Kongwa (kwa Kiingereza: yoke) ni fimbo yenye panda au mgawanyiko[1] ambayo zamani ilitumika kwa kuwafunga wanyama ili kuvuta ama mkokoteni ama plau au watumwa shingoni ili kuwasafirisha.

Watumwa wakisafirishwa kwa kufungwa makongwa; karibu na mto Ruvuma mnamo 1866.

Wakati wa biashara ya watumwa, makongwa yalikatwa mtini. Wafungwa walioonyesha nia na uwezo wa kutoroka walifungiwa kongwa shingoni[2]. Mara nyingi makongwa mawili yalifungwa pamoja, hali iliyooongeza ugumu wa kukimbia.

Katika Biblia hariri

Mfano wa kongwa ulitumika sana katika Agano la Kale na katika Agano Jipya kwa namna mbalimbali, kama vile kuhusu unyanyasaji katika jamii (1Fal 12:4) na kuhusu dhambi iliyofunga na kulemea watu (Mao 1:14).

Torati pia ilifananishwa na kongwa ambayo ilifanywa nzito zaidi na mafundisho ya Mafarisayo hata kulemea waumini (Mdo 15:10). Ndiyo maana Yesu aliwaalika kuachana nao ili kupokea kongwa lake (Math 11:28-30).

Hatimaye Mtume Paulo aliita kongwa la utumwa (Gal 5:1) ambalo Yesu ametuondolea ili tuwe huru, hivyo tusikubali kutekwa tena.

Marejeo hariri

  1. "Kongwa2", TUKI Kamusi ya Kiswahili Sanifu, uk 273
  2. Jean George Deutsch, Slavery & Social Change in Unyamwezi, c. 1860–1900, katika: Slavery in the Great Lakes Region of East Africa. - (East African studies), I. Medard, Henri II. Doyle, Shane (Shane Declan) (James Currey Ltd 2007)