Shehena (kwa Kiingereza: freight, cargo) inamaanisha mzigo wa bidhaa ambazo zinasafirishwa, mara nyingi kwa kutumia chombo cha usafiri kama vile lori, treni, meli au eropleni[1][2]. Kihistoria, na hadi leo katika maeneo yasiyo na njia nzuri, shehena zilisafirishwa pia kwa njia ya wapagazi na wanyama kama vile punda, farasi au ngamia.

Bandari ya shehena ya kontena mjini Hamburg, Ujerumani.
Punda anayebeba shehena za chupa za gesi huko Moroko.

Vyombo vya usafiri wa shehena kwa kawaida hutengenezwa kwa namna ya pekee inayolingana na shehena yake. Tangu kuenea kwa kontena zenye vipimo sanifu, vyombo vya usafiri vya shehena vimesanifishwa pia ili kulingana na vipimo vile, hasa malori, mabehewa ya reli na meli.

Shehena hupatikana kwa maumbo tofauti, kama vile ya gesi au kiowevu inayofungwa katika matangi, na kubebwa kwa chombo cha tangi. Bidhaa zinazofungwa katika vifurushi kwa kawaida huwekwa ndani ya kontena; bidhaa za pekee kama mashine kubwa, mabomba, magogo ya miti au zisizofunguka kama mchanga na kokoto huhitaji vyombo vyake.

Marejeo hariri

  1.   Chisholm, Hugh, ed. (1911). "Cargo". Encyclopædia Britannica (11th ed.). Cambridge University Press.
  2. McLeod, Sam; Schapper, Jake H.M.; Curtis, Carey; Graham, Giles (2019). "Conceptualizing freight generation for transport and land use planning: A review and synthesis of the literature". Transport Policy (in English) 74: 24–34. doi:10.1016/j.tranpol.2018.11.007.