Askofu Mkuu wa Canterbury

Askofu Mkuu wa Canterbury anafahamika kama kiongozi wa kiroho katika Kanisa la Uingereza na katika Jumuiya Anglikana.

Asofu Mkuu Justin Welby
Kanisa Kuu la Canterbury

Kimsingi ndiye askofu wa dayosisi ya Canterbury, Uingereza na askofu mkuu wa Jimbo la Canterbury la Kanisa Anglikana; jimbo hilo linaunganisha dayosisi 30 katika Uingereza. Katika dayosisi hizo Askofu Mkuu wa Canterbury ana mamlaka za kisheria.

Katika Kanisa la Uingereza kwa jumla na katika Jumuiya Anglikana ana nafasi ya heshima kama ishara ya umoja wao.

Askofu Mkuu anateuliwa na Mfalme wa Uingereza aliyetambuliwa kuwa "gavana mkuu" wa Kanisa la Uingereza, akifuata mapendekezo ya waziri mkuu wa Uingereza anayepokea majina kutoka kanisa lenyewe.

Asili ya kipaumbele wa askofu wa Canterbury ni historia, kwa sababu Canterbury ilikuwa mji wa kwanza katika Uingereza uliokuwa na askofu wa Kanisa la Kilatini mnamo mwaka 597. Baada ya kuongezeka kwa dayosisi katika nchi hiyo askofu wa Canterbury alitambuliwa kama askofu mkuu.

Askofu Mkuu wa Canterbury aliwahi kuwa mkuu wa Kanisa Katoliki la Uingereza hadi karne ya 16, ambako Uingereza lilijitenga na mamlaka ya Papa wa Roma. Kanisa liliendelea kujiita "Kanisa la Uingereza", na Askofu Mkuu wa Canterbury ndiye kiongozi wa kanisa hilo.

Kutokana na uenezaji wa mamlaka ya Milki ya Uingereza (British Empire) duniani katika karne za 18 na 19, Kanisa la Uingereza lilianza kutuma maaskofu katika makoloni. Dayosisi zilizoanzishwa kwa njia hiyo zimekuwa makanisa ya kujitawala katika Jumuiya Anglikana yanayoendelea kumpa Askofu Mkuu wa Canterbury nafasi ya heshima katika umoja wao.

Askofu Mkuu wa sasa ni Justin Welby (tangu mwaka 2013).

Marejeo hariri

Tovuti za Nje hariri