Ruanda-Urundi ni jina la zamani kwa ajili ya nchi za Rwanda na Burundi. Zote mbili zilikuwa sehemu ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani hadi 1916. Wakatu wa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia jeshi la Force Publique la Ubelgiji kutoka Kongo lilivamia maeneo yake; katika ugawaji wa koloni ya Kijerumani maeneo yale yalikubaliwa na Uingereza kubaki upande wa Ubelgiji.

Mahali pa Ruanda-Urundi kando la Kongo ya Kibelgiji
Ramani ya Ruanda-Urundi wakati wa ukoloni
Wafanyakazi wahamiaji wa kiruanda katika mgodi wa Kisanga huko Katanga(Kongo ya Ubelgij)

Baadaye zilikabidhiwa na Shirikisho la Mataifa kama eneo la kudhaminiwa kwa Ubelgiji. Ubelgiji ilitawala nchi zote mbili kama eneo moja la "Ruanda - Urundi". Hali halisi ziliangaliwa kwa muda mrefu kama eneo la nyongeza la Kongo ya Kibelgiji. Lakini hali yake katika sheria ya kimataifa kuwa eneo la kudhaminiwa iliizuia kuunganishwa rasmi na koloni ile kubwa.

Nchi zote mbili zilitawaliwa kwa mfumo wa "utawala usio moja kwa moja" ihali Wabelgiji walitumia watawala wa jadi. Wafalme hao waliotwa Mwami walitoka kimapokeo katika kundi la Watutsi ilhali idadi kubwa ya wananchi walihesabiwa katika kundi la Wahutu. Makundi haya hayakuwa makabila tofauti maana walikuwa na lugha na utamaduni wa pamoja; walikuwa zaidi matabaka katika jamii ambayo yaliwahi kuanza karne kadhaa zilizopita kama makabila tofauti lakini zimeshaunganika kiutamaduni; hata hivyo yalikuwa tofauti kiuchumi kwa mkazo wa ufugaji upande wa Watutsi na ukulima upande wa Watutsi. Hata hivyo iliwezekana kwa Mhutu kupata ng'ombe wengi na kuitwa Mtutsi, na Mtutsi maskini kuanza kulima akitazamiwa kuwa Mhutu. Kisiasa tofauti ilisababishwa na mfumo wa utawala wa mwami (mfalme) aliyepaswa kuteuliwa kutoka familia za Watutsi.

Katika kipindi cha ukoloni uhusiano baina ya Watutsi na Wahutu ulibadilika kwa sababu wakoloni walitazama Watusi kuwa watu wa mbari wa juu. Waliimarisha tofauti kwa kuanzisha mfumo wa kuorodhesha na kutoa vitambulisho kwa wananchi ambako kila mtu aliandikishwa ama kama Mtutsi au Mhutu, na hivyo njia ya kuhama kundi ilifungwa. Wakipendelea Watutsi idadi ya Wahutu walioteuliwa kuwa mchifu wa maeneo ilipungua, hasa upande wa Rwanda.

Katika miaka ya 1950 elimu ya kisasa ilifanya Wahutu kudai haki za kisiasa sawa na Wahutu. Mwaka 1959 upinzani wa Wahutu dhidi ya utawala wa Watutsi uliendelea kwenye mapinduzi katika Rwanda ambako Mwami alipinduliwa na mauaji ya wapinzani wa kisiasa yalifanya Watutsi zaidi ya 100,000 kukimbia katika nchi jirani. Wakati huohuo uhusiano baina ya makundi ndani ya Burundi haukuonyesha mafarakano makali vile bado na mfalme wa Burundi alilenga kutengwa kwa Burundi na Rwanda.

Wakati wa mwisho wa utawala wa kikoloni kwenye mwaka 1961 sehemu zote mbili ziliachana na kuingia katika uhuru kama nchi mbili za Rwanda na Burundi. Burundi huru ilianza kama ufalme, ilhali Rwanda imeshakuwa jamhuri.

Kujisomea hariri