Rudolf Christian Karl Diesel (18 Machi 1858 - 30 Septemba 1913) alikuwa mhandisi na mvumbuzi kutoka nchini Ujerumani. Uvumbuzi wake unaojulikana zaidi ni injini ya dizeli.

Rudolf Diesel.

Alizaliwa huko Paris akiwa mtoto wa wahamiaji Wajerumani; familia ilipaswa kurudi Ujerumani wakati wa Vita ya Kifaransa-Kijerumani ya 1870.

Baada ya kumaliza shule alipenda kuwa mhandisi akafaulu kupata msaada wa masomo akaingia katika chuo cha ufundi cha Bavaria pale Munich alipohitimu mwaka 1880. Alianza kazi katika kampuni ya profesa wake wa awali, Carl von Linde, alipobuni na kutengeneza hasa mashine ya kupoza. Pamoja na hayo alianza kazi yake ya injini ya mwako wa ndani yenye shinikizo kubwa.

Alikuwa na wazo la kuunda injini ambayo ilitegemea ukandamizaji mkubwa wa fueli (mafuta) ili kuiwasha. Na hii angeweza kufanya bila cheche. Mbinu unaotumia cheche ulibuniwa tayari na Nikolaus Otto aliyeunda injini ya mwako ndani.

Mnamo 1892 alipata hakimiliki ya injini yake na mwaka 1896 injini ya kwanza ya dizeli ilipatikana iliyoendelea jinsi alivyotaka.

Injini ya dizeli iliendelea kutengenezwa kwa milioni nyingi; ilikuwa hasa injini ya kuendesha vyombo vikubwa kama vile meli na malori; maendeleo ya teknolojia yameleta pia injini ndogo.

Diesel alipata pesa nyingi kutokana na leseni kwa uvumbuzi wake.

Makala hii kuhusu mwanasayansi fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Rudolf Diesel kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.