Sheikh Ilunga Hassan

Sheikh Ilunga Hassan Kapungu (1957 - 5 Mei 2014) alikuwa mwanaharakati wa Kiislamu kutoka Tanzania. Enzi ya uhai wake, alipigania haki na mustakabali wa Waislamu nchini humo. Shughuli zake hasa zilikuwa kueneza habari za dini na kupiga vita nadharia ya "Mfumo Kristo". Alianza kutoa Da’wah , tangu miaka ya 1980 mpaka kifo chake ambapo sababu iliyopelekea kifo chake ni ugonjwa wa kisukari.

Sheikh Ilunga Hassan
Nyuma wapili Bakari Saleh, mwisho kulia Ilunga Hassan Kapungu, Mstari wa mbele watatu kutoka kushoto Mwanahistoria - Mwandishi Mohamed Said. Hawa walikuwa baadhi ya vijana wa Kiislamu waliohudhuria Semina Dodoma Chuo Cha Biashara 1988.
Nyuma wapili Bakari Saleh, mwisho kulia Ilunga Hassan Kapungu,

Mstari wa mbele watatu kutoka kushoto Mwanahistoria - Mwandishi Mohamed Said. Hawa walikuwa baadhi ya vijana wa Kiislamu waliohudhuria Semina Dodoma

Chuo Cha Biashara 1988.
Jina la kuzaliwa Ilunga Hassan Kapungu
Alizaliwa 1957
Alikufa 5 mei 2014
Nchi Tanzania
Kazi yake Mwana harakati wa kiislamu

Alianza harakati za kuamsha watu dhidi ya nadharia hiyo tarehe 15 Januari 2011 hadi tarehe 16 Oktoba 2011. Ambapo ziara ya kuzunguka nchi nzima ilianza mnamo 15 Januari 2011 jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Diamond Jubilee chini ya Kamati Maalumu ya Maandalizi ya Makongamano ya Waislamu Dhidi ya Mfumokristo Tanzania.

Maisha, harakati na historia yake hariri

Sheikh Ilunga Hassan Kapungu kaingia katika historia ya Dar es Salaam katika kifo chake. Bahari ya watu walijazana Msikiti wa Kichangani kuja kuswalia jeneza lake na kisha kulifata nyuma jeneza hilo hadi Makaburi ya Mwinyimkuu, Magomeni Mapipa. Sheikh Ilunga ni mgeni katika mji wa Dar es Salaam kwa maana ya kuwa hakuzaliwa Dar es Salaam wala hakuwahi kuishi Dar es Salaam. Alikuwa akija na kuondoka zamani akirejea kwao Tabora na baadaye kuhamia Mwanza, akija Dar es Salaam na kurejea Mwanza.

Sheikh Ilunga Hassan Kapungu alikuwa kipenzi cha Waislam wa Tanzania nzima. Kibla cha kila msikiti wa Waislam katika Tanzania kilikuwa kinamkaribisha kama si kuwaidhi basi angalau asimame awasalimie nduguze Waislam. Sheikh Ilinga Hassan Kapunga hakuwa katika lile kundi la mesheikh ambao wao wenyewe kwa hofu tu kuna baadhi ya misikiti wanaogopa si kuingia kuswali, bali hata kupita nje. Sheikh Ilunga hakuwa katika lile kundi la masheikh wenyeji katika futari za serikali misikiti ya wakubwa na shughuli zinazohusiana na mambo kama hayo lakini wageni katika misikiti ya ndugu zao Waislam. Kubwa Sheikh Ilunga hakukosa usingizi kwa kukosa kualikwa futari Ikulu au kualikwa katika dhifa za serikali akapigwa picha na waheshimiwa na kutokea katika runinga na magazeti siku ya pili ukurasa wa mbele. Sheikh Ilunga Hassan Kapungu hakushughuliswa na hayo. Yeye alishughulishwa na kuliweka juu jina la Allah. Hili ndilo lililokuwa likimshughulisha mpaka siku Allah alipomfisha.

Sheikh Ilunga kaweka historia katika historia ya mazishi makubwa Dar es Salaam, historia inayokwenda nyuma kiasi miaka takriban 100 ukianzia mazishi ya Sheikh Mwinyikheri Akida, sheikh aliyeasisi Msikiti wa Mwinyikheri Akida, Kitumbini unakuja kwa Sheikh Idrissa bin Saad Khalifa wa Tariqa Askariyya, kisha Sheikh Kaluta Amri Abeid, halafu Abdulwahid Sykes, kisha Sheikh Kassim bin Juma, halafu Prof. Kighoma Ali Malima unaishia kwa Mzee Kitwana Dau baba yake Dk. Ramadhani Dau.

Kilichopelekea kumpandisha daraja Ilunga katika jamii ya Kiislam Tanzania, Ilunga alikuwa mtumishi wa Waislam. Wakimtuma Ilunga kila kazi na akiifanya kwa moyo mkunjufu, kuanzia kujenga madras na shule kisha akawasomeshea na watoto wao hadi siku aliposimama Ukumbi wa Diamond kuitahadharisha serikali kuwa kuna Mfumokrsisto nchini unaotawala na kudhulumu haki za Waislam. Hii ilikuwa mwaka 2012. Tukio ambalo kwa Waislamu wengi walilichukulia kitendo kile cha kihistoria.

Ilichukuliwa hivyo kwa sababu takriban miaka 40 Waislam walikuwa wanasemea pembeni. Wakati ulikuwa umefika Waislam wakasimama kuitahadharisha serikali kuhusu kujiachia dini moja ikahodhi fursa zote za nchi kwa hila na Radio Imaan na TV yake vilikuwapo na Radio Imaan ilirusha hafla ile na mubashara, yaani live. Kote Radio Imaan ilikosikika Waislam walimsikia Sheikh Ilunga akieleza nini Waislam walifanya katika Tanganyika wakati wa kupigania uhuru kuuondoa dhulma na kuleta haki kwa kila mwananchi. Hili lilikuwa jambo kubwa na zito kwa serikali yoyote ile kuwa inashutumiwa kwa kulea udini ndani ya serikali. Hasa kwa kuamini ya kwamba nchi nyingi Afrika zimeangamia kwa ugonjwa huu.

Katika hili, vyombo vyote vya habari ukitoa vile vya Kiislam viligoma kabisa kuitaarifu jamii kuhusu kongamano hili la Waislam. Ikawa kama vile hapajapatapo kutokea kitu chochote. Kuanzia siku ile Sheikh Ilunga alitembea nchi nzima na kufanya mikutano ya hadhara kuitahadharisha kwanza serikali kuhusu Mfumokristo na pili Waislam ili wajue nini kilikuwa kinawatafuna.[1]

Mwanzo wa kufahamika na wanaharakati wengine hariri

 
Mazishi yake yameweka historia baada ya maelfu ya Waislamu kujitokeza kushiriki, hali iliyopelekea mchanga wa kaburi lake kufukiwa kwa mikono badala ya kutumia mapauro na majembe kama ilivyozoeleka.[2].

Sheikh Ilunga Hassan Kapungu ailianza kusikika sifa zake katika miaka ya 1980. Wakati ule Sheikh Ilunga alikuwa kijana mdogo sana. Umaarufu wake ulianza pale Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam Ilunga katika msikiti wa Muslim Students Association of the University of Dar es Salaam (MSAUD) kiasi unaweza ukadhani kuwa na yeye ni mwanafunzi.

Ilikuwa Ilunga na wenzake ndiyo walioleta Nyaraka za Mzee Bilali Rehani Waikela pale MSAUD. Hizi nyaraka zilikuwa zimefichwa Tabora kwa karibu miaka 20. Katika nyaraka hizi kulikuwa na kisa kizima cha kile kilichokuja kujulikana kama Mgogoro wa East African Muslim Welfare Society (EAMWS), Ndani ya jalada lililofikishwa MSAUD kulikuwa na taarifa, za mikutano ya EAMWS, taarifa ya Kamati ya Upatanishi iliyokuwa inajaribu kupatanisha kati ya kundi la Adam Nasibu na wenzake waliokuwa wanaipiga vita EAMWS, kulikuwa na vipande vya magazeti ya Uhuru, Nationalists na Tanganyika Standard, magazeti makubwa ya zama zile yaliyokuwa yakifuatilia kwa karibu sana mgogoro ule.

Nyaraka hizi za Mzee Bilal Rehani Waikela zilikuwa hazina kubwa. Kutokana na nyaraka hizi ndipo ukweli wa nini na nani alikuwa nyuma ya kuvunjwa EAMWS na kuundwa kwa BAKWATA. Lakini kubwa zaidi waliokabidhiwa Nyaraka za Waikela walizileta zikiwa na maelezo ili maelezo yale yaenda na kile kitakachosomwa ndani ya jalada. Ilunga alikuwa kijana wa Mzee Waikela. Katika hali ya unyonge sana walikuwa wakiendesha shule ya Nujum katika juhudi za Waislam kujitoa katika dhulma ya elimu.

Mzee Waikela alimsomesha vyema Ilunga kuhusu fitna na chuki ya Nyerere kwa Uislamu na Waislam na mbinu zinazotumika kuudhalilisha Uislam. Bilali Rehani Waikela alikuwa mmoja wa waasisi wa TANU Western Province mwaka wa 1955 na ni yeye na wenzake ndio waliomleta Nyerere na Bi. Titi Mohamed kuja kuitia nguvu TANU Western Province. Ilunga akasomeshwa na Mzee Waikela historia ya kweli ya uhuru wa Tanganyika. Mzee Waikela vilevile alikuwa Katibu wa EAMWS Western Province. Mzee Waikela alikuwa mfano na kigezo kikubwa kwa Ilunga katika maisha yake ya kuwatumikia Waislam na kwa upande wake Ilunga alikuwa mwanafunzi hodari.

Nyaraka hizi zilimfikia sheikh Mohamed Said na alisoma jalada lile tena na tena na akaweka azma ya kwenda Tabora kuonana na Mzee Waikela. Mambo haya yote ambayo Ilunga aliyokuwa akisomeshwa na Mzee Waikela kuhusu hujuma dhidi ya Uislam ilikuwa kabla hata John Sivalon hajaandika kile kitabu chake maarufu Kanisa Katoliki... na kitabu cha P. Van Bergen, Religion and Development in Tanzania, vilivyothibitisha hujuma hiyo.

Kwa ajili hii basi Ilunga alikuwa kajua mengi kabla hata siri hii haijakuwa wazi kwa Waislam wengi na kayajua haya akiwa na umri mdogo sana. Ndiyo maana kwa waliokuwa wanamjua Ilunga walijua wazi na fika kuwa kama katika Tanzania kuna mtu ambae anastahili kupanda jukwaa akazungumza na Waislam na serikali kuhusu Mfumokristo hakuna mwingine isipokuwa Sheikh Ilunga.

Ilunga taaluma yake ni ualimu na kwa hakika aliwasomesha Waislam kuhusu dhulma iliyodumu Tanganyika kwa kipindi chote Tanganyika ilipokuwa huru. Ilunga alizungumzia kuhusu historia ya uhuru, kuhusu mabilioni katika Makubaliano ya Serikali na Kanisa (Memorandum of Understanding) ambayo serikali ilikuwa ikitoa kuwapa Wakristo kujiendeleza.

Ilunga miaka ya 1990 hariri

Miaka ya 1990 Sheikh Ilunga alikuwa amehamia Mwanza akitokea Tabora. Hii ilikuwa baraka kubwa kwa Mwanza kwani mara tu alipofika alianza kuendesha darsa katika misikiti na kutoa mihadhara. Haikupita muda hali ya Mwanza ikabadilika darsa za Sheikh Ilunga zilizaa matunda vijana walijitathmini upya na taratibu umoja wa Kiislam ukaimarika na hii iliangia hadi BAKWATA.

Viongozi waliochaguliwa kuongoza BAKWATA walikuwa kweli viongozi na viongozi hawa wakawa sasa wanafanya kazi ya Mola. BAKWATA ya Mwanza ikawa tofauti na BAKWATA nyingine nchini. Kuna siku Ilunga alinifahamisha kuwa BAKWATA ya Mwanza inamtumikia Allah Waislam wasiwe na hofu yoyote. Alinifahamisha kuwa msimamo waliouweka ni kuwa kutiana nguvu katika yale ambayo wanakubaliana mathalan elimu kwa vijana. Haukupita muda mrefu Mwanza ukawa mji wa kupigiwa mfano katika juhudi maendeleo ya Waislam. Ilikuwa katika kipindi hiki ndipo yalipotokea Mauaji ya Waislamu Msikiti wa Mwembechai mwaka 1998.

Hili lilikuwa jambo kubwa katika historia ya Uislam Tanzania na yapo mengi yaliyopitika. Katika hayo mojawapo ni kualikwa kwa Sheikh Ilunga mwaka 1999 kuja Msikiti wa Mtambani kufanya mhadhara kuadhimisha mwaka mmoja tangu mauaji yale. Dares Salaam ilikuwa haijamsikia Ilunga. Siku ile ndipo walipokiona kipaji chake cha kuzungumza.[3]

Tazama pia hariri

Marejeo hariri