Magimbi, majimbi au nduma (Kiing. taro) ni kimoja ya vyakula vyenye asili ya sehemu ya chini ya shina la mimea fulani. Hupatikana sehemu mbalimbali duniani. Yanafanana na viazi au hata matunguu lakini huitwa mashinagimbi. Mmea wao huitwa mgimbi, mjembe, mjimbi au myugwa (Colocasia esculenta) unaoainishwa katika familia Araceae.

Majani ya magimbi
Magimbi sokoni

Magimbi hupendwa sana na watu, hasa kwenye msimu wa Ramadhani kama futari. Mara nyingi hupikwa kwa nazi. Na watu wa Unguja huita zege kwa sababu tu, chakula kitamu na ukila sana unavimbirwa haraka mno. Isitoshe hakiishi haraka tumboni. Kuna miundo mingi ya upishi wa magimbi, aidha kwa kuchemsha tu (chukuchuku) au utie na nazi (hasa kwa watu wa Pwani), yaani, Tanga, Mombasa, Kilwa, Zanzibar na kwingineko. Chakula hiki hakina tabia ya kuliwa sana katika miezi ya kawaida. Ndiyo maana upatikanaji wake wakati mwingine inakuwa vigumu kiasi. Kuna baadhi ya maneo hupatikana sana, lakini kwingineko inakuwa shida. Mara nyingi yanauzwa masokoni au katika masoko yasiyo rasmi, yaani, barabarani.

Colocasia esculenta inasemekana ina asili ya huko kusini mwa India na Asia ya Kusini, lakini vilevile huko ndiko hasa inakolimwa mno. Barani Afrika, Oceania na India Kusini ni chakula kikuu na huenda ikawa ni miongoni mwa vyakula vilivyowahi kulimwa tangu hapo awali. Vilevile inaaminika ya kwamba chakula hiki ni maarufu huko India, Nepal na Bangladesh, na kutoka huko kinaenea hadi Kusini mwa Asia, Mashariki ya Asia na Visiwa vya Pasifiki; magharibi hadi Misri halafu kusini kisha Mashariki na Magharibi mwa bara la Afrika. Kutoka huko yakaenea hadi huko visiwa vya Karibi na Amerika.

Viungo vya Nje hariri