Neema Lugangira

mwanamke mwanasiasa kutoka Tanzania

'

Neema K. Lugangira
Majina mengineNeema K. Lugangira
Kazi yakeMtaalamu wa Masuala ya Sera, Lishe, Kilimo na Mwanasiasa
Ndoa2002 - 2015
WatotoGeorgia Blessings (17) na Cornel James (15)


Neema K. Lugangira (alizaliwa 1982) ni mtaalamu wa masuala ya sera, kilimo na lishe. Kwa sasa anafanya kazi kama mkurugenzi wa Idara ya Sera katika Mpango wa Kuendeleza Kilimo Ukanda wa Mikoa ya Nyanda za Juu za Kusini mwa Tanzania (Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania (SAGCOT)[1].

Kati ya majukumu yake kwenye nafasi hiyo ni kuhakikisha kuwa sera za kisekta zilizopo zinachangia mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji kushamiri. Anajulikana zaidi kwa ushawishi na ushiriki wake kwenye kuandaa na kuendeleza sera na kanuni zinazohusiana na uchimbaji wa madini, gesi na mafuta Tanzania [2] [3] [4] [5] na alitajwa kuwa kati ya wanawake 100 wenye ushawishi mkubwa nchini Tanzania chini ya kampeni ya #100Sheroes mwaka 2018.

Neema pia ni mwanasiasa na mwanzilishi wa kampuni ijulikanayo kama HealthyMaisha inayojihusisha na lishe na afya. Pia, ni mwanzilishi na mkurugenzi wa asasi isiyo ya kiserikali iitwayo AgriThamani yenye lengo la kuboresha lishe nchini kupitia sera wezeshi, elimu ya lishe na sekta za kilimo.

Maisha hariri

Neema ni mtoto pekee na ni mama wa watoto wawili, Georgia Blessings na Cornel James.

Kazi hariri

Neema amefanya kazi kwa muda mrefu na kwenye sekta ya uchimbaji madini, mafuta na gesi asilia hadi mwaka 2016 ambapo alihamia kwenye sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi. Kwa ujumla, anajihusisha zaidi na kazi za taaluma za sera na biashara. Amekua mkuu wa kitengo cha sera na mazingira wezeshi katika katika jukwaa la kuendeleza kilimo maeneo ya kusini mwa Tanzania (SAGCOT) tangu Oktoba 2016, ambapo majukumu yake makubwa ni kuchochea mabadiliko ya kisera yatakayopelekea kuongeza "Local Content" na kuinua uwekezaji. [6]. Pia, aliwahi kua mwanachama wa kamati ya kimataifa ya kuandaa mpango wa kupokea na kutathmini viwango vya taarifa za manunuzi vya ndani ya nchi mbalimbali kwenye sekta ya madini.

Kabla ya kufanya kazi SAGCOT, Neema alikua kaimu mkurugenzi wa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) [7]. Moja ya majukumu yake ikiwa ni kuanzisha idara ya ushiriki wa watanzania kwenye uwekezaji (Local Content in Investments). Sehemu nyingine ambazo amewahi kufanya kazi ni Wizara ya Nishati na Madini kama afisa mwandamizi wa vifaa na masuala ya sera ya "local content"[8]. Pia amewahi kufanyia kazi kampuni ya kimataifa ya mafuta na gesi asilia, Statoil, na kampuni ya Adam Smith International. Aidha, Neema ni mshauri wa kujitegemea kwenye maeneo ya mkakati wa maendeleo.

Nje ya kazi hizo, Neema anajihusisha na siasa. Ni mwanachama wa kamati kuu ya Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na mwanachama wa baraza la taifa la UWT mkoa wa Kagera. Pia ni mwenyekiti wa kamati ya mahusiano ya umma ya UWT.

Neema ni mwanzilishi wa HealthyMaisha, biashara ya kijamii inayojihusisha na tiba-lishe hasa kwa mkoa wa Dar es Salaam. Neema alinukuliwa akisema kwamba alianzisha kampuni hiyo baada ya yeye binafsi kukutana na changamota za kiafya na kuona umuhimu wa lishe sahihi. HealhtyMaisha imejikita katika uuzaji wa vyakula vinavyofaa kwa afya bora kama mboga mboga, matunda na juisi, kwa watoto na wanawake wenye upungufu wa damu pamoja na wanawake waliozidi uzito. Pia, inajishughulisha na kutoa elimu ya lishe kwenye maeneo mbalimbali kama hospitali, sehemu za mazoezi, kwenye mashule na maofisi [9].

Pia, Neema ni mwanzilishi na mwenyekiti wa asasi isiyo ya kiserikali, AgriThamani Foundation. Lengo la asasi hiyo ni kuinua hali ya lishe na kukuza kilimo lishe mkoani Kagera na kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana wa kwenye minyororo ya thamani ya kilimo. Taasisi hii inashirikina na ofisi ya mkuu wa mkoa wa Kagera katika kutekeleza majukumu yake tangu Oktoba mwaka 2018 [10].

Elimu hariri

Neema ana stashahada ya juu kwenye masomo ya biashara kutoka chuo cha Boston, Uingereza, na shahada ya uzamivu ya usimamizi wa bishara (manunuzi na minyororo ya usambazaji) kutoka taasisi ya usimamizi wa ununuzi ya ulaya iliyopo nchini Ufasansa (2011 - 2013). Andiko lake la kumaliza shahada ya uzamivu, limeongelea uwezekano wa kutumia hifadhi ya gesi iliyopo ardhini kwa manufaa ya kiuchumi ya taifa na mchango wa wadau mbalimbali wanaohusika kwenye sekta hiyo katika kufika malengo tajwa [11].

Kwa upande mwingine, Neema alisoma ushauri wa kiafya na tiba ya juisi kwa njia ya mtandao na kufuzu mafunzo hayo mwaka 2017.

Neema alipata elimu ya msingi shule ya Mt. Constantine, Tanzania, na elimu ye sekondari shule ya Braeburn, Kenya.

Tuzo alizowahi kupata hariri

Neema ameshinda tuzo mbalimbali kwa kupitia kampuni yake HealthyMaisha. Mwaka 2018 wakati kampuni hiyo ikiwa na miezi minne tu, ilifanikiwa kuingia tano bora na kupata fedha kiasi cha Euro 3500 kwenye mashindano ya “Scaling Up Nutrition Pitch Competition” yaliyofanyika nchini Kenya [12]. Mwaka huo huo, kampuni ya HealthyMaisha ilishinda tuzo kwenye “SUN Regional Pitch Competition” [13].

Machapisho hariri

Kwenye taaluma ya uchimbaji madini, mafuta na gesi Tanzania, Neema ameandia kitabu kiitwacho “Local Content in Supplier Development: Developing Local Suppliers in Order to Optimize and Maximize Local Content in Tanzania's Natural Gas Industry” kilichochapishwa mwaka 2014 [14]. Kitabu hiki kimetokana na andiko la shahada yake ya uzamivu.

Andiko lake la kumaliza shahada ya uzamili lilichambua sekta ya gesi asilia Tanzania na jinsi gani inaweza kutumika kuinua uchumi wa nchi. Kwenye andiko hilo, Neema alichambua mchango wa washikadau wakubwa watatu kwenye mnyororo wa usambazaji wa gesi asilia; serikali ya Tanzania, wasambazaji na wateja. [15].

Akiwa kama mkuu wa kitengo cha sera na mazingira wezeshi SAGCOT, Neema pia alitoa andiko lenye kichwa “SAGCOT - AFRICA’S SUCCESS STORY” ambalo limeongelea mchango na mafanikio ya SAGCOT kwenye maendeleo ya sekta ya kilimo ukanda wa Kusini mwa Tanzania [16] [17].

Tanbihi hariri

  Makala hii kuhusu mtu huyo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Neema Lugangira kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.