Uhai (kutoka neno la Kiarabu; pia uzima; kwa Kiingereza: life) kwa maana ya biolojia ni jumla ya tabia zinazotofautisha kiumbehai na mata kwa jumla. Hata hivyo kila uhai ulioweza kuchunguzwa na sayansi unapatikana pamoja na mata.

Kati ya tabia hizo kuna uwezo wa kushawishiwa na mazingira, kujipanga, kukua, metaboli na kuzaa. Kila tabia peke yake haifanyi uhai, kwa sababu mojamoja zinaweza kutokea pia kwa mata isiyo hai: fuwele zinakua, ulimi wa moto una umbo maalumu na ndani yake kuna aina ya metaboli inayobadilisha molekuli za nta pamoja na oksijeni ya hewani dioksidi kabonia na maji. Kwa hiyo ni jumla ya tabia zinazothibitisha uwepo wa uhai, lakini hadi leo wataalamu hawajapatana bado ni masharti gani yanayohitajika, kwa sababu kuna tofauti kati ya viumbehai ambazo hazifanani katika tabia zote kwa pamoja.

Uhai unapatikana kwa umbo la viumbehai wanaopangwa katika vikundi vinavyofanana kati yao. Kila kiumbehai hufanywa na vitengo hai ndani yake vinavyoitwa seli.

Dunia kama mahali pa uhai hariri

Dunia yetu ni sayari pekee inayojulikana mpaka sasa ambapo binadamu na viumbehai vingine wanaweza kuishi.

 
Nyumba ni moja ya sehemu ya kuishi kama jamii.

Kuna sababu mbili:

  1. dunia yetu ina umbali na jua unaofaa kwa maisha kwa sababu sayari zilizoko karibu zaidi na jua (k.m. Zuhura) zina joto kubwa mno na sayari zilizoko mbali zaidi kama Mrihi ni baridi mno.
  2. dunia yetu ina angahewa yenye asilimia 78 ya naitrojini, asilimia 21 ya oksijini na asilimia 1 ya aina nyinginezo za hewa, na kwa sababu hii uhai na maisha yanamakinika katika ardhi, kinyume na sayari nyinginezo.

Asili ya uhai na uenezi wake hariri

Inakadiriwa kwamba dunia ina miaka bilioni 4.54, na kwamba uhai uliweza kujitokeza juu yake walau miaka bilioni 3.5 iliyopita, baada ya ganda la la nje la dunia ilikauka. Ushahidi wa zamani zaidi ulipatikana huko Greenland (mabaki ya viumbe hai wa miaka bilioni 3.7 iliyopita). Hata hivyo wataalamu wengine wanakadiria miaka bilioni 4.25 na hata 4.4 iliyopita.

Jinsi uhai ulivyoweza kuanza haijajulikana, ingawa zimependekezwa dhana mbalimbali.

Hakika, baada ya kuanza, uhai umejitokeza kwa namna nyingi sana ambazo zimeainishwa na wanabiolojia.

Uhai umeweza kustawi au kudumu katika mazingira tofauti sana, lakini zaidi ya 99% za spishi zote zilizowahi kutokea (zaidi ya bilioni 5) kwa sasa zimetoweka.

Makadirio kuhusu zile zilizopo yanataja spishi milioni 10 hadi 14: kati ya hizo, milioni 1.2 tu zimechunguzwa, wakati zaidi ya asilimia 90 bado.

Tazama pia hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya biolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Uhai kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.