Jamhuri ya Texas ilikuwa sehemu ya Mexiko iliyojitenga mwaka 1836 na kuendelea kama nchi ya kujitegemea hadi mwaka 1845 ilipotekwa na Marekani na kuwa jimbo la Texas ndani ya Maungano ya Madola ya Amerika (USA).

Maeneo ya Jamhuri ya Texas; Kibichi cheusi: Maeneo yaliyotawaliwa halihali halisi Kibichi cheupe: Maeneo yaliyodaiwa kuwa sehemu ya Texas

Chanzo cha harakati ya kujitenga kilikuwa idadi ya walowezi kutoka Marekani waliopewa ardhi na serikali ya Mexiko katika miaka ya awali lakini baadaye hawakuwa tayari tena kukubali mamlaka ya Mexiko. Sababu mojawapo ilikuwa sheria ya Mexiko iliyowapa watumwa wote uhuru ilhali walowezi kutoka Marekani walianzisha mashamba wakiingiza watumwa Weusi kama wafanyakazi. Lakini uasi wa walowezi wa Texas ulianza wakati serikali ya Mexiko ilichukuliwa na jenerali Santa Anna aliyejitangaza kuwa dikteta na kufuta mamlaka ya serikali za kieneo. Mapigano yalianza wakati jeshi la Mexiko lilijaribu kukusanya silaha za wanamgambo wa Texas na hapo vita ilianza.

Katika mapigano ya kijeshi wanamgambo wa Texas walishinda jeshi la Mexiko na jenerali Santa Anna alipaswa kukubali uhuru wa Texas hata kama baadaye bunge la Mexiko lilikataa.

Hali halisi Texas ilikuwa nchi ya kujitegemea lakini dhaifu na idadi kubwa ya raia walipendelea kujiunga na Marekani. Mwaka 1845 rais wa Marekani James K. Polk aliamua kuteka Texas na kuifanya sehemu ya Marekani. Baadaye bunge la Marekani lilikubali Texas kuwa jimbo la kujitawala wa Maungano ya Madola ya Amerika.

Utekaji wa Texas ulikuwa chanzo cha vita ya Marekani na Mexiko ya 1846-1848 ambako Mexiko ilishindwa.