Kambi za KZ

(Elekezwa kutoka Makambi ya KZ)

Kambi za KZ ni jina la kutaja kambi za wafungwa yaliyotumiwa hasa na Ujerumani wakati wa utawala wa Wanazi miaka 1933 hadi 1945. "KZ" ni kifupi cha neno la Kijerumani "Konzentrationslager". Maana yake ni "Kambi ya kukusanya wafungwa" (Kiingereza: concentration camp).

Wafungwa katika kambi ya KZ
Makambi ya KZ chini ya Ujerumani wa Nazi miaka 1933-1945;
makambi ya mauti yamepewa alama nyekundu

Wanazi walianzisha hizo kambi za KZ baada ya kuteka Ujerumani mwaka 1933. Walikamata wapinzani wao wengi, kiasi kwamba magereza hayakutosha tena. Kambi hizo hazikuwa tena chini ya wizara ya sheria bali chini ya polisi ya kisiasa na vitengo vya chama cha Nazi. Tangu mwaka 1934 zilikuwa zote chini ya kikosi cha SS.

Wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia zilitumiwa kukusanya mamilioni ya watu waliokamatwa na Wanazi kote Ulaya, hasa vikundi viwili:

  • Wayahudi pamoja na vikundi vingine vilivyobaguliwa upande mmoja na
  • wapinzani wa utawala wa Nazi kwa upande mwingine.

Kambi za KZ za kawaida hariri

Kambi hizo zilikuwa hasa na kusudi la kuadhibu wapinzani na kutumia wafungwa kwa ajili ya kazi za kulazimishwa. Hasa wakati wa vita Wajerumani wengi walikuwa wanajeshi na nchi ikaona uhaba wa wafanyakazi. Hivyo kambi hiza zilijengwa mara nyingi karibu na viwanda.

Idadi ya vifo ilikuwa kubwa hasa katika miaka ya mwisho ya vita kutokana na unyama wa walinzi na uhaba wa chakula pamoja na ukosefu wa matibabu. Njaa ilisababisha magonjwa na vifo vingi.

Wafungwa katika kambi ya KZ Buchenwald wakati wa ukombozi mwaka 1945.

Makambi ya mauti hariri

Baada ya azimio la kuanzisha Maangamizi makuu dhidi ya Wayahudi wa Ulaya serikali ya Ujerumani ilijenga kambi za mauti kwa kusudi la kuua Wayahudi wengi iwezekanavyo pamoja na vikundi vingine.

Kambi za mauti ni lugha ya kutaja hasa Kambi saba zifuatazo:

Zote zilijengwa nje ya eneo la Ujerumani wenyewe, sita katika Poland na moja katika Belarusi.

Mwisho wa mwaka 1941 Adolf Hitler na viongozi wengine wa Ujerumani waliamua kuwaua Wayahudi wote waliopatikana Ulaya. Majaribio ya kwanza ya kuua Wayahudi katika Ulaya ya Mashariki yalionyesha matatizo mbalimbali: uchovu kwa upande wa wanajeshi wa vikosi maalumu waliopaswa kutekeleza mauaji haya ya watu kwa maelfu na sauti za masikitiko upande wa wanajeshi wa kawaida waliobahatika kuona mauaji hayo. Azimio lilifanywa la kutumia mbinu za kisasa katika kambi maalumu ambako tendo lenyewe liliweza kufichwa vizuri zaidi.

Wayahudi na wengine waliotakiwa kuuawa walipelekwa kwa treni hadi kambi hizo maalumu. Huko wafungwa waligawiwa katika makundi:

  • watu wenye afya nzuri walipelekwa kando na kupewa kazi katika viwanda vilivyojengwa pamoja na makambi haya kwa kusudi la uzalishaji kwa ajili ya mahitaji ya uchumi wa vita. Wafanyakazi hao walitakiwa kufanya kazi ngumu wakipewa chakula kidogo hadi kuchoka. Mara walipokuwa hawaleti tena faida walipelekwa kuuawa kwenye chumba cha gesi.
  • watoto, wazee na wagonjwa walipelekwa kando mara moja hadi vyumba vilivyoitwa "bafu". Hapo milango ilifungwa, na gesi ya sumu kuingizwa. Maiti zilichomwa katika majiko makubwa.

Kwa jumla watu milioni sita waliuawa katika kambi za KZ hadi mwaka 1945.

Jina la "KZ" hariri

Wanazi walitumia jina la KZ = "Konzentrationslager" kama tafsiri ya neno la Kiingereza "concentration camp". Waingereza waliwahi kutumia mbinu ya kusimamia wafungwa wengi katika kambi maalumu zilizofungwa kwa seng'enge tangu vita yao dhidi ya Makaburu katika Afrika Kusini miwaka 1899-1902; Waingereza walianzisha kambi hizo kwa sababu walitaka kutenganisha familia za Makaburu na wanaume wao walioendesha vita vya porini ili kuzuia wasipate chakula na usaidizi kutoka kwa wasio wanajeshi. Kambi hizo zilisababisha vifo vya wanawake, watoto na wazee kwa makumi elfu kutokana na njaa na magonjwa ingawa hayakujengwa kwa kusudi hilo.

Tangu kuanzishwa na Waingereza huko Afrika Kusini imeonekana ya kwamba kambi za aina hiyo husababisha mara nyingi vifo hata kama wale wanaoanzisha makambi hawana nia ya kuua watu kwa njia hiyo. Matatizo ya kulisha watu wengi mahali pamoja, ya kuhakikisha usafi na matibabu ama shambani tu au katika mahema au kwenye majengo yasiyo imara, kuwalinda wafungwa dhidi ya baridi na joto na juu ya haya yote kuzuia kuambukizana kwa magonjwa ni magumu ya kushinda uwezo wa walinzi wa kambi. Hasa kama wafungwa wanatazamwa kama maadui ambao hawapaswi kupewa uangalizi mwingi.

Tazama pia hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kambi za KZ kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.