Mto Msimbazi (Dar es Salaam)

Msimbazi ni kati ya mito ya mkoa wa Dar es Salaam (Tanzania Mashariki) ambao maji yake yanaishia katika Bahari Hindi.

Beseni la mto Msimbazi jijini Dar es Salaam.

Njia ya mto hariri

Chanzo chake kinapatikana katika vilima vya Pugu, upande wa kaskazini wa Kisarawe. Njia yake ni km 42.5 hadi mdomo wake kwenye daraja la Selander. Mto Msimbazi unapitia eneo lote la Dar es Salaam ikiwa ni mto mkuu wa jiji hili. Mafuriko yake yanaathiri maisha ya watu wengi mara kwa mara.

Matawimito makubwa zaidi ni Sinza (Ng'ombe) (urefu km 19.5), Ubungo (km 20) na Luhanga (km 12.15)[1], pamoja na matawimito midogo kama vile Mambizi (km 6.5), Zimbire (km 3.6), Kimanga (km 3), Kinyenyele (km 4.35) na Kwangula (km 2.25)[2].

Machafuko hariri

Mto huo una viwango vikubwa vya uchafu, hasa kutokana na kuwepo kwa metali nzito zinazotokana na viwanda na ambazo ni sumu; sumu nyingine zinazidi kutoka kwenye majalala ya takataka ya Vingunguti zikipelekwa na maji ya mvua mtoni.

Machinjio makubwa kando ya mto yanaongeza uchafuzi. Vyanzo vingine ni vyoo vya shimo vinavyotumiwa na idadi kubwa ya wakazi.

Bonde la mto ambalo ni kavu sehemu kubwa ya mwaka ni sehemu ya kumwaga takataka kwa wakazi wa karibu.

Shughuli za kilimo huongeza tatizo kwa kutumia samadi na mbolea za chumvi. Maji ya mto Msimbazi hayafai kwa matumizi ya binadamu hata hayafai kwa matumizi ya kilimo cha mazao.[3] Mboga za majani kutoka bustani mbalimbali za bonde la Msimbazi, pia kutoka masoko ya eneo hilo, zilipimwa na kuonekana kuwa na viini vingi hatari vya magonjwa, kama vile "Escherichia coli, Citrobacter ssp, Proteus ssp, Klebsiella ssp, Salmonella spp na Basillus spp"[4]

Tazama pia hariri

Tanbihi hariri

  1. [https://www.researchgate.net/publication/329706184 Malale/Munishi, Surface Water Quality in the Peri-Urban Areas in Dar-Es_Salaam, Tanzania: The case of Ng’ombe River], Tanzania Jornal of Engineering and Technology, vol 37, June 2018, pp 37ff
  2. W. J. S. Mwegoha and C. Kihampa: Heavy metal contamination in agricultural soils and water in Dar es Salaam city, Tanzania, African Journal of Environmental Science and Technology Vol. 4(11), pp. 763-769, November, 2010, online hapa
  3. Tanzania – Msimbazi River Action Network, tovuti ya pureearth.org (zamani Blacksmith Institute, New York), iliangaliwa Desemba 2019
  4. Mary C. Kayombo, Aloyce W. Mayo . "Assessment of Microbial Quality of Vegetables Irrigated with Polluted Waters in Dar es Salaam City, Tanzania." Environment and Ecology Research 6.4 (2018) 229 - 239. doi: 10.13189/eer.2018.060403

Viungo vya nje hariri