Haruna Taratibu alikuwa mzalendo muasisi wa TANU Jimbo la Kati (Central Province) mnamo 1954 - Dodoma. Sifa kuu katika ujumbe wa Nyerere ilikuwa ni kule kueleweka kwa mantiki yake na kuweza kuwavutia wananchi wa kawaida. Hawa ndiyo walikuwa watu walioyageuza majumba yao kuwa ofisi za TANU, wakafanya kampeni kupata wanachama, wakauza kadi za TANU, na katika kufanya hivyo wakahatarisha maisha yao.

Kushoto: Iddi Faiz Mafungo, Sheikh Mohamed Ramia, Julius Nyerere, Saadan Abdu Kandoro na Haruna Taratibu.

Historia ya harakati za uhuru hariri

African Association mjini Dodoma ilikuwa ikiongoza katika harakati baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Ilikuwa na wanasiasa wenye juhudi sana na wabunifu kuliko wanasiasa wengine wote waliopata kutokea katika historia ya Tanganyika. Wanasiasa hawa walikuwa Ali Ponda, Mmanyema na Hassan Suleiman, Myao, rais na katibu wake. Mwaka 1945 Ali Ponda alitoa wito kwa Waafrika wote kuungana kama umma mmoja. Lakini kuanzia mwaka 1948 harakati za siasa mjini Dodoma zilififia, na TANU ilipoanzishwa mnamo Julai, 1954, tawi la TAA Dodoma lilikuwa limedorora kiasi kwamba kilishindwa hata kupeleka mjumbe kwenye mkutano ule wa TAA wa kuundwa kwa TANU.

Pamoja na ukweli kuwa mji wa Dodoma kulikuwa na Kikuyu Secondary School (sasa Alliance Secondary School) ambako kulikuwa na walimu wa Kiafrika, wengi wao kutoka Makerere, ambao kama wasomi, wangechukua juhudi kuihuisha African Association. Labda kwa kuhisi kuwa hapakuwapo na ukinzani unaokwenda kinyume na maslahi yao katika mfumo wa kikoloni, walimu wale waliamua kujitenga na siasa. Kwa hiyo basi, harakati dhidi ya serikali ya kikoloni ziliachwa kuwa mikononi mwa wa Waislam wa mjini Dodoma, wengi wao wakiwa wachache wa elimu.

Mkono wa Taratibu katika siasa ya Kanda ya Kati hariri

Mwaka 1953, Haruna Taratibu, alikuwa na umri wa miaka 23. Wakati akifanya kazi Public Works Department (PWD) kama mwashi, alijaribu kuunda chama cha wafanyakazi kwa kuwahamasisha na kuwakusanya vibarua walioajiriwa katika kazi za ujenzi. Kwa sababu ya harakati hizo za kutaka kuanzisha chama cha wafanyakazi, Taratibu alionekana na wakoloni kama mtu mkorofi na mzusha vurugu. Hata hivyo Taratibu hakufanikiwa kuanzisha chama hicho na matokeo yake akapewa uhamisho kwenda Singida kama adhabu. Taratibu alivutiwa sana na harakati za Mau Mau nchini Kenya na alizoea kufuatilia matukio yake katika gazeti lake alilokuwa akilipenda sana, Baraza, gazeti la Kiswahili la kila wiki kutoka Kenya.

Ilikuwa katika Novemba 1954 wakati Taratibu alipokuwa akipekuapekua gazeti hilo ndipo alioposoma habari kuhusu TANU. Taratibu aliuliza pale Singida mjini kama kuna tawi la TANU. Taratibu alifahamishwa kukuwepo kwa tawi la TANU pale mjini na katibu wake alikuwa mzee mmoja kwa jina la Mzee Kinyozi. Taratibu alikata kadi yake toka kwa huyo mzee na akawa mwanachama wa chama cha siasa. Asubuhi iliyofuata Taratibu aliingia ofisini kwake na akaiweka kadi yake ya uanachama wa TANU yenye rangi nyeusi na kijani juu ya meza yake, kila mtu aione. Ofisa Mzungu wa PWD Singida hakuweza kuvumila ufedhuli kama ule, alishauri Taratibu apewe uhamisho kurudi Dodoma alikotoka, kabla hajaeneza sumu yake kwa Waafrika wengine.

Mwaka 1955 wakati wimbi la utaifa wa Tanganyika lilipokuwa limepanda sana nchini Tanganyika Omari Suleiman alikuwa na umri wa miaka 43. Suleiman alikuwa fundi cherahani akifanya shughuli zake katika nyumba moja katikati ya mji wa Dodoma. Mkabala na nyumba ambamo Suleiman alikuwa amepanga chumba kimoja ilikuwa nyumba aliyopanga Taratibu. Mara baada ya kupewa uhamisho kutoka Singida, Taratibu alimuuliza jirani yake, Suleiman, kama kuliwepo na tawi la TANU pale mjini. Suleiman alimwambia Taratibu kuwa hapakuwepo na tawi la TANU mjini Dodoma na alimjulisha habari kuwa kulikuwa na tetesi mjini kuwa Hassan Suleiman amemuahidi na kumhakikishia DC kuwa yeye, akiwa katibu wa Jimbo wa TAA, hatairuhusu TANU kusajiliwa katika Jimbo la Kati bila ya idhini yake.

Lakini ukweli ulikuwa Hassan Suleiman alikuwa tayari ameisajili TANU lakini hakumfahamisha mtu yoyote wala kufanya juhudi yoyote kuitisha uchaguzi au kufanya mkutano. Hassan Suleiman kama, Omar Suleiman alikuwa na umri wa miaka arobaini na tatu mwaka 1955. Tofauti na Omari Suleiman, Hassan Suleimani alikuwa ameelimika na alikuwa mwanasiasa mwenye uzoefu akiwa amekiongoza chama cha African Association. Halikadhalika alikuwa amehudhuria mikutano ya African Association Tanganyika na Zanzibar. Baba yake Hassan Suleimani, Taufik bin Suleiman alikutana na Burton, mvumbuzi mashuhuri, kisiwani Zanzibar; na aliajiriwa kama mmoja wa wapagazi katika safari yake ya kutafuta chanzo cha mto Nile. Alisafiri na Burton hadi Bagamoyo ambako kuanzia hapo ndipo walipofunga safari ya bara. Taufik alifariki mwaka 1920 Hassan Suleiman akalelewa na shangazi yake, Binti Taufik. Kisa cha kusoma kwa Hassan Suleiman ni mfano mmoja muhimu sana unaoonyesha jinsi wazazi wa Kiislam walivyokuwa waiuthamini Uislam. Hassan Suleiman alichaguliwa kuingia darasa la sita St. Andrewís College Minaki, mwaka 1925. Shangazi yake alipopata taarifa kuwa mtoto wa ndugu yake alikuwa anasoma shule ya wamishionari alipata hofu ya kile ambacho huenda kitamtokea mwanae, yaani kubatizwa. Alitembea kwa miguu kutoka Dar es Salaam hadi Minaki kumchukua mtoto wake. Siku hizo njia iliyokuwapo kwenda Minaki kutoka Dar es Salaam ilikuwa njia ya miguu kupitia vichakani. Hassan Suleiman alikuwa hajasoma hata majuma mawili mara akamuona shangazi yake anaingia darasani kumtoa shule na akarudinae nyumbani. Sababu aliyoitoa bibi mkubwa yule kwa mwalimu mkuu mmshionari ilikuwa, anahofu mwanae atakuwa murtadi. Safari ya miguu ya kurudi Dar es Salaam iliwachukua siku mbili.

Kukutana na Nyerere katika harakati za Uhuru Kanda ya Kati hariri

Mwaka 1953 Nyerere alipokwenda Dodoma kuhudhuia mkutano wa Kamati ya Elimu ya Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Nyerere alifikia kwa Hassan Suleiman na Nyerere akatambulishwa kwa wazalendo wengine waliokuwa wakiondokea katika siasa kama Oscar Kambona, wakati huo akifundisha katika Kikuyu Secondary School, Nsilo Swai na Kanyama Chiume ambao wote hapo baadaye walikuja kuwa mawaziri katika Tanganyika huru. Kanyama Chiume naye vilevile alikuja kuwa waziri Nyasaland (Malawi) ilipopata uhuru.

Haruna Taratibu, Omari Suleimani na marafiki zake wachache waliunda kamati ndogo kisha wakaandika barua kwenda makao makuu ya TANU Dar es Salaam kuomba ruhusa ya kufungua tawi la chama. Katibu mwenezi wa TANU, wakati ule Oscar Kambona, aliwaandikia kuwaeleza kuwa Hassan Suleiman tayari alikuwa ameshaisajili TANU na ikiwa uchaguzi wa viongozi haujafanyika basi waonanena na yeye pamoja na Ali Ponda. Omari Suleiman na Haruna Taratibu hawakuridhika na majibu kutoka makao makuu ya TANU kwa hiyo walikwenda kutafuta ushauri kwa Edward Mwangosi, aliyekuwa mwanachama mkongwe wa African Association. Mwangosi aliishauri kamati ile iitishe mkutano Community Centre ili kujadili kufungua tawi la TANU, na Hassan Suleiman na Ali Ponda waalikwe kuhudhuria. Kadhalika Mwangosi aliishauri kamati ile kuwaalika walimu waliokuwa wakifundisha Kikuyu Secondary School, wengi wao wasomi kutoka Makerere kuhudhuria mkutano huo. Mwangosi aliwaambia wajumbe wa kamati ile ndogo kuwa wasomi wa Makerere walikuwa ni muhimu sana kwenye chama kwa kuwa wangetoa uongozi uliokuwa unatakiwa.

Karibu ya watu arobaini pamoja na wale wasomi wa Makerere, miongoni mwao Job Lusinde walihudhuria mkutano ule. Lusinde alikuja kuwa waziri, na Amon Nsekela, alikuja kushika nyadhifa muhimu katika serikali na vilevile kuwa balozi wa Tanzania nchini Uingereza. Hassan Suleiman na Ali Ponda hawakutokea mkutanoni. Wakati wanakusanyika kwa ajili ya mkutano, afisa wa Community Centre aliwaambia kuwa alikuwa amepokea amri kutoka kwa DC kuwa mkutano huo usifanyike. Kufuatia amri ile watu walitawanyika mara moja. Alexander Kanyamara aliyekuwa Mwafrika tajiri mjini Dodoma na rafiki wa John Rupia, wakati ule makamu wa rais wa TANU, aliwataka kuahirisha mkutano huo kwa sababu ya kutokuwepo kwa viongozi wa juu wa TAA, Hassan Suleiman na Ali Ponda. Kutokana na sababu hii na vile vitisho vya DC, mkutano uliahirishwa bila kupanga tarehe ya mkutano mwingine.

Asubuhi iliyofuata Taratibu alikamatwa na polisi na kupelekwa kwenye ofisi ya DC, (hivi sasa ofisi hiyo ni ofisi ya Waziri Mkuu). Taratibu alimkuta Hassan Suleiman pale ofisini akizungumza na DC, Bwana Smith. DC alianza kumsaili Taratibu kwa kumuuliza kama alikuwa akijua kuzungumza Kiingereza. Taratibu alijibu kuwa yeye hakusoma. Akizungumza Kiingereza Hassan Suleiman alimwambia DC kuwa yeye ndiye katibu wa TANU mjini Dodoma. DC, Bwana Smith, alimshutumu Taratibu kwa kuunda chama haramu na kwa kuitisha mkutano usio na idhini ya serikali katika Community Centre jana yake ambao ulielekea kuvuruga amani. Bila woga Taratibu alijibu kwamba yeye alikuwa na mamlaka ya kuitisha mkutano kwa sababu alikuwa mwanachama wa chama cha siasa kilichosajiliwa kihalali. Taratibu aliichomoa kadi yake ya TANU kutoka mfukoni kwake yenye rangi nyeusi na kijani na kumwonyesha DC. Bwana Smith alimuuliza Hassan Suleiman kama ikiwa na yeye pia alikuwa na kadi ya TANU. Hassan Suleiman hakuwa nayo. Hassan Suleiman na DC walizungumza Kiingereza kwa muda baada ya hapo aliwataka wote wawili kuandika maelezo yao. Baada ya kuandika maelezo yake Taratibu aliruhusiwa kurudi nyumbani. Inasadikiwa kuwa wakati ule mwanachama pekee wa TANU mjini Dodoma walikuwa Haruna Taratibu na Alexander Kanyamara ambae yeye alikata kadi yake Dar es Salaam.

Wasomi wa Makerere na mkasa wa Taratibu na DC Smith, safari ya DAR na kukutana na Nyerere, kamati ya siri ya TANU na ujumbe Mkuu wa Jimbo la Kati kwa Taratibu hariri

Wasomi wa Makerere, ambao Mwangosi aliwaamini sana katika kuunda TANU, walipopata habari kuhusu mkasa wa Taratibu na DC, Bwana Smith, waliogopa. Waliamua kujiweka mbali kabisa na mambo ya siasa na kuendelea na kazi yao ya kufundisha. Haruna Taratibu na Omari Suleiman sasa waliamua kugeuza mbinu, waliitisha mkutano wa siri usiku nyumbani kwa Swedi bin Athumani. Mkutano huu uliamua kuwa Taratibu lazima aende makao makuu ya TANU Dar es Salaam akazungumze na Nyerere ana kwa ana kuhusu matatizo yaliyokuwa yakiikabili TANU Dodoma. Mahdi Mwinchumu aliyekuwa mwanachama wa TANU Dar es Salaam alijitolea kufuatana na Taratibu hadi makao makuu ya chama Dar es Salaam kwa kuwa alikuwa akijuana na viongozi wa TANU. Said Mussa mjumbe mwingine wa ile kamati ya siri alijitolea vilevile kufuatana na Taratibu na Mwinchumu hadi Dar es Salaam. Siku ya kuondoka Job Lusinde alikwenda stesheni ya gari moshi kuagana na ule ujumbe uliokuwa ukielekea Dar es Salaam, makao makuu ya TANU. Lusinde aliuambia ule ujumbe kuwa jamaa wa Makerere wanaunga mkono maamuzi yote yatakayoamuliwa na ile kamati ya siri.

Kwa bahati nzuri katika gari moshi lile lile ambamo Taratibu na wenzake walikuwa wakisafiri kulikuwa na wajumbe wa TANU kutoka Kigoma, Bukoba na Mwanza wakisafiri kwenda Dar es Salaam kuhudhuria mkutano mkuu wa kwanza wa mwaka wa TANU. Wahudumu ndani ya gari moshi walipofahamu kuwa walikuwa na wajumbe wa TANU kwenye gari moshi lile, waliwafanyia heshima kubwa. Mmoja wa wahudumu wale alijitolea kumpa malazi Salum Mussa nyumbani kwake Dar es Salaam. Mahdi Mwinchumu aliwapeleka Haruna Taratibu na Said Mussa makao makuu ya TANU New Street ambako walifanya mazungumzo na Nyerere pamoja na Rupia. Uongozi wa makao makuu ulielezwa kwa ufupi matatizo yaliyokuwa yakikabili Dodoma katika kufungua tawi la TANU. Papo hapo Nyerere alimwalika Taratibu kuhudhuria mkutano mkuu Hindu Mandal Hall kama mjumbe wa Jimbo la Kati. Mkutano ule ulimchagua Taratibu kuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya Taifa ya TANU. Taratibu na ujumbe wake walirudi Dodoma washindi, walikwenda Dar es Salaam watu wasiojulikana na walirudi nyumbani wakifuatana na mjumbe wa Kamati Kuu ya Taifa wa TANU, chombo cha juu kabisa katika chama. Nyerere alimpa Taratibu dafari ya tasjili ya wanachama, kadi mia moja hamsini za uanachama wa TANU na nakala hamsini za Bill of Rights. Kazi ya kuwahamasisha na kuwaingiza watu TANU alipewa Omari Suleiman, na fundi cherahani mwingine aliyejulikana kwa jina la Abdu Mohamed Mkamba. Mara tu baba mwenye nyumba wake alipopata habari za kuwa mpangaji wake, Haruna Taratibu alikuwa mwanachama wa TANU, alimfukuza kutoka kwenye nyumba yake.

Kutafuta wanachama wapya, Uchaguzi na viongozi rasmi wa wa TANU Jimbo la Kati hariri

Baada ya kupata kikundi kidogo cha wanachama, Taratibu alipiga simu makao makuu ya TANU na kuzungumza na kaimu katibu, Elias Kissenge akaomba ruhusa ya kufanya uchaguzi. Kissenge hakuweza kutoa uamuzi wowote wa maana kuhusu tatizo la uongozi wa TANU Dodoma. Taratibu alifanikiwa kumpata Kambona ambaye aliidhinisha uchaguzi ufanyike kwa shuruti moja la kuwa Hassan Suleiman na Ali Ponda waruhusiwe kushiriki na kugombea uongozi wa chama. Kusisitiza kwa Kambona juu ya uongozi wa zamani wa TAA kuongoza chama kipya huenda kulishawishiwa na mafanikio ya zamani ya uongozi wa Hassan Suleiman mbae alimfahamu huko Dodoma wakati Kambona alipokuwa mwalimu akifundisha Kikuyu Secondary School. Kwa bahati mbaya, wanachama wa TANU waliokuwa wanainukia na chama pale mjini Dodoma waliwaona Hassan Suleiman na Ali Ponda kama wasaliti kutokana na kutokushirikiana na wenzao katika kuanzisha TANU.

Wakati ametatizwa na tatizo la uchaguzi wa TANU, Taratibu alijulishwa na makao makuu kuwa makamo wa rais, John Rupia, atapita Dodoma kwa gari moshi akiwa njiani kwenda Tabora kushughulikia mambo ya chama. Gari moshi liliposimama Dodoma Rupia alishangazwa kuona kundi la wananchama wa TANU wakimsubiri katika kituo cha gari moshi wakimtaka avunje safari waende mjini kujadili na kutatua tatizo la uchaguzi. Rupia aliwaeleza wanachama wa TANU wa Dodoma kuwa yeye hakuwa na idhini kutoka makao makuu kufanya shughuli yoyote ya chama mjini Dodoma. Wanachama wa TANU hawakutaka kusikia lolote na walimwambia Rupia kuwa wamechoshwa na makao makuu kwa kushindwa kwake kutoa uamuzi wa tatizo la uchaguzi. Mizigo ya Rupia ilishushwa chini kutoka kwenye gari moshi na Rupia akawa hana khiyari isipokuwa kuwafuata wale wanachama wa TANU hadi mjini.

Ghafla mji mzima ukavuma tetesi kuwa makamu wa rais wa TANU, John Rupia, yupo mjini kufungua tawi la TANU. Rupia alimwita Hassan Suleimna na akamtaka alete hati ya tasjili ya TANU Hindu Mandal siku inayofuata, mahali ambako mkutano utafanyika. Hassan Suleiman hakutokea mkutanoni lakini alimtuma mtu apeleke ile hati. Ali Ponda alihudhuria mkutano ule. Rupia alikuwa mwenyekiti wa mkutano na TANU ikafanya uchaguzi wake wa kwanza. Alexander Kanyamara alichaguliwa Rais; Haruna Taratibu Makamu wa Rais, Abdallah Mohammed Mkamba, Katibu na Omari Suleiman Mweka Hazina. Miongoni mwa wanachama waasisi alikuwa mwanamke mmoja wa Kimanyema, Binti Maftah Karenga; wengine walikuwa Bakari Yenga, Maalim Khalfan, mwanachuoni wa Kiislamu aliyekuwa akiheshimiwa sana, Idd Waziri na Said Suleiman. Wale wasomi wa Makerere hata mmoja hakujitokeza kwenye mkutano huu wa kuasisi TANU. Ali Ponda, mwanasiasa mkongwe alipuuzwa na hakuchaguliwa kushika wadhifa wowote. Walipoona hawakupewa wadhifa wowote katika TANU, Ali Ponda na Hassan Suleiman walijiunga na UTP kuipinga TANU.

Baada ya uchaguzi huo, wale mafundi cherahani wawili, Abdu Mohamed Mkamba na Omari Suleiman, walianza kuhamasisha wananchi wazi wazi kujiunga na TANU ili wapiganie uhuru wa Tanganyika. Tawi la TANU la Dodoma baada ya kujizatiti pale mjini, lilituma wanaharakati kuwahamasisha watu wa Kondoa ili wafungue tawi la TANU katika wilaya hiyo. Abdallah Jumbe alizipenyeza kadi za TANU na kuzipeleka kwenye wilaya hiyo kwa siri akaanza kuandikisha watu. D.C. wa Singida alikuwa jeuri sana kiasi kwamba ni baada ya Mkutano Mkuu wa Tabora wa mwaka 1958 ndipo Abdallah Jumbe aliweza kufanikiwa kufungua tawi mjini Singida. Wakati huo TANU ilikuwa na nguvu sana ikiwa na wajumbe wake katka Baraza la Kutunga Sheria. Kwa ajili hii hakuna Mzungu aliyethubutu kuwa fedhuli kwa TANU na kuwabughudhi wanachama wake.

Tazama pia hariri

Viungo vya Nje hariri