Wallah bin Wallah (alizaliwa 1952) ni mwandishi wa Kiswahili kutoka Kenya anayetambulika kwa jina la Ustadh (profesa) kwa hatua zake katika kuimarisha lugha ya Kiswahili katika jamii ya Afrika Mashariki.

Mwalimu Wallah bin Wallah ameandika vitabu vya Kiswahili Mufti na Insha Mufti vinavyotumika katika shule za msingi.

Wallah alianzisha wakfu ya tuzo za Wasta mwaka 2010 ambazo anawatuza wanaojitahidi kukitumia Kiswahili kwa umakini.

Utoto wake na elimu hariri

Wallah bin Wallah alizaliwa mwakani 1952 kule Nyakach, wilaya ya Nyando[1]. Jina alilopewa na wazazi wake lilikuwa Ndedah lakini alilibadilisha baadaye maana aliliona kana kwamba lilikuwa likimsaliti kama mkabila. Alilichukua jina la babake Wallah na baadaye akaona ni vyema kujiita Wallah mwanawe Wallah. Hivyo, jina Wallah bin Wallah likakita mizizi. Wallah alisomea nchini Tanzania maana alifuatana na babake aliyekuwa akifanya kazi na kampuni ya reli ya Afrika Mashariki huko Tanzania. Alijiunga na shule ya msingi la Lukungu alikosomea kutoka darasa la kwanza hadi la nne. Baadaye alijiunga na shule ya Bukumbu alikosomea hadi darasa la saba na kuhitimu katika mtihani wa G.E.E.

Maisha ya Wallah shuleni hayakuwa mepesi maana babake hakuwa akimpa msaada na mara kwa mara, Wallah alijilipia karo. Alifanya hivi kwa kuchuuza samaki pamoja na kuwanyoa wenzake ili apate pesa. Baada ya shule ya msingi, alijiunga na shule ya seminari ya Nyegezi ambako alikuwa akisomea somo la dini ya Kikristo. Hakumaliza hayo masomo maana aling'amua kwamba kama angetaka kuendeleza ujuzi wa Kiswahili, alifaa awe Muislamu. Aliacha shule na kurudi Kenya alikojiunga na shule ya upili ya Ravals, Latema. Aliweza kupata diploma ya ualimu katika chuo cha Morogoro Teachers' College mwakani 1976.

Baada ya shule, Wallah alianza kazi ya ualimu wa Kiswahili. Akiendelea kufunza katika shule mbalimbali Kenya kama vile Misiani Girls, Moi Girls Isinya, aliweza kufanya shahada ya Kiswahili na Kiarabu. Baadaye, aliendeleza uchu wake wa kukikujua Kiswahili kwa kufanya Shahada ya Uzamili katika chuo cha Dar es Salaam.[2].

Vitabu vyake vya shule vimekosolewa kwa makosa ya kilugha, kama kutoeleza sahihi matumizi ya saa na wakati[3]

Vitabu hariri

Wallah bin Wallah ameandika vitabu vya Kiswahili Mufti vinavyotumiwa katika shule za Msingi. Pia ameandika kitabu cha Insha Mufti ambacho kinawezesha wanafunzi kuandika insha nzuri. Chemsha Bongo ni kitabu kingine ambacho Wallah alikiandika kwa madhumuni ya kutayarisha wanafunzi wanapojiandaa kuufanya mtihani wa Mwisho shuleni za msingi Kenya.

Wallah pia ameandika vitabu vya hadithi fupi kama vile:

  • Mbwa wa Majini
  • Tumgidie Bwege
  • Sitaki Simu
  • Kicheko Cha Maiti
  • Zawadi Ya Sanda,
  • Kifo Cha Wema
  • Kitanzi cha Utandawizi
  • Simtu
  • Moto Wa Maisha
  • Uongo wa Ukweli
  • Mitego ya Wendawazimu

Pamoja na vitabu vinginevyo ambavyo vyote vimechapishwa na shirika la Maxwell Publishers.

Viungo vya nje hariri

  1. All about Wallah bin Wallah the author of Kiswahili mufti,tovuti ya litratureafrica ya 2013
  2. The teacher who became Kenya’s highest earning author, gazeti la Nation, Kenya Saturday March 23 2013
  3. Kiswahili cha Wallah Bin Wallah: Ni Mufti Kweli?, blogu ya Shiku Ngigi, ya tar. 2014
  Makala hii kuhusu mwandishi fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wallah bin Wallah kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.