Frumensyo, kwa Kigeez ፍሬምናጦስ, Frēmnāṭōs (Turo, Lebanon, mwanzoni mwa karne ya 4 - Ethiopia, 383 hivi) alikuwa askofu wa kwanza wa Aksum, akiwa ndiye aliyeingiza Ukristo katika ufalme wa Aksum.[1]

Picha takatifu ya Mt. Frumensyo.
Mt. Frumensyo katika ufalme wa Aksum.

Mwaka 316 hivi, wakati alipotawala Kaisari Konstantino Mkuu kule Roma, meli moja ilikuwa safarini kutoka Shamu kwenda Bara Hindi ikaharibika kwenye pwani ya Ethiopia. Vijana wawili waliokolewa wakapelekwa mbele ya mfalme kule Aksum.

Mmojawao, kwa jina Frumensyo, alipata haraka sifa za kuwa mwenye elimu na hekima. Akapanda ngazi kuwa mshauri wa mfalme na mwalimu wa mwana wa mfalme aliyeitwa Ezana. Frumensyo aliweza kupanda mbegu za imani moyoni mwa kijana huyo. Baada ya kuwa mfalme, Ezana akaendelea kumtumia Frumensyo kama mshauri wake.

Siku moja Frumensyo aliomba ruhusa ya mfalme aende nyumbani kuangalia kama wazazi wake bado wanaishi. Mfalme akamruhusu akamwomba atafute kule walimu wanaoweza kufundisha elimu aliyokuwa nayo Frumensyo pamoja na imani ya Kikristo. Frumensyo akamwendea Atanasi wa Aleksandria, Askofu Mkuu wa Misri, aliyemweka wakfu kuwa askofu kwa ajili ya Waethiopia[2]. Hivyo Kanisa lilianza katika nyanda za juu za Ethiopia. Mfalme Ezana akabatizwa akifuatwa na watu wengi wa makao makuu.

Anaheshimiwa kama mtakatifu na Wakristo Waorthodoksi wa Mashariki, Waorthodoksi na Wakatoliki.

Sikukuu yake inaadhimishwa nao katika tarehe tofauti: 20 Julai[3], 18 Desemba[4], 30 Novemba na 27 Oktoba, lakini huko Ethiopia tarehe 1 Agosti.[5]

Tazama pia hariri

Tanbihi hariri

  1. Saheed A. Adejumobi (2007). The History of Ethiopia. Westport, Conn: Greenwood Press. uk. 171. ISBN 0-313-32273-2. 
  2. https://www.santiebeati.it/dettaglio/75400
  3. Martyrologium Romanum
  4. "Date of Feast/Consecration as Bishop of Ethiopia". Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2008-01-19. Iliwekwa mnamo 2015-07-26. 
  5. Festivals and Commemorations: Handbook to the Calendar in Lutheran Book of Worship, Augsburg Press, 1980

Marejeo hariri

  • Martyrologium Romanum, Editio Altera, (Citta del Vaticano: Libreria Editrice Vaticana, 2004), p. 401

Viungo vya nje hariri

  Makala hii bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mkristo huyu, kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Je, unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.