Coordinates: 6°53′59″S 39°48′17″E / 6.8996158°S 39.8048396°E / -6.8996158; 39.8048396


Fungu Kizimkazi ni kisiwa kidogo katika Bahari Hindi ambacho ni sehemu ya Zanzibar kinachojulikana pia kwa majina ya Latham Island na Fungu Mbaraka[1]. Hakuna wakazi.

Mahali pa Fungu Kizimkazi (Kisiwa cha Latham) mbele ya pwani ya Tanzania.

Tabia hariri

Inahesabiwa kuwa sehemu ya funguvisiwa la Zanzibar (Tanzania). Kipenyo chake ni takriban mita 300. Kipo kilomita 64 upande wa kusini-mashariki kutoka Unguja, na mahali pa karibu kwenye bara ni Kimbiji katika Wilaya ya Kigamboni, Dar es Salaam.

Hakuna wakazi wala maji matamu hapa. Viumbe vya pekee ni ndege wala samaki wanaounda hapa viota na kulea vinda wao. Hivyo kisiwa chote kimefunikwa na guano (mavi ya ndege).

Kisiwa kinainuliwa mita 3 pekee juu ya uwiano wa bahari hakionekani vema ni hatari kwa meli[2].

Kulikuwa na majaribio ya kupunguza hatari na kuboresha mwonekano wa kisiwa kwa kujenga alama iliyoinuliwa au kupanda miti iliyoharibika tena na ndege.[3]

Majina hariri

Jina la Latham linatokana ya jahazi ya Kampuni ya Kiingereza kwa Uhindi wa Mashariki yenye jina "Latham" iliyopita hapa mnamo mwaka 1798 na kuacha taarifa ya kimaandishi[4]. Hata hivyo habari hii ilichukuliwa pia kwa maana kwamba Mhindi mwenye jina la "Latham" alikuta kisiwa na kukipa jina.[5]

Wavuvi wa sehemu hizi za Bahari Hindi hutumia majina mbalimbali hasa Fungu Mbaraka na Fungu Kizimkazi. Jina la Mbaraka linatokana na Mzanzibari Mbaruk au Mbaraka aliyepata kibali cha sultani Seyyid Bargash kukusanya mabaki ya meli zilizokwama hapa zikigonga miamba.[6] Hii ni habari ya kwanza kwamba Zanzibar alidai utawala wa Fungu Kizimkazi.

Utawala hariri

Kisiwa hiki kiliingizwa rasmi katika Usultani wa Zanzibar mnamo mwaka 1898 wakati bendera ya sultani ilipelekwa hapa[7].

Lakini katika miaka mnamo 1910/1912 kulikuwa na mabishano baina ya mwakilishi Mwingereza huko Zanzibar kwa niaba ya sultani na ofisi ya gavana Mjerumani pale Dar es Salaam kuhusu mamlaka juu ya Latham Island, hasa usimamizi wa uvunaji wa guano ya ndege. Tarehe 11 Aprili kaimu gavana Wilhelm Methner alitembelea kisiwa wakati wa kurudi Dar es Salaam kutoka kusini ya koloni[8]. Mzozo ulikwisha na tokeo la Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia na kuondolewa kwa Ujerumani katika Afrika ya Mashariki. Mwaka 1924 kisiwa kilitajwa kuwa sehemu ya mbali ya usultani wa Zanzibar[9].

Mnamo mwaka 2011 kulikuwa na taarifa ya kutokea kwa uvutano baina ya ofisi za serikali ya Zanzibar na Tanzania bara kuhusu mamlaka juu ya kisiwa hiki[10][11].

Kwa mtazamo wa Zanzibar ni sehemu ya Mkoa wa Unguja Kusini.

Tazama pia hariri

Marejeo hariri

  1. Latham Island sa Geonames.org (cc-by); post updated 2012-01-17; database download sa 2017-01-30
  2. Hydrographic Office, Admiralty (1878), The Africa Pilot: South and east coasts of Africa, from the Cape of Good Hope to Cape Guardafui, including the islands in Mozambique Channel. Part III, ukurasa 302 f online hapa
  3. Harold Ingrams (1998) Arabia & The Isles, p. 60, ISBN 13:978-0-7103-0567-1, online hapa kwa archive.org
  4. Hydrographic Office, Admiralty (1878), The Africa Pilot
  5. [1]M. D. Gwynne, I. S. C. Parker and D. G. Wood: Latham Island: An Ecological Note, The Geographical Journal, Vol. 136, No. 2 (Jun., 1970), pp. 247-251, iliangaliwa kupitia Jstor mwezi wa Aprili 2019
  6. Gwynne & alii (1970)
  7. Gwynne & alii (1970)
  8. Under Three Governors (Unter drei Gouverneuren) The Memoirs of a German Colonial Official in Tanzania 1902-1917 by Wilhelm Methner translated into English with an introduction by John East, 2019, ukurasa 282,
  9. Harold Ingrams (1998) Arabia & The Isles, p. 60
  10. Taarifa ya wavuwi kuhusu uvutano baina ya Zanzibar na bara kuhusu sheria za uvuwi. Jalada kutoka ya awali juu ya 2018-12-20. Iliwekwa mnamo 2019-02-06.
  11. linganisha pia mchango mrefu kwenye facebook ya mwaka 2016 kuhusu swali la mamlaka juu ya Kisiwa cha Latham

Viungo vya nje hariri