Dhahari ya Dubu (lat. & ing. Dubhe pia α Alfa Ursae Majoris, kifupi Alfa UMa, α UMa) ni nyota angavu ya pili katika kundinyota la Dubu Mkubwa (Ursa Major).

Dhahari ya Dubu (Alfa Ursae Majoris, Dubhe)[1]
Kundinyota Dubu Mkubwa (Ursa Major)
Mwangaza unaonekana 1.7
(Zinazofuata ni tabia za nyota A)
Kundi la spektra K0 III
Paralaksi (mas) 26.54 ± 0.48
Umbali (miakanuru) 124
Masi M☉ 4.25
Nusukipenyo R☉ 30±
Mng’aro L☉ 316
Jotoridi usoni wa nyota (K) 4,660
Majina mbadala α Ursae Majoris, 50 UMa, BD+62°1161, CCDM J11037+6145AB, FK5 417, GC 15185, HD 95689, HIP 54061, HR 4301, PPM 17705, SAO 15384, WDS J11037+6145AB

Jina hariri

Dhahari ya Dubu inayomaanisha “Mgongo wa Dubu” ilijulikana vile kwa mabaharia Waswahili tangu miaka mingi wakifuata njia yao baharini wakati wa usiku kwa msaada wa nyota. [2]. Walipokea jina hili kutoka kwa Waarabu wanaosema ظهر الدب الأكبر dhahar ad-dub al-akbar inayomaanisha „mgongo wa dubu mkubwa" [3]. Hivyo walitafsiri maelezo ya Ptolemaio katika Almagesti aliyeandika "iliyo mgongoni"[4]

Kwa matumizi ya kimataifa Umoja wa Kimataifa wa Astronomia ulikubali jina la Kiarabu na kuorodhesha nyota hii kwa jina la "Dubhe" [5].

Alfa Ursae Majoris ni jina la Bayer ingawa ni nyota angavu ya pili tu; kwa sababu Alfa ni herufi ya kwanza katika alfabeti ya Kigiriki basi Dhahari ya Dubu ingepaswa kuwa nyota angavu zaidi katika Dubu Mkubwa - Ursa Major lakini si vile. Hapa Bayer alitumia herufi za Kigiriki kwa kufuata ufuatano unaoonekana angani, si uangavu.

Tabia hariri

Dhahari ya Dubu iko kwa umbali wa miakanuru takriban 123 kutoka Jua letu. Mwangaza unaoonekana ni mag 1.7 .

Kwa darubini kubwa imetambuliwa kuwa mfumo wa nyota nne zinazoshikamana na kuzunguka kitovu cha graviti cha pamoja. Kati yao ni jozi mbili za nyota.

Nyota kuu ni Dhahari ya Dubu A (Dubhe A) ambayo ni jitu jekundu inayoelekea kufikia mwisho wa maisha yake. Ina nusukipenyo cha R☉ 30 na mng'aro wa L☉ 200-300. Masi ya ni M☉ 4 pekee. Jotoridi usoni ni karibu K 5000.

Inazungukwa na Dhahari ya Dubu B inayoendelea kuyeyunganisha hidrojeni. Nuru yake inaonyesha kundi la spektra K0 V ikiunguka nyota A katika kipindi cha miaka 44.

Nyota C iko kwa umbali wa vizio astronomia 8000 (miakanuru 0.12) ni nyota ya kundi F8 V na masi yake inafanana na Jua letu. Inazungukwa kila baada ya siku 7 na nyota ndogo ndogo zaidi ambayo tabia zake hazikutambuliwa bado.

Kielekezo cha Nyota ya Ncha ya Kaskazini hariri

Kwenye angakaskazi nyota hii ni moja kati ya mbili zinazosaidia kukuta Kutubu (Polaris) ambayo ni nyota ya ncha ya kaskazini. Mtazamaji anaweza kufuata mstari wa kudhaniwa kati ya Merak (β UMa) na Dhahari ya Dubu na atakuta nyota ya Kutubu kwa kuongeza umbali kati ya α UMa na β UMa mara tano.

Tanbihi hariri

  1. vipimo kufuatana na Lyubimkov, Leonid S.; et al. (February 2010)
  2. ling. Knappert 1993
  3. Waarabu wanatumia pia kifupi الدبة al-dubha ambayo ni jina mbadala kwa dubu na hili lilingia katika vitabu vya astronomia ya magharibi kama „Dubhe“
  4. Tooner (1984), Almagest , uk 344
  5. Naming Stars, tovuti ya Umoja wa Kimataifa wa Astronomia (Ukia), iliangaliwa Novemba 2017

Viungo vya Nje hariri


Marejeo hariri

  • Allen, Richard Hinckley: Star-Names and their Meanings; kwa G. E. Stechert New York, Leipzig, London, Paris 1899, ukurasa 437 (online kwenye archive.org)
  • Knappert, Jan: The Swahili Names of Stars, Planets and Constellations; The Indian Ocean Review September 1993 Volume 6 No. 3 September 1993, kurasa 6-7, ISSN 1031-2331
  • Guenther, D. B.; Demarque, P.; Buzasi, D.; Catanzarite, J.; Laher, R.; Conrow, T.; Kreidl, T. (2000). "Evolutionary Model and Oscillation Frequencies for α Ursae Majoris: A Comparison with Observations". The Astrophysical Journal. 530 (1): L45–L48. online hapa
  • Ptolemy's Almagest, translated and annotated by G.J. Toomer, London 1984, ISBN 0-7156-1588-2 online hapa