Zimbabwe African National Liberation Army

Zimbabwe African National Liberation Army (ZANLA) ilikuwa mkono wa kijeshi wa chama cha Zimbabwe African National Union (ZANU) katika vita ya msituni ya Rhodesia iliyoleta uhuru wa Zimbabwe. Ilipigana na jeshi la Rhodesia Kusini pamoja na jeshi la ZIPRA ingawa pande zote mbili zilifuata itikadi tofauti na wakati mwingine kupigana kati yao.

ZANLA ilianzishwa mwaka 1965 huko Tanzania na hadi 1970 hivi makambi yake yalikuwa nje ya Rhodesia Kusini katika Zambia. Baadaye vikosi vyake vilikaa hasa Msumbiji.

Kiongozi wa kwanza wa ZANLA alikuwa Herbert Chitepo aliyefuatwa na Josiah Tongogara kuanzia 1973 hadi kifo chake 1979. Ilhali vita ilieleka kuisha Robert Mugabe alichukua uongozi aliyewahi kuongoza mkono wa kisiasa, yaani ZANU.

Mwanzoni ZANLA ililenga kushambulia jeshi la Rhodesia lakini kuanzia 1972 ilitumia mbinu za vita ya msituni kwa kufuata mfano wa wanamgambo wa Mao Tse Tung; mbinu hizi ziliwahi kutumiwa na jeshi la FRELIMO pale Msumbiji: kupeleka wanamgambo vijijini kwa siri, kufundisha wakulima na kutafuta wanamgambo wapya kati yao na kupanga mashambulio madogo.

ZANLA ilipata msaada kutoka China pamoja silaha na walimu wa kijeshi na kisiasa.[1]

Mugabe mwenyewe aliwahi kujitambulisha kuwa "Mfuasi wa Umarx-Ulenin upanda wa Mao" hivyo ZANLA na ZANU hawakupokea usaidizi kutoka Urusi iliyosaidia pekee jshi la ZIPRA.[2]

Itikadi ya ZANLA na ZANU ilipangwa kufuatana na mafundisho ya ukomomunisti wa Kichina kwa hiyo walijitazama kama kikosi cha mbele kitakachoongoza wananchi kuelekea mapinduzi. Ukosoaji ndani ya chama haukuvumiliwa.[3]:6 Mwanahistoria wa Afrika Kusini, Sabelo Ndlovu-Gatsheni aliona ZANLA kuwa na muundo ambako takaso za kisiasa (ziliitwa kwa neno la Kishona "gukurahundi") ambako maafisa waliuawa zilitokea mra kwa mara na maafisa yake walitakiwa kutekeleza amri zozote bila kuonyesha mashaka.[3]:6 Kiongozi mmoja wa ZANLA Edson Zvobgo alitaja kuwa "itikadi ya bunduki" ilikuwa suluhisho bora kwa kuondoa matatizo na maafisa wa ZANU wawe tayari kufyeka maadui wote wa chama.[3]:12 Mauaji ya maafisa waliotofautiana na siasa rasmi ya uongozi yalitokea mara kwa mara.[3]:12

ZANLA ilishirikiana karibu na FRELIMO wa Msumbiji. Kuanzia 1972 makambi yake makuu yalikuwepo kwenye Mkoa wa Tete katika kaskazini ya Msumbiji. Baada ya uhuru wa Msumbiji 1975 ZANLA iliruhusiwa kutumia makambi kote kwenye mpaka baina ya Rhodesia na Msumbiji.

ZANLA na ZIPRA hariri

ZANLA haikuwa jeshi la kupigania uhuru pekee, kundi lingine muhimu ilikuwa Zimbabwe People's Revolutionary Army (ZIPRA). ZIPRA ilikuwa mkono wa kijeshi wa chama cha Zimbabwe African People's Union (ZAPU). Kiasili viongozi wa ZANU/ZANLA walikuwa wanachama wa ZAPU hadi farakano kwenye mwaka 1963. Tofauti kuu zilikuwa:

  • ZANLA ilipata msaada wake hasa kutoka China na kuwa na makambi yake Msumbiji, ilhali ZIPRA ilisaidiwa na Urusi na kuwa na makambi pale Zambia na Angola
  • ZANLA ilikuwa na wanamgambo hasa kutoka Washona, ambao ni kabila kubwa la Zimbabwe, ZIPRA ilikuwa hasa na wapiganaji kotoka Wandebele.
  • ZANLA ilifuata itikadi ya kuingia kwa siri kati ya wakulima na kufanya mashambulio madogomadogo kufuatana na mafundisho ya Mao Tse Tung. ZIPRA iliunda vikosi vilivyofanana na jeshi la kawaida, ilivamia Rhodesia mara kadhaa, kushambulia jeshi lake na kurudi tena katika makambi yake ng_ambo ya mpaka.

Katika miaka ya mwsho wa 1970 kulitokea mara kadhaa mapigani baina ya wapiganaji wa ZANLA na ZIPRA ndani ya Rhdesia-Zimbabwe.

Baada ya mapatano ya Lancaster House na uchaguzi huru wa kwanza sehemu za ZANLA waliingizwa katika Jeshi la Zimbabwe pamoja na askari wa jeshi la awali la Rhodesia na askari wa ZIPRA. Lakini serikali ya Zimbabwe huru haikupanga njia kwa wapiganaji wengi wa uhuru waliorudi katika maisha ya umaskini. Wengi walijiunga na Chama cha wanajeshi wastaafu na wakongwe wa vita ya uhuru; kuanzia mwaka 1990 hivi walianza kuvamia mashamba ya kibiashara yaliyokuwa bado mkononi mwa masetla Wazungu.

Marejeo hariri

  1. Mutanda, Darlington (2017). The Rhodesian Air Force in Zimbabwe's war of liberation, 1966-1980. Jefferson, North Carolina: McFarland & Company, Inc., Publishers. p. 177. ISBN 978-1476666204. 
  2. Andrew, Christopher; Gordievsky, Oleg (1990). KGB : the inside story of its foreign operations from Lenin to Gorbachev. New York, NY: HarperCollinsPublishers. p. 465. ISBN 9780060166052.  Unknown parameter |url-access= ignored (help)
  3. 3.0 3.1 3.2 3.3 Ndlovu-Gatsheni, Sabelo J. (18 October 2013). "Rethinking Chimurenga and Gukurahundi in Zimbabwe: A Critique of Partisan National History". African Studies Review 55 (03). doi:10.1017/S0002020600007186. 

Kujisomea hariri