Wema ni neno lenye kumaanisha kumfanyia mambo mazuri na kumfanya mwingine aweze kufurahi. Tunaweza kuwafanyia wema ndugu zetu, marafiki zetu na watu wengine wengi wanaotuzunguka. Jambo hili ni la thamani sana kwa wengine na hata kwetu wenyewe, kwa sababu mtu unayemfanyia wema unaweza ukakutana naye na akakusaidia pia, lakini kama wewe ulishindwa kumfanyia wema naye pia hatashindwa kukulipizia ubaya.

Wema tunaweza kutumia neno hili kwa maana nyingi tofauti wapo watakaotumia kama jina tu kwa sababu zao binafsi na wengine kwao ni kama jambo la kumfanyia mwingine mambo mazuri. Basi pamoja na yote haya ni muhimu kuwafanyia wengine wema na hata kujifanyia mwenyewe; kwa kufanya hivyo tunaweza kuishi kwa amani na furaha katika maisha yetu sote.

Katika falsafa, wema ni kati ya sifa za msingi za uwepo, pamoja na umoja, ukweli na hatimaye uzuri. Kwa msingi huo, Mungu ambaye anasadikiwa kuwepo milele bila kuweza kutokuwepo ana sifa hiyo bila kipimo: ndiye wema wenyewe, chanzo cha mema yote yanayopatikana katika viumbe vyake.