Akhenaten

(Elekezwa kutoka Farao Akhenaten)

Akhenaten (tamka akhen-aten, pia Echnaton) alikuwa farao (mfalme) wa nasaba ya kumi na nane ya Misri ya Kale. [1] Utawala wake ulikuwa 1353 KK - 1336 KK au 1351 KK - 1334 KK. Alitawala pamoja na mke wake, malkia Nefertiti.

Sanamu ya Akhenaten (leo katika makumbusho ya Luxor, Misri).
Akhenaten, malkia Nefertiti na watoto wawili wakiabudu Aten (Jua).

Akhenaten ni mmoja wa mafarao maarufu zaidi wa Misri. Alianza kutawala akitumia jina Amenhotep linalomaanisha "mungu Amun ameridhika" kuwa "Akhen-Aten" inayomaanisha ama "mtumishi wa Aten" au "Nuru ya Aten". Jina jipya lilisababishwa na mabadiliko yake ya kidini na kisiasa ambako alihamia kumwabudu pekee mungu wa Jua aliyemwita Aten. Kwa hiyo alianzisha dini ya kumwabudu Mungu mmoja, hata kama ibada za miungu mingine ziliendelea. Lakini kulikuwa pia na kipindi ambapo jina la Amun aliyewahi kuabudiwa kama mungu mkuu liliondolewa katika majengo mengi kwa amri ya mfalme. Wataalamu wanaamini Akhenaton alipambana pia na makuhani wa Amun waliomiliki utajiri wa mahekalu makubwa, [2] [3]

Baada ya kifo chake mafarao waliofuata hawakuendelea na siasa na mwelekeo wake wa kidini. Mwanawe aliyekuwa na jina Tutankhaten alibadilisha jina kuwa Tutankhamun na kurudisha ibada za awali zilizokuwa zilisimamishwa na baba yake. Mafarao waliofuata hata walijaribu kufuta kumbukumbu ya Akenaten kwa kuondoa jina lake kwenye majengo lilipoandikwa. Wanaakiolojia walitambiua maandishi katika miamba ambamo alama ya jina lake lilikatwa au kubadilishwa. [4] Hasa farao Horemheb aliharibu majengo na sanamu nyingi za Akhenaten.

Akhenaten alikuwa amesahauliwa kwenye historia hadi kugunduliwa kwa mji Amarna alioujenga kama mji mkuu wake kwa ajili ya ibada ya Aten. Ugunduzi wake na uchunguzi wa maghofu yake uliofanywa na profesa Mwingereza Flinders Petrie katika miaka baada ya 1892 ulivuta watalii waliotaka kuona mji huo ukasababisha farao na malkia wake Nefertiti kujulikana na watu wengi. Watu walivutwa na habari za dini mpya aliyoanzisha na sanaa mpya inayoonekana katika taswira za ukutani kwenye majengo ya Amarna. Baadaye ugunduzi wa kaburi la Farao Tutankhamun aliyekuwa mwana wa Anekhaten uliongeza umaarufu wake.

Marejeo hariri

  1. Shaw I (ed) 2000. The Oxford history of Ancient Egypt. Oxford University Press, p276.
  2. Redford, Donald B. 1984. Akhenaten: the heretic king. Princeton University Press.
  3. Aldred, Cyril 1991 [1988]. Akhenaten, King of Egypt. London: Thames and Hudson. ISBN 0500276218
  4. Manniche, Lise 2010. Akhenaten, Colossi of Karnak. Cairo: American University in Cairo Press.

Viungo vya nje hariri

Jua habari zaidi kuhusu Akhenaten kwa kutafuta kupitia mradi wa Wikipedia Sister
  Uchambuzi wa kamusi kutoka Wikamusi
  Vitabu kutoka Wikitabu
  Dondoo kutoka Wikidondoa
  Matini za vyanzo kutoka Wikichanzo
  Picha na media kutoka Commons
  Habari kutoka Wikihabari
  Vyanzo vya elimu kutoka Wikichuo
  Makala hii kuhusu mtu huyo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Akhenaten kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.