Haumea (alama: 🝻)[1] ni sayari kibete inayozunguka jua letu katika umbali mkubwa kwenye ukanda wa Kuiper. Ilitambuliwa mwaka 2004. Ina umbo la duaradufu; kipenyo chake baina ya ncha zake ni kilomita 1,138 lakini kipenyo kwenye ikweta ni kati ya km 2322 na km 1704. Umbo hili linatokana na mzunguko wa haraka kwenye mhimili wake.

Haumea na miezi yake
Mbingirio wa Haumea

Haumea ina miezi miwili: Hiiaka na Namaka.

Haumea inapita Njia Mzingo yake ya kuzunguka Jua katika muda wa miaka 283 na miezi 6.[2]

Periheli yake ina umbali wa vizio astronomia 35, afeli wa vizio astronomia 51 kutoka Jua.

Obiti ina mwinamo wa nyuzi 28,2° dhidi ya ekliptiki.

Masi yake ni takriban theluthi moja ya Pluto. Umbo halifanani na tufe; umbo la Haumea limefananishwa na kiazi au sigara. Vipimo vyake vinakadiriwa kuwa kilomita 2,322 × 1,701 × 1,138.

Nadharia moja inajaribu kueleza umbo na mzunguko wake wa haraka kutokana na mgongano na gimba kubwa takriban miaka bilioni 4 iliyopita.[3]. Kutokana na mgongano huu inadhaniwa ya kwamba vipande vingi vya gimba la awali viliachana na Haumea vikiifuata sasa kama wingu la vipande vidogo.[4]

Marejeo

  1. JPL/NASA (2015-04-22). What is a Dwarf Planet?.
  2. (136108) Haumea, Hi'iaka, and Namaka , data za haumea kwenye tovuti ya johnstonsarchive.net, iliangaliwa Oktoba 2017
  3. Haumea the strangest known object in the Kuiper belt, tovuti ya Caltech, iliangaliwa Oktoba 2017
  4. A collisional family of icy objects in the Kuiper belt, hitimisho ya makala kwenye tovuti ya nature.com, Nature 446, 294-296 (15 March 2007), iliangaliwa Oktoba 2017

Viungo vya nje