Argo au Merikebu ya Argo (lat. Argo Navis, ing. The Ship Argo) ni jina la kundinyota kubwa kwenye angakusi ya Dunia iliyojulikana tangu zama za kale. Haitumiki tena leo maana katika karne ya 19 wanastronomia wa Ulaya waliivunja na kuhesabu sasa makundinyota matatu ya Mkuku (lat. Carina au sehemu ya chini ya merikebu), Shetri (lat. Puppis au sehemu ya nyuma ya merikebu) na Tanga (lat. Vela au kitambaa kikubwa kinachopokea nguvu ya upepo).

Nyota za Argo, sasa Mkuku (Carina), Shetri (Puppis) na Tanga (Vela)
Argo Navis kwenye atlasi ya nyota ya Johannes Hevelius mnamo mwaka 1690

Argo ilikuwa kati ya makundinyota 48 yaliyoorodhehwa na Klaudio Ptolemaio wakati wa karne ya 2 BK. Jina linatokana na Argo, shujaa wa mitholojia ya Ugiriki ya Kale aliyesafiri kwa merikebu yake kutafuta lundo la manyoya ya kondoo ya dhahabu hadi mwisho wa Dunia iliyojulikana wakati wake. Waarabu waliita Al-Safina au pia Markab.

Wakati wa kuorodhesha nyota zote zilionekana baada ya kugunduliwa kwa darubini ilionekana idadi ya nyota za Argo zilikuwa nyingi mno; Nicolas-Louis de Lacaille alihesabu zaidi ya nyota 160 zilizopaswa kuorodheshwa na hii ilikuwa vigumu kwa kutumia majina ya Bayer yaliyokuwa kawaida, yaani kwa kutumia herufi ya alfabeti za Kigiriki pamoja na ya Kilatini. Hivyo Lacaille aligawa nyota za merikebu ya Argo kuwa sehemu tatu. Tangu karne ya 19 sehemu hizi zilihesabiwa kama makundinyota tofauti.

Argo Navis ni kundinyota ya pekee kutoka orodha ya Ptolemaio ambayo haikupokelewa kati ya makundinyota 88 za kisasa zilizotangazwa na Umoja wa Kimataifa ya Astronomia.

Viungo vya Nje

  • Argo Navis, tovuti ya Ian Ridpath "Star Tales", iliangaliwa Oktoba 2017
  • BAYER'S ARGO, tovuti ya Prof Jim Kaler, Unibversity of Illinois, iliangaliwa Oktoba 2017