Ofisi ya Taifa ya Takwimu ya Tanzania

Ofisi ya Taifa ya Takwimu ya Tanzania (kifupi: OTTT; kwa Kiingereza: Tanzania National Bureau of Statistics) ni shirika rasmi la takwimu nchini Tanzania.

Utangulizi:

1.0         Ofisi ya Taifa ya Takwimu Kabla ya Uhuru Mpaka Kuwa Wakala wa Serikali

Shughuli za kitakwimu kabla ya Uhuru wa Tanganyika, zilifanyika kwa kutumia Sheria ya Takwimu Sura ya 443 ya Mwaka 1949 (Statistics Ordinance of 1949 – Chapter 443). Sheria hii ilikuwa inatumika katika nchi zilizotawaliwa na wakoloni za Afrika Mashariki ambazo ni Kenya, Uganda na Tanganyika. Makao Makuu ya Ofisi yalikuwa Nairobi, Kenya. Aidha, kupitia Sheria hiyo, Idara ya Takwimu ya Afrika Mashariki ilipewa mamlaka ya kuratibu mfumo na muundo wa takwimu za uchumi na jamii wa nchi zote tatu.


Baada ya Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961, Ofisi hii ilijulikana kama Idara Kuu ya Takwimu (Central Bureau of Statistics) ambayo Makao Makuu yalikuwa Dar es Salaam. Aidha, katika kipindi tajwa, Ofisi ilikuwa ikifanya kazi chini ya Sheria ya Takwimu, Sura ya 443 ya Mwaka 1961 (Statistics Ordinance Cap. 443 of 1961).


Mnamo tarehe 26 Machi, 1999 jina la Ofisi hii lilibadilika kuwa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (National Bureau of Statistics-NBS) kutokana na kuzinduliwa kuwa Wakala wa Serikali (Executive Agency) kupitia Sheria ya Wakala wa Serikali Na. 30 ya Mwaka 1997.  NBS ina ofisi za mikoa katika mikoa yote ya Tanzania Bara.


Mara baada ya kuwa Wakala wa Serikali, NBS ilikuwa chini ya  Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango na iliendelea kufanya kazi na majukumu yake kwa Sheria ya Takwimu Sura ya 443 ya Mwaka 1961 (Statistics Ordinance Cap. 443 of 1961) hadi mwaka 2002, ilipofutwa kwa Sheria ya Takwimu Sura ya 351 ya Mwaka 2002. Kutokana na Sheria hiyo, NBS ilipewa majukumu ya kuendesha, kusimamia na kuratibu shughuli zote za takwimu rasmi Tanzania Bara na kwa suala la Sensa ya Watu na Makazi, Ofisi ya Taifa ya Takwimu hushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali-Zanzibar.


1.1       Ofisi ya Taifa ya Takwimu kama Taasisi Inayojitegemea

Kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu Sura 351, Ofisi ya Taifa ya Takwimu ni taasisi ya Serikali inayojitegemea. Ofisi hii ipo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango. Kufuatia Makao Makuu ya Serikali kuhamishiwa rasmi Dodoma, Makao Makuu ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu yalihamia mkoani Dodoma mwezi Agosti, 2018.


1.2                  Dira

Dira ya NBS ni “kuwa kitovu cha takwimu rasmi Tanzania”.

1.3                  Dhamira

Dhamira ya NBS ni “Kutoa takwimu rasmi zilizo bora na huduma zinazokidhi mahitaji ya wadau wa kitaifa na kimataiafa kwa ajili ya kupanga mipango na kutoa maamuzi sahihi”.


2.0       Majukumu ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu

Kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu, jukumu la msingi la Ofisi ya Taifa ya Takwimu ni kuzalisha, kuratibu, kusimamia na kusambaza takwimu rasmi na kuwa mhifadhi/mtunzaji mkuu wa takwimu rasmi nchini. Katika kutekeleza majukumu yake ya kisheria, Ofisi ya Taifa ya Takwimu inafanya kazi zifuatazo:


2.1    Kufanya Tafiti Mbalimbali za Kijamii na Kiuchumi

       Ofisi ya Taifa ya Takwimu imeendelea kufanya tafiti mbalimbali ili kutoa viashiria vya kijamii na kiuchumi kwa ajili ya kutathmini utekelezaji mipango ya maendeleo ya kitaifa na kimataifa. Tafiti za Kijamii ni kama Utafiti wa Afya ya Mama na Uzazi (TDHS); Utafiti wa Viashiria vya Ukimwi na Malaria Tanzania na Utafiti wa Mapato na Matumizi ya Kaya Binafsi (HBS). Aidha, Tafiti za Kiuchumi ni pamoja na Sensa ya Viwanda, Utafiti wa Biashara na Ujenzi (Integrated Business Survey), na Sensa ya Kilimo (Agricultural Censuses).


2.2    Kufanya Sensa ya Watu na Makazi kwa Kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Zanzibar

       NBS hufanya Sensa ya Watu na Makazi kila baada ya miaka kumi kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar. Aidha, Sensa ya Watu na Makazi ijayo inatarajiwa kufanyika mwaka 2022.


2.3    Kutoa Takwimu za Msingi (Core Statistics)

       Pamoja na tafiti mbalimbali ambazo huwa zinafanyika, Ofisi ya Taifa ya Takwimu hutoa Takwimu za Msingi katika maeneo muhimu ya uchumi kama ifuatavyo:

(a)       Pato la Taifa

        Takwimu za Pato la Taifa zinatolewa kila robo mwaka (Quarterly Gross Domestic Product – GDP) na kwa kila mwaka (Annual Gross Domestic Product) na Pato la Taifa Kimkoa (Regional Gross Domestic Product).

(b)       Takwimu za Kilimo

        Takwimu za Kilimo na Mifugo kama vile Sensa na Utafiti wa Kilimo (Agricultural Sample Surveys).

(c)       Takwimu za Viwanda na Ujenzi

        Takwimu za Uzalishaji Bidhaa Viwandani, na Takwimu za Fahirisi za Bei za Uzalishaji (Producer Price Index) ambazo hukusanywa kwa robo mwaka, Utafiti wa kila mwaka wa Uzalishaji wa Viwandani na Sensa ya Viwanda.

(d)       Takwimu za kila mwaka za Biashara, Usafirishaji , Utalii na Uhamiaji (Trade, Transport, Tourism and Migration).

(e)       Mfumuko wa Bei

        Mfumuko wa Bei kwa kila mwezi hutolewa kila tarehe 8 ya mwezi unaofuata ili kupima kasi ya mwenendo wa bei za bidhaa na huduma mbalimbali zinazotumika katika kaya binafsi. 

(f)        Takwimu za Ajira

Ofisi ya Taifa ya Takwimu imeendelea kukusanya takwimu za ajira kwa kutumia vyanzo vifuatavyo:

       i.  Utafiti wa Watu wenye Uwezo wa Kufanya kazi (Integrated Labour Force Survey). Utafiti huu umekuwa ukifanyika kila baada ya miaka mitano.

ii.   Utafiti wa Ajira na Mapato (Employment and Earnings Survey) hufanyika katika sekta rasmi kwa mikoa yote Tanzania Bara. Utafiti huu umekuwa ukifanyika kila mwaka;

  iii.    Utafiti wa Sekta Isiyo Rasmi


(g)       Wasifu wa Kiuchumi na Kijamii wa Mikoa na Wilaya (Regional and District Social Economic Profiles)

Uandaaji wa taarifa hizi hufanywa na NBS kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

(h)       Takwimu za Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi

Makala hii kuhusu "Ofisi ya Taifa ya Takwimu ya Tanzania" ni fupi mno. Inahitaji kupanuliwa mapema.