Henry Alfred Wolfgang Kissinger (jina la awali: Heinz Alfred Wolfgang Kissinger; 27 Mei 1923 - 29 Novemba 2023)[1] alikuwa mtaalamu wa elimu ya siasa aliyeendelea kuwa mshauri wa marais wa Marekani na hatimaye waziri wa mambo ya nje ya nchi.

Henry Kissinger
Henry Kissinger
Henry Kissinger
Alizaliwa 27 Mei 1923
Alikufa {{{alikufa}}}
Kazi yake mtaalamu wa elimu ya siasa Marekani

Mwaka 1973 alishinda Tuzo ya Nobel ya Amani.[2]

Maisha ya awali hariri

Kissinger alizaliwa nchini Ujerumani mnamo 1923. Familia yake ilikuwa ya Kiyahudi, hivyo alipata matatizo tangu Adolf Hitler aliposhika madaraka mwaka 1933 na kuanza siasa yake ya ubaguzi wa Wayahudi.

Mnamo mwaka 1938, akiwa na umri wa miaka 15, familia iliondoka Ujerumani ikahamia Uingereza halafu Marekani. Wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia alikuwa mwanajeshi wa Marekani akatumwa Ujerumani aliposhiriki kwenye mapigano wakati wa mwisho wa vita [3] na baadaye katika utawala wa kijeshi juu ya Ujerumani.

Baada ya kurudi Marekani, alisoma kwenye Chuo Kikuu cha Harvard alipohitimu digrii ya kwanza mwaka 1950, digrii ya pili mwaka 1951 na hatimaye shahada ya uzamivu mnamo mwaka 1954[4] [5]. Alipata nafasi ya kufundisha kwenye chuo chake akawa profesa kwenye idara ya elimu ya siasa. Katika miaka ile aliitwa pia kushiriki kwenye kamati zilizoshauri serikali katika masuala ya usalama na siasa.[6]

Serikali ya Nixon hariri

Mwaka 1969 Richard Nixon, rais wa Marekani, akamteua Kissinger kuwa mshauri wake katika mambo ya nje. Wakati ule Marekani ilishiriki katika Vita ya Vietnam. Mwaka 1973 Nixon alimfanya kuwa Waziri wa Mambo ya Nje (Secretary of State).

Kissinger aliendesha majadiliano na Vietnam Kaskazini akafaulisha mapatano yaliyoruhusu kupumzishwa kwa mapigano na kuondoka kwa jeshi la Marekani huko Vietnam. Kwa mapatano hayo alipokea Tuzo ya Nobel ya Amani pamoja na mwakilishi wa Vietnam Kaskazini Le Đuc Tho. Hata hivyo, mikaka 2 baadaye vita ilianza upya na Vietnam Kaskazini iliweza kushinda Vietnam Kusini.

 
Kissinger na Mao Zedong

Kissinger alianza pia majadiliano na serikali ya kikomunisti ya China akatembelea Beijing alipokutana na Mao Zedong[7]. Hivyo aliandaa ziara ya rais Nixon huko Beijing kwenye mwaka 1971.

Kissinger alisisitiza pia majadiliano na Umoja wa Kisovyeti kwa shabaha ya kupunguza ukali wa Vita Baridi. Aliweza kupata mapatano na uongozi wa Kisovyeti kuhusu kudhibiti idadi ya silaha za nyuklia.

Baada ya kujiuzulu kwa Nixon, Kissinger aliendelea kama waziri wa mambo ya nje chini ya rais Gerald R. Ford. .

Miaka ya baadaye hariri

Baada ya kutoka serikalini, Kissinger alirudi kwenye nafasi ya kufudisha kwenye vyuo vikuu na pia kufanya utafiti katika fani yake. Pamoja na William Perry, Sam Nunn, na George Shultz alitoa wito kwa serikali kupunguza silaha za nyuklia, na katika makala tatu za Wall Street Journal alipendekeza mpango wa hatua za haraka kufikia mwisho huo.

Marejeo hariri

  1. "Definition of KISSINGER". www.merriam-webster.com. 
  2. The Nobel Peace Prize 1973 Henry Kissinger & Le Duc Tho, Award ceremony speech
  3. Isaacson, Walter (1992). Kissinger: A Biography. Simon & Schuster. ISBN 978-0-671-66323-0, uk. 38
  4. Ferguson, Niall (2016). Kissinger, 1923 - 1968: The Idealist. Penguin Books. uk. 237. 
  5. https://www.foreignaffairs.com/reviews/capsule-review/1979-03-01/kissinger-and-meaning-history Kissinger and the Meaning of History
  6. "Henry Kissinger – Biography". NobelPrize.org. Iliwekwa mnamo December 30, 2006.  Check date values in: |accessdate= (help)
  7. Dube, Clayton. "Getting to Beijing: Henry Kissinger's Secret 1971 Trip". USC U.S.-China Institute. Iliwekwa mnamo July 21, 2011.  Check date values in: |accessdate= (help)