Ugaidi (kutoka Kiar. غيظ ghaiz kwa maana ya hasira[1]) ni hasa mfumo wa kulenga mabadiliko ya kisiasa kwa kutisha watu kwa njia ya vurugu au mauaji. Matendo ya kigaidi yanatisha kwa sababu watu wanajeruhiwa au kuuawa. Watendaji wa ugaidi kwa kawaida ni vikundi au watu wasio na cheo au nafasi rasmi.

Mashambulio ya kigaidi New York, 11 Septemba 2001.

Mara nyingi si rahisi kutofautisha kati ya magaidi, wapigania uhuru au watu wanaoendesha vita ya msituni. Hata jeshi rasmi ya serikali linaweza kutumia mbinu za kigaidi lakini kwa kawaida hawahesabiwi kati ya magaidi.

Mfano wa tendo la kigaidi hariri

Tarehe 7 Agosti 1998 kundi la Al-Qaida lililipua mabomu kwenye balozi za Marekani majijini Nairobi na Dar es Salaam. Watu 223 walikufa na zaidi ya 4,100 walijeruhiwa. Kwa njia hiyo Al-Qaida ilitaka kupinga matendo ya Marekani katika Somalia. Kuna madokezo ya kwamba shabaha ya nyongeza ilikuwa kusababisha mashambulio ya Marekani dhidi ya Afghanistan ambako Al-Qaida ilikuwa na kimbilio. Lakini inasemekana ya kwamba viongozi waliogopa majadiliano kati ya makampuni ya Kimarekani na serikali ya Taliban nchini Afghanistan na mashambulio dhidi ya balozi yalilenga kuvuruga majadiliano yale na hivyo kuimarisha kimbilio kwa Al-Qaida. Kundi la Al-Qaida haikusikia uadui dhidi ya watu wa Tanzania au Kenya lakini haikusita kuwaua wengi kwa kutimiza shabaha yake ya kutisha serikali ya Marekani.

Marejeo hariri

  1. linganisha Sacleux, Dictionnaire Swahili-Francais, Paris 1939, "Gaizi"