La Amistad (neno la Kihispania kwa "Urafiki") ilikuwa jahazi yenye milingoti miwili katika karne ya 19, iliyomilikiwa na Mhispania kwenye kisiwa cha Kuba, wakati ule koloni la Hispania.

Picha ya Amistad mwaka 1839.
Uasi kwenye Amistad, jinsi ulivyochorwa mwaka 1839 kwenye magazeti ya Marekani.

Ilijulikana mnamo Julai 1839 kwa uasi wa wafungwa Waafrika waliomwua nahodha na kuteka chombo hicho. Mbele ya pwani ya Marekani walikutana na manowari ya Kimarekani iliyowakamata. Katika kesi zilizofuata mbele ya mahakama mbalimbali madai ya Hispania ya kuwarudisha Kuba kama watumwa yalikataliwa. Kesi ya La Amistad ilikuwa na ushawishi mkubwa kwa harakati ya kupinga utumwa Marekani.

Uasi huo, pamoja na kesi zake, ni msingi wa vitabu mbalimbali pamoja na filamu "Amistad" iliyoongozwa na Steven Spielberg kwenye mwaka 1997.

Wafungwa wa Amistad hariri

 
Mfalme Siaka (Sharka) Massaquoi aliyeuza watumwa waliofika baadaye kwenye Amistad
 
Sengbe Pieh ( Joseph Cinqué), kiongozi wa uasi kwenye Amistad

Amistad ilibeba wafungwa Waafrika 53 ambao walikuwa Wamende kutoka maeneo ya Sierra Leone ya leo. Waliwahi kukamatwa nyumbani kwao kwa njia mbalimbali; wengine na wawindaji wenyeji wa watumwa, wengine walikuwa wafungwa wakati wa vita, wengine walitolewa na familia zao kama rahani ya deni, wengine walizaliwa watumwa, wengine kuhukumiwa utumwani kwa makosa fulani[1].

Walinunuliwa na mfalme Siaka aliyeuza kila mwaka watumwa 2000 hivi kwa wafanayabiashara Wazungu waliowapeleka kwenye visiwa vya Karibi na nchi za Amerika Kusini. Wakati ule kusafirisha watumwa kutoka Afrika iliwahi kupigwa marufuku kwa njia ya mikataba kati ya nchi za Ulaya na Marekani. Hasa jeshi la maji la Uingereza lilijaribu kukamata wafanyabiashara wa watumwa baharini kwa hiyo kisheria biashara hiyo ilitazamiwa kama magendo ya kijinai. Hata hivyo, serikali za nchi za Amerika Kusini na za Karibi ambako uchumi bado ulitegemea kazi ya watumwa zilifunga macho na kuvumilia biashara hiyo haramu.

Wafungwa waliofika baadaye kwenye Amistad waliuzwa pamoja kundi la mateka 500 kwa mfanya biashara Mhispania Pedro Blanco na kupelekwa Kuba kwenye jahazi ya watumwa Teçora kutoka Ureno. Takriban theluthi moja wa wafungwa walikufa njiani.

Wamiliki Wahispania wawili wa mashamba ya miwa, Don José Ruiz na Don Pedro Montes, walinunua mateka 53, pamoja na watoto wanne, huko Havana, Kuba na walikuwa wakiwasafirisha kwenye jahazi La Amistad kwenda kwenye mashamba yao karibu na Puerto Príncipe ( Camagüey ya kisasa, Kuba). [2] Uasi ulianza wakati wa safari hiyo. Sengbe Pieh, mtu wa Mende, aliyejulikana baadaye pia kama Joseph Cinqué, alijifungua mwenyewe na wengine siku ya tatu na kuanza uasi. [3] Walichukua udhibiti wa meli, wakimuua nahodha na mpishi. Katika mapigano hayo, Waafrika watatu waliuawa pia.

Wanunuzi wa mateka Ruiz na Montes walifungwa kwenye jahazi na Pieh aliwaamuru kuendesha chombo kwenda Afrika. Badala yake, Ruiz na Montes walisafiri kuelekea kaskazini, kuelekea pwani la mashariki mwa Marekani, wakiwa na hakika kwamba meli hiyo ingezuiliwa, na Waafrika wangerudishwa Kuba wakiwa watumwa.

Manowari ndogo ya idara ya forodha ya Marekani ilikamata Amistad karibu na Long Island, New York. Pieh na kikundi chake walitoroka kwenye jahazi lakini walikamatwa pwani na raia. Walikuwa wamefungwa katika New Haven, Connecticut, kwa mashtaka ya mauaji na uharamia. Mtu aliyemkamata Pieh na kikundi chake aliwadai kama mali yake. La Amistad ilivutwa hadi New London, Connecticut, na wale waliobaki kwenye chombo walikamatwa. Hakuna hata mmoja wa manusura 43 kwenye meli hiyo aliyezungumza Kiingereza, kwa hivyo hawakuweza kuelezea ni nini kilifanyika. Hatimaye profesa wa lugha Josiah Gibbs alimpata mkalimani, James Covey, na akajifunza juu ya utekaji nyara wao.

Kesi za Amistad hariri

Kesi mbili zilifunguliwa mahakamani.

Kesi ya kwanza ililetwa na maafisa wa manowari ya forodha waliodai kulingana na desturi za siku zile eti wana haki ya kumiliki jahazi waliyookoa kutoka maharamia, pamoja na mzigo wake, yaani watumwa.

Katika kesi ya pili, jimbo la Connecticut lilishtaki Wahispania wawili Ruiz na Montes kuwatumikisha Waafrika huru. Serikali ya Hispania ilimwomba Rais wa Marekani Martin Van Buren awarudishe mateka wa Kiafrika kwa Kuba chini ya mkataba wa kimataifa kwa madai walikuwa watumwa halali waliozaliwa watumwa huko Kuba.

Hatimaye kesi iliamuliwa na Mahakama Kuu ya Marekani iliyotoa hukumu kuwa mateka walichukuliwa kutoka Afrika dhidi ya sheria za Marekani na za Hispania, na pia dhidi ya mikataba ya kimataifa. Kwa hiyo wote walipata uhuru wao tena. Watu 35 walirudi Afrika miaka miwili baadaye wakisaidiwa usafiri na shirika ya misioni.[4]

 
Uchapishaji wa Cinqué ambao ulionekana katika The Sun mnamo Agosti 31, 1839

Miaka ya baadaye hariri

Baada ya kutunzwa nyuma ya Jumba la Ushuru huko New London, Connecticut, kwa mwaka mmoja na nusu, La Amistad ilipigwa mnada mnamo Oktoba 1840. Ilinunuliwa na nahodha Hawford aliyeipa jina jipya la Ion . Mwisho wa 1841, alisafiri kwa meli Ion kwenda Bermuda na Saint Thomas na shehena ya vitunguu, tufaha, kuku hai na jibini.

Baada ya kusafiri Ion kwa miaka michache, Hawford aliiuza huko Guadeloupe mnamo 1844.  Hakuna habari zaidi ya kile kilichotokea baadaye.

Kati ya 1998 na 2000, mafundi katika bandari ya Mystic, Connecticut, waliunda mfano wa La Amistad, wakitumia ustadi wa jadi na mbinu za ujenzi zilizozoeleka kwa jahazi za mbao zilizojengwa katika karne ya 19..Jahazi hiyo mpya ilitangazwa kama "Freedom Schooner Amistad ". [5] [6] Jahazi hiyo mpya sio mfano kamili wa La Amistad, kwani ni ndefu kidogo na ina bodi ya juu zaidi.

Siku hizi iko kwenye bandari ya New Haven, Connecticut. Kutoka hapa inafanya safari fupi za kielimu baharini. Safari hizo ni hasa kwa wanafunzi wanaosikia historia na kujifunza kuhusu utumwa na ubaguzi wa kisasa.

Marejeo hariri

  1. History of the Amistad Captives, page 9 ff
  2. "Teaching With Documents:The Amistad Case". National Archives and Records Administration. Iliwekwa mnamo March 14, 2013.  Check date values in: |accessdate= (help)
  3. Purdy, Elizabeth. Encyclopedia of African American History, 1619–1895: From the Colonial Period to the Age of Frederick Douglass. Oxford African American Studies Center. ku. Amistad. 
  4. https://www.wdl.org/en/item/3080/
  5. "Amistad". Coast Guard Vessel Documentation. NOAA Fisheries. Iliwekwa mnamo January 14, 2017.  Check date values in: |accessdate= (help)
  6. Marder, Alfred L. "About the Freedom Schooner Amistad". Amistad Committee, Inc. Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2021-08-11. Iliwekwa mnamo January 14, 2017.  Check date values in: |accessdate= (help)

Viungo vya nje hariri