Leonard Mbotela

mtangazaji wa redio

Leonard "Mambo“ Mbotela ni mtangazaji mashuhuri wa redio nchini Kenya. Amejulikana kwa huduma yake ya zaidi ya miaka 40 tangu mwaka 1964. Alikuwa mtangazaji wa habari na michezo, haswa soka. Tangu mwaka 1966 amekuwa hewani na kipindi chake "Je, Huu ni Ungwana?".

Leonard Mbotela alizaliwa Freretown, Mombasa katika familia ya Kianglikana ya watoto nane. Babake James Mbotela alikuwa kati ya walimu wa kwanza Waafrika Kenya. Mamake Ida alifanya kazi ya ustawi wa jamii.

Leonard alisoma shule ya msingi ya Freretown kati ya 1948 na 1953 halafu akaenda Buxton shule ya kati Mombasa kuanzia 1954 hadi 1958. Alihudhuria shule ya sekondari ya Kitui High School kuanzia 1959 hadi 1963.

Alipata nafasi ya kuingia katika ukurufunzi wa Sauti ya Kenya akishirikiana na Simon Ndesanjo katika kipindi ‘Hodi hodi mitaani’. 1964 aliajiriwa kama mtangazaji wa huduma ya Kiswahili. Mbotela alianzisha kipindi chake cha ‘Salamu za vijana’ na pia akasoma taarifa za habari za huduma ya Kiswahili.

Mwaka 1966 alianzisha ‘Je, huu ni ungwana?’ ambacho ni kipindi cha pekee kinachoendelea hadi leo (2006). Alijulikana zaidi nchini kama mtangazaji wa soka kuanzia mwaka 1967. Kati ya vipindi vyake vilivyopendwa ni Uhalifu Haulipi, Ongea Lugha Sanifu na Waliosifika.

Wakati wa uasi wa 1982 (jaribio la kijeshi kuipindua serikali ya rais Moi) Mbotela alilazimishwa kusoma habari za waasi kwa sababu sauti yake ilijulikana kote nchini.

Katika maisha yake ya kazi alikuwa pia mhusika wa huduma ya "Presidential Press Service" chini ya Rais Moi kwa miaka saba.

Alirudi KBC akastaafu mwaka 1997 akiwa na cheo cha mwangalizi mkuu wa vipindi vya redio.

Hata baada ya kustaafu ameendelea kusikika redioni akisoma habari na kipindi chake "Je Huu ni Ungwana?".

Mbotela alimuoa Alice Mwikali mwaka 1970 na pamoja wamezaa watoto watatu - Ida, Jimmy na George.

Viungo vya nje hariri

  Makala hii kuhusu mtu huyo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Leonard Mbotela kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.