Topido (kwa Kiingereza: torpedo) ni silaha inayotumiwa kwenye maji. Kimsingi ni bomu lililounganishwa na injini na parapela, kwa hiyo inaweza kujisukuma katika maji (mara nyingi chini ya maji) na kuelekea lengo lake ambako bomu linalipuka.

Topido nyepesi ya Kimarekani aina "A Mark 46 Mod 5" ikirushwa kutoka manowari; itaanguka kwenye maji na kuendelea chini ya uso wa maji
Topido ikiingizwa katika bomba la kurushia kwenye nyambizi ya Kifaransa
Topido ya kwanza ya Whitehead: mbele iko sehemu kilipukaji, katikati sehemu ya hewa iliyoshinikizwa, nyuma injini inayozungusha parapela

Topido inajulikana kama silaha kuu ya nyambizi lakini historia yake ilianza kama silaha ya manowari za kawaida. Awali neno "torpedo" lilitumiwa kutaja aina mbalimbali za mabomu ya maji yasiyokuwa na injini.

Mwaka 1866 mhandisi Mwingereza Robert Whitehead alitengeneza topido ya kwanza katika utumishi wa wanamaji wa Austria-Hungaria; aliunda silaha yenye baruti kg 9 iliyoendeshwa kwa nguvu ya hewa iliyoshinikizwa na kuendesha parapela; iliweza kujisukuma kwa umbali wa mita 300-400 kwa kasi ya km/h 11.

Silaha hiyo ya kwanza iliboreshwa haraka ikatambuliwa kwamba hata boti dogo linaweza kubeba topido kadhaa na kuwa hatari kwa manowari kubwa. Hii ilithibitishwa kwa kuzamishwa kwa manowari ya Milki ya Osmani mwaka 1878 iliyoshambuliwa na maboti madogo ya Urusi yaliyobeba topido.

Tangu kupatikana kwa nyambizi topido ilikuwa silaha kuu iliyorushwa chini ya maji. Lakini kulikuwa pia na sehemu za kurusha topido kwenye nchi kavu kwa shabaha ya kutetea hori au mlango wa bandari dhidi ya manowari.

Injini za hewa iliyoshinikizwa zilitumiwa hadi Vita Kuu ya Pili ya Dunia lakini wakati ule tayari injini za umeme zilianza kutumiwa.

Leo hii kuna injini tofautitofauti. Umbali wa topido umeongezwa hadi kufikia kilomita kadhaa. Manowari hubeba topido hasa kwa kujihami dhidi ya nyambizi.

Viungo vya Nje hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya teknolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hiyo kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.