Wamuwahidun (kwa Kiing.: Almohad kutoka Kiarabu: al-muwahhidun, yaani "Wanaomwamini Mungu mmoja") walikuwa nasaba ya Waberberi Waislamu waliotawala Afrika ya Kaskazini kutoka bahari Atlantiki hadi Libya pamoja na Al-Andalus yaani kusini mwa Hispania.

Bendera ya Almuwahidun 1121 - 1269
Ukhalifa wa Wamuwahidun (nyekundu)

Historia hariri

Wamuwahidun walianza kama kundi la wafuasi wa Ibn Tumart aliyekuwa mtaalamu wa Kiislamu na mhubiri kutoka Waberberi wa Moroko kusini. Katika mahubiri yake alikosoa yale aliyoyaona kama makosa na dhambi ya Waislamu katika himaya ya Wamurabitun; baada ya kufukuzwa mara kadhaa katika miji yao hatimaye mwaka 1121 alitangaza ufunuo wa wito wake kuwa mahdi. Tangu mwaka uliofuata aliongoza mashambulio dhidi ya jeshi na wawakilishi wa watawala Wamurabitun. Mwaka 1130 alijaribu kushambulia mji mkuu Marakesh lakini alishindwa akafa miezi michache baadaye.

Nafasi yake ilichukuliwa na Abd al-Mu'min al-Kumi. Kuanzia mwaka 1130 hadi kifo chake mnamo 1163, Abd al-Mu'min al-Kumi kutoka kabila la Waberberi Masmuda, alishinda watawala wa Almurabitun (Almoravid) na kuwa mtawala juu ya Afrika kaskazini yote hadi Libya. Alikuwa Amiri wa Marakesh mnamo 1149 akavamia na kutwaa Al-Andalus yaani sehemu ya kusini ya Hispania iliyokaliwa na Waislamu wengi wakati ule.

Makhalifa wa kwanza wa Wamuwahidun walionyesha ukali dhidi ya raia wasio Waislamu. Wayahudi na Wakristo walipewa miezi saba halafu kuamriwa kugeukia Uislamu[1]. Wayahudi na Wakristo walipata hivyo kuwa na mashahidi walioamua kutoacha ungamo lao badala ya kusilimu. Upande wa Wakristo mashahidi wafuatao wanakumbukwa katika enzi ya Wamuwahidun:

 
Kifodini cha Watakatifu Danieli na wenzake.

Mnamo 1170 Wamuwahidun walihamishia mji mkuu wao kwenda Sevilla. Lakini kufikia mwaka 1212 Muhammad III, "al-Nasir" (1199-1214) alishindwa na muungano wa wafalme wanne wa Kikristo wa Kastilia, Aragon, Navarra na Ureno. Wamuwahidun walipoteza karibu maeneo yote ya Kiislamu huko Iberia.

Miji mikubwa ya Cordoba na Sevilla ilianguka katika mikono ya Wakristo katika nusu ya kwanza ya karne ya 13.

Wamuwahidun waliendelea kutawala Afrika kwa muda, lakini walipoteza sehemu kubwa ya eneo lao. Mtawala wa mwisho wa nasaba hiyo, Idris II, alikuwa amebaki na Marakesh pekee. Huko aliuawa na mtumwa mnamo 1269.

Makhalifa wa Muwahidun (Almohad), 1121-1269 hariri

 
Mnara wa Alhomad huko Safi
 
Ramani inayoonyesha eneo la udhibiti wa Wamuwahdun huko Hispania na mashambulio kutoka Kastilia (C) na Aragón (A). ((L) Leon, (P) Ureno, (N) Navarra)
  • Ibn Tumart 1121-1130
  • Abd al-Mu'min 1130-1163
  • Abu Ya'qub Yusuf I 1163–1184
  • Abu Yusuf Ya'qub al-Mansur 1184–1199
  • Muhammad an-Nasir 1199-1213
  • Abu Ya'qub Yusuf II 1213-1224
  • Abd al-Wahid mimi 1224
  • Abdallah al-Adil 1224-1227
  • Yahya 1227-1235
  • Idris I 1227-1232
  • Abdul-Wahid II 1232-1242
  • Ali 1242–1248
  • Umar 1248-1266
  • Idris II 1266-1269


Usanifu wa wakati huo hariri

Chini ya Wamuwahidun usanifu wa Kiislamu uliona maendeleo makubwa katika ujenzi wa misikiti, madrasa, vyuo, nyumba na majengo mengine. Mbinu mbalimbali za kupamba majengo zilibuniwa zinazoendelea hadi leo katika usanifu wa Moroko.

Picha hariri

Waandishi wa wakati huo hariri

Waandishi wa Usufii:

  • Sidi Abu Madyan Choaïb ben al-Houssein al-Ansari (1126-1198)
  • Ali ibn Harzihim (m. 114)
  • Abi Mohammed Salih (1153-1234)
  • Abu Abdallah ibn Harzihim (m. 1235)
  • Abu-l-Hassan ash-Shadhili (1197-1258)
  • Abdelwahid al-Marrakushi (b. 1185) mwanahistoria na mwandishi
  • Salih ben Sharif al-Rundi (1204-1285)

Tanbihi hariri

  1. Amira K. Bennison and María Ángeles Gallego. "Jewish Trading in Fes On The Eve of the Almohad Conquest." MEAH, sección Hebreo 56 (2007), 33–51

Marejeo hariri

  • History of the Almohades, Reinhart Dozy, (toleo la pili, 1881)
  • Mica Enciclopedie de Istorie Universala, Marcel D. Popa, Horia C. Matei, (Bucharest, Editura Politica 1988)

Viungo vya Nje hariri