Wandali ni kabila linalopatikana hasa kusini magharibi mwa nchi ya Tanzania, katika Wilaya ya Ileje, Mkoa wa Songwe. Kabla mkoa huo haujaanzishwa ilikuwa wilaya ya mkoa wa Mbeya. Pia wako nchini Malawi.

Ni kabila la watu wapole na wakarimu sana kwa wageni, pia lenye juhudi sana kwa kazi za mikono, mathalani, kulima kwa jembe la mikono na kupasua mbao kwa msumeno wa mikono.

Hii pia inachangiwa kwa kiasi kikubwa na jiografia ya wilaya hiyo kuwa na miinuko mingi kwa sehemu kubwa, hasa kwa ukanda wa Undali yaani ukanda ambao wilaya ya Ileje inapakana na wilaya ya Rungwe na wilaya ya Kyela.

Wanadumisha sana lugha yao, ambayo inaitwa Kindali na inafanana na Kinyakyusa. Hii ni kwa sababu kabila la Wandali kwa asili, historia ya masimulizi ya watu wa zamani inaonyesha kuwa na chimbuko moja na kabila la Wanyakyusa. Tofauti kati ya makabila hayo mawili hutokana na utengano wa watu wa zamani kijiografia tu.

Wanawake wa Kindali ni watu wastaarabu sana, wachapakazi na wenye mapenzi ya kweli na dhati: pesa kwao ni hitaji la mwisho kabisa baada ya namba moja ambayo ni mapendo.

Upande wa dini wengi wao ni Wakristo, hasa wa madhehebu ya Wamoravian.

Chakula chao kikuu ni ugali wa mahindi, pamoja na ndizi, maparachichi na magimbi bila kusahau viazi vitamu na mihogo. Pia hujishughulisha na ufugaji wa ng'ombe, mbuzi, kondoo na kuku, na ususi wa nyungo ambao umekuwa sehemu muhimu ya biashara ndani na nje ya mkoa.

Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wandali kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.