Hubble (darubini ya anga-nje)

(Elekezwa kutoka Darubini ya Hubble)

Darubini ya Anga-Nje ya Hubble, au mara nyingi Hubble, ni darubini ya anga-nje iliyotengenezwa kwa ushirikianao baina ya taasisi za NASA na ESA kwa utafiti wa nyota. Ilipokea jina lake kwa heshima ya mtaalamu wa anga Edwin Hubble.

Picha ya Darubini ya Hubble kwenye njiamzingo yake, kutoka Feri ya Ange-Nje Discovery mnamo 1997
Picha za Hubble za majarra M100 kabla ya matengenzo ya 1993 na baadaye zinaonyesha jinsi kasoro za awali ziliboreshwa

Kusudi lake hariri

Hubble iliandaliwa na kupelekwa angani kwa gharama za USD bilioni 4.7 na gharama za kwa jumla hadi mwaka 2010 zilikadiriwa kufikia biloni 10, zikiwa pamoja na chombo chenyewe, safari 5 za matengenezo, vipuli, kamera mpya na usimamizi na wanasayansi walioko duniani. Darubini kwenye anga-nje zinaweza kutambua nyota na majarra kwa umakini usiowezekana kwa darubini zilizopo duniani kwa sababu zinachukua picha na vipimo nje ya angahewa ya Dunia inayochafusha vipimo vinavyotekelezwa kwenye uso wa Dunia.

Inachunguza pande zote za taswirangi ya sumakuumeme yaani mnururisho kuanzia masafa marefu ya mialekundu hadi upeo wa masafa fupi za urujuanimno. Kifaa chake kikuu ni kiakisi parabola chenye kipenyo cha mita 2.4. Inazunguka Dunia kwenye njiamzingo kilomita 540 juu ya uso wa ardhi katika muda wa dakika 93[1].

Hubble ilipelekwa kwa feri ya anga-nje kwenye njiamzingo yake mwaka 1990. Baada ya kutuma picha za kwanza ilionekana kuna kosa kwenye kiakisi lililozuia kulenga fokasi ya kutosha. Kasoro hii ilisahihishwa wakati wa matengenezo yaliyotekelezwa mwaka 1993.

Matokeo ya tafiti zake hariri

Hubble ililenga hasa kuangalia na kupima nyotabadilifu za kupwita katika majarra za karibu zinazoruhusu kukadiria umbali wa majarra hizi. Kwa jumla matokeo ya vipimo vyake

 
Sombrero Galaxy in infrared light (Hubble Space Telescope and Spitzer Space Telescope)
  • Tangu mwaka 1994 Hubble ilifanya utafiti wa uga ndefu (Hubble Deep Field) kwa kulenga kwenye eneo la anga-nje pasipokuwa na nyota yoyote iliyotazamiwa hadi wakati ule. Kwenye obiti yake iliweza kuchukua picha mara kwa mara kila baada ya dakika 97 kwenye kipindi cha siku 10. Ilichukua jumla ya picha 342 ambazo baada ya kuunganishwa zilionyesha majarra 3,000. Kwa njia hii iliwezekana kuonyesha mara ya kwanza majarra zenye umbali wa miaka ya nuru bilioni 10 zilizoweza kuthibitishwa. Matokeo haya yalipatikana kwa sababu kiasi cha fotoni (kwanta za nuru) kinachofika kutoka nyota za mbali ni kidogo sana na kwa kuongeza muda wa kuchukua picha idadi hii inaongezeka.[2]
  • Hubble ilirudia kuchukua picha za nyuga ndefu na mwaka 2012 picha ya "Hubble eXtreme Deep Field" iliunganishwa baada ya mfichuo wa jumla ya sekunde milioni 2 uliokunsaywa katika kipindi cha miaka 10; hapa majarra 5,500 zinaonekana na umbali mkubwa ilikuwa miaka ya nuru milioni 13.2.
  • Vipimo vyake vilileta maelewano kati ya wataalamu kuwa umri wa ulimwengi ni mnamo miaka bilioni 13.7
  • Hubble ilipiga picha ya kwanza ya sayari-nje inayozunguka nyota nje ya mfumo wa Jua letu.

Marejeo hariri

  1. Hubble’s orbital path, tovuti ya spacetelescope.org, iliangaliwa Julai 2019
  2. Hubble Breakthroughs. HubbleSite. Iliwekwa mnamo 31 March 2013.

Viungo vya Nje hariri

Weblinks hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu: