Muumba

(Elekezwa kutoka Mwumba)

Muumba ni sifa mojawapo ya Mwenyezi Mungu, kutokana na imani ya kwamba ndiye aliyesababisha vyote vianze na vidumu kuwepo.

Imani hiyo katika Uyahudi na Ukristo inafafanua kwamba Mungu pekee ndiye aliyetokeza viumbe vyote kutoka utovu wa vyote.

Katika dini zisizomsadiki Mungu mmoja tu, kazi ya uumbaji inafikiriwa kutokana na wahusika zaidi ya mmoja.

Katika Biblia hariri

Kadiri ya Biblia, asili ya uhai wote ni Mwenyezi Mungu. “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi” (Mwa 1:1).

Mungu aliumba vyote kwa kutaka tu, bila kutumia chochote. “Nakusihi, mwanangu, inua macho yako utazame mbingu na nchi, ukaone vitu vyote vilivyomo; fahamu kwamba Mungu hakuviumba kwa vitu vilivyokuwapo. Na ndivyo alivyofanya wanadamu pia” (2Mak 7:28). Anaambiwa: “Najua ya kuwa waweza kufanya mambo yote, na ya kuwa makusudi yako hayawezi kuzuilika” (Ayu 42:2).

Mungu aliumba vyote bila kulazimika, kusudi tu adhihirishe na kushirikisha utukufu wake. “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake” (Zab 19:1). “Kwa kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu una yeye milele. Amina” (Rom 11:36).

Baada ya kuumba, Mungu anazidi kushughulikia viumbe vyake, akividumisha na kuviongoza vyote vifikie lengo alilovipangia. “Ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda na kuwa na uhai wetu” (Mdo 17:28). Tunamtegemea pande zote: angetuacha kidogo tungetoweka mara. Yesu alipolaumiwa kwa kuponya watu siku ya pumziko, alijitetea kwamba, “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi” (Yoh 5:17). “Yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu” (1Pet 5:7).

Ikiwa Mungu anatushughulikia, tunapaswa kujiachilia mikononi mwake kwa moyo wa kitoto, tukiwajibika bila mahangaiko yanayowapata watu wasiomjua. “Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je, si bora kupita hao?” (Math 6:26). “Nawe una nini usichokipokea?” (1Kor 4:7). “Nimrudishie Bwana nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?” (Zab 116:12).

Mungu akiwa wema mkuu na mwenye uwezo wote, hakuumba ubaya wowote. Tena kila anapovumilia ule uliosababishwa na viumbe vyenye hiari (malaika na binadamu) anaufanya uzae mema makubwa zaidi kwa njia tusizoweza kuzifahamu vizuri hapa duniani. “Mimi ni Yusufu, ndugu yenu, ambaye mliniuza kwenda Misri. Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa kuniuza huku; maana Mungu alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu… Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo” (Mwa 45:4-5; 50:20).

Viungo vya nje hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.