chuo kilipanuliwa chini ya mfalme Faruk wa Misri, tena chini ya serikali ya kanali Gamal Abdel Nasser kwa kuongeza idara za kisasa.

Viungo vya nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu: