Sayari ya Tisa (pia Sayari Tisa, kwa Kiingereza Planet Nine) ni jina la muda kwa sayari isiyojulikana bado lakini inayoaminiwa kuwepo kwenye sehemu za nje kabisa za mfumo wa jua letu.

Wazo la mchoraji kuhusu Sayari Tisa; jua linaonekana kwa mbali sana, na mstari wa duaradufu ni njia ya sayari ya nane Neptun
Sayari Tisa imekadiriwa kufanana na sayari za rangi buluu kwenye picha hii ya mlingano wa ukubwa wa sayari za jua letu.

Hadi mwaka 2006 Pluto ilihesabiwa kama sayari ya tisa; lakini mwaka ule ufafanuzi mpya ulisababisha kuhesabiwa kwake kama "sayari kibete". Kwa hiyo sasa sayari inayoaminiwa kuwepo nje ya obiti ya Pluto huitwa "ya tisa".

Hadi sasa Sayari Tisa haijaonekana moja kwa moja, hivyo ni sayari ya kinadharia tete.

Sababu za kutunga nadharia tete ya Sayari Tisa

Kuwepo kwa sayari hii imependekezwa na wataalamu wa astronomia baada ya kutazama miendo ya ajabu katika kundi la magimba yaliyopo kwenye mpaka wa nje wa ukanda wa Kuiper; magimba hayo ni asteroidi na angalau sayari kibete moja. Hadi sasa magimba sita yametambuliwa ambayo obiti zake za kuzunguka jua hazifuati njia inayolingana na magimba mengine.

Walipotafuta kwa nini obiti hizo si za kawaida, wataalamu walianza kuwaza ya kwamba kuna kitu chenye masi kubwa kinachoathiri magimba hayo na kubadilisha njia zake. Awali mawazo yalitofautiana kama ni kitu kimoja au labda vitu viwili huko nje.

Historia ya uchunguzi na nadharia

  • Mwaka 2004: kutambuliwa kwa asteroidi au sayari kibete inayoitwa Sedna inayotembea nje ya Ukanda wa Kuiper kwenye umbali wa vizio astronomia 76 - 936 kutoka jua. Umbo la obiti yake lilistaajabisha watazamaji. Walitafuta sababu za Sedna kuwa na njia hii nje ya Ukanda wa Kuiper; sababu zilizotajwa zilikuwa nyota nyingine iliyowahi kupita karibu na jua letu au sayari nyingine huko nje isiyojulikana bado. [1][2][3]
  • Mwaka 2008: Hadi mwaka huo obiti nyingine za magimba ya ng'ambo ya Neptun zilitambuliwa zilizotembea nje ya obiti za kawaida. Mwanaastronomia wa Japani Tadashi Mukai na wenzake waliwaza kuwepo kwa sayari yenye ukubwa wa Dunia au Mirihi kwenye umbali wa vizio astronomia 100 hadi 200 .[4][5][6][7]
  • Mwaka 2012: Rodney Gomez wa Brazil alichungulia obiti za magimba nje ya Neptun akaona kundi lenye obiti zisizo za kawaida; akaunda kielelezo cha hesabu iliyoonyesha ya kwamba kuwepo kwa sayari yenye masi kati ya Mirihi na Neptun ikitembea mbali sana na jua kunaeleza umbo la obiti zisizo za kawaida.[8][9] Wataalamu wengine walisema ya kwamba alishindwa kuonyesha uthibitisho wa kuwepo kwa sayari huko nje.[10]
  • Mwaka 2014: Magimba mengine yanayofanana na Sedna na obiti yake yalitambuliwa. Ugunduzi huo uliongeza uwezekano wa kuwepo kwa sayari kubwa katika umbali ya nje.[11]
  • 2014 tena: Uchunguzi wa obiti 12 za mbali nje ya Neptun, na hasa kulinganisha kwa afeli na periheli zake, uliofanywa na Trujillo na Sheppard ulileta tokeo ya kwamba usumbufu wa obiti zao hauwezi kuelezwa na nguvu za graviti zilizopo ndani ya mfumo wa jua jinsi unavyoonekana hadi sasa, sharti kuwe na kitu nje. [12][13]

Kielelezo cha Sayari ya Tisa

Kufuatana na makadirio ya Konstantin Batygin na Michael E. Brown wa California Institute of Technology (Caltech) ya mwaka 2016, uwezekano wa kuwepo kwa Sayari ya Tisa ni mkubwa. Waliingiza data zote za obiti katika vielelezo vya kompyuta, wakafikia suluhisho la kwamba, kuwepo kwa sayari kubwa inayozunguka jua katika umbali mkubwa nje ya ukanda wa Kuiper kunaweza kueleza mambo yasiyo ya kawaida ya obiti zilizochunguliwa. [14]

Katika hesabu yao Sayari ya Tisa ingekuwa sayari jito ya gesi yenye masi takriban mara kumi kuliko dunia. Brown anawaza ya kwamba sayari itagunduliwa katika miaka mitano ijayo. [15] Kama ina masi hii na kama muundo wake unafanana na Uranus na Neptun, ni lazima sayari hii iwe na kipenyo mara 3.7 za dunia (km 46,600) na halijoto usoni ya K 47 (−226°C). [16]

Katika kielelezo obiti ya Sayari ya Tisa ingekuwa kabisa nje ya obiti ya Neptun.

Nadharia tete mbadala

Uwepo wa Sayari ya Tisa haujakubaliwa na wanaastronomia wote. Kuna nadharia mbadala. Zote zinakubali kuna kitu nje ambacho kutokana na graviti yake kinasumbua obiti za magimba zilizopimwa.

Magimba mengi yasiyotambuliwa bado

Ann-Marie Madigan na Michael McCourt wameangalia uwezekano wa kuwepo kwa ukanda wenye masi kubwa kushinda ukanda wa Kuiper huko nje ambao haujatambuliwa bado. [17][18]

Masi ya ziada isiyotambuliwa bado pamoja na Sayari Tisa

Matthew J. Holman na Matthew J. Payne kwenye Harvard–Smithsonian Center for Astrophysics walichungulia obiti ya Pluto wakaona mikengeuko mikubwa kushinda utabiri wa Batygin na Brown. Waliona njia tatu za kueleza tofauti hizo

  • inawezekana data zinazohusu obiti ya Pluto zina makosa makubwa
  • inawezekana bado kuna masi isiyotambuliwa ndani ya mfumo wa jua letu, kama vile sayari ndogo, pamoja na Sayari ya Tisa inayowezekana nje.
  • inawezekana kuna sayari iliyo ama kubwa zaidi au iko karibu zaidi na jua kuliko Sayari ya Tisa iliyotabiriwa na Batygin na Brown.[19]

Uhakiki

Uhakiki wa nadharia unahitaji kutambua Sayari ya Tisa au magimba mengine kwa vipimo. Hii haitakuwa rahisi. Sayari zinaonekana kwa sababu zinaakisia nuru ya jua. Katika umbali mkubwa vile ni nuru ndogo sana inayofika kutoka jua na kiasi kidogo zaidi kinachoweza kuakisiwa tena. Kwa hiyo ingeonekana kama nukta hafifu sana kwa darubini za astronomia. Njia ya pekee inategemea tabia ya sayari inayobadilisha mahali pake angani hata kama ni polepole, tofauti na nyota zinazokaa mahali pamoja. Hapa watazamaji wanapiga picha nyingi za maeneo wanayochungulia wanapoona mamilioni ya nyota. Sasa wanalinganisha kwa kompyuta kama kuna nukta za nuru zinazobadili mahali. Katika chaguo la sehemu wanapochungulia wanategemea utabiri zinazowezekana kutegemeana na vielelezo.

Uwezekano utategemea pia mahali pa Sayari ya Tisa kenye obiti yake - kama iko karibu na periheli yake itakuwa rahisi zaidi; kama iko karibu na afeli yake itakuwa vigumu zaidi.

  Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Sayari ya Tisa kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.

Marejeo

  1. Mike Wall (24 August 2011). "A Conversation With Pluto's Killer: Q & A With Astronomer Mike Brown". Space.com. Iliwekwa mnamo 7 February 2016.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)
  2. "Discovery of a Candidate Inner Oort Cloud Planetoid". The Astrophysical Journal 617 (1): 645–649. Bibcode:2004ApJ...617..645B. arXiv:astro-ph/0404456. doi:10.1086/422095. 
  3. Brown, Michael E. (28 October 2010). "There's something out there – part 2". Mike Brown's Planets.  Check date values in: |date= (help)
  4. Patryk S., Lykawka; Tadashi, Mukai (April 2008). "An Outer Planet Beyond Pluto and the Origin of the Trans-Neptunian Belt Architecture". The Astronomical Journal 135 (4): 1161–1200. Bibcode:2008AJ....135.1161L. arXiv:0712.2198. doi:10.1088/0004-6256/135/4/1161.  Check date values in: |date= (help)
  5. "Earth-Size Planet to Be Found in Outer Solar System?". 
  6. "Large 'Planet X' May Lurk Beyond Pluto". 
  7. "Japanese scientists eye mysterious 'Planet X'". Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2016-04-02. Iliwekwa mnamo 2016-05-06. 
  8. Natalie Wolchover (25 May 2012). "Planet X? New Evidence of an Unseen Planet at Solar System's Edge". LiveScience. Iliwekwa mnamo 7 February 2016. More work is needed to determine whether Sedna and the other scattered disc objects were sent on their circuitous trips round the sun by a star that passed by long ago, or by an unseen planet that exists in the solar system right now. Finding and observing the orbits of other distant objects similar to Sedna will add more data points to astronomers' computer models.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)
  9. Gomes, Rodney (2015). "The observation of large semi-major axis Centaurs: Testing for the signature of a planetary-mass solar companion". Icarus 258: 37–49. Bibcode:2015Icar..258...37G. doi:10.1016/j.icarus.2015.06.020. 
  10. "New Planet Found in Our Solar System?". 
  11. Ian Sample. "Dwarf planet discovery hints at a hidden Super Earth in solar system", 26 March 2014. 
  12. Christopher Crocket (14 November 2014). "A distant planet may lurk far beyond Neptune". Science News. Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 15 April 2015. Iliwekwa mnamo 7 February 2015.  Check date values in: |date=, |archivedate=, |accessdate= (help)
  13. David Dickinson (6 August 2015). "Stealing Sedna". Universe Today. Iliwekwa mnamo 7 February 2016.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)
  14. New evidence suggests a ninth planet lurking at the edge of the solar system, The Washington Post 2016-01-20, iliangaliwa 2016-01-21
  15. Evidence suggests huge ninth planet exists past Pluto at solar system’s edge, TheGuardian.com 20 Januari 2016, iliangaliwa 20  Januari 2016]
  16. Esther F. Linder, Christoph Mordasini (04 2016). "Evolution and magnitudes of candidate Planet Nine" (PDF). Astronomy & Astrophysics. arXiv:1602.07465. doi:10.1051/0004-6361/201628350. Iliwekwa mnamo 2016-04-08.  Check date values in: |date= (help)
  17. "Why Planet Nine might not exist". 
  18. "'Planet Nine'? Cosmic Objects' Strange Orbits May Have a Different Explanation". We need more mass in the outer solar system," she (Madigan) said. "So it can either come from having more minor planets, and their self-gravity will do this to themselves naturally, or it could be in the form of one single massive planet — a Planet Nine. So it's a really exciting time, and we're going to discover one or the other. 
  19. Kigezo:Cite arXiv