Ulaji mboga

(Elekezwa kutoka Vegetarianism)

Ulaji mboga (kwa Kiingereza: vegetarianism) ni namna ya maisha inayoepuka vyakula vinavyotokana na wanyama waliouawa, kama vile nyama na samaki.

Vyakula vya mbogamboga
Vyakula vya tofu huwa na protini nyingi
Soko la Kinhindi la vyakula vya mbogamboga

Watu wanaokataa kula nyama huitwa wala mboga (vegetarians), wakitumia mboga, matunda, majani, nafaka, jozi na mbegu mbalimbali.

Mara nyingi azimio kwa ajili ya ulaji mboga ni la kidini, kifalsafa au kwa namna nyingine kimaadili.

  • katika dini za Ujain na Uhindu, waumini hupewa moyo kuachana na nyama kama chakula. Katika imani yao uhai wote duniani ni mmoja. Kila nafsi huzaliwa upya, ama kama binadamu au kama mnyama, kwa hiyo mauaji hayana tofauti kama yanahusu binadamu au mnyama, ni kosa na dhambi.
  • wako pia Wakristo wanaoamini kwamba ulaji nyama si hali iliyolengwa na Mungu katika uumbaji, hasa wakirejelea maandiko kama Mwanzo 1:29 ambako Mungu anataja majani pekee kama chakula kwa binadamu na wanyama
  • bila marejeo ya kidini kuna watu wanaosikia kuwa hawana haki ya kutesa viumbehai na kuwaua kwa chakula
  • wako pia walaji mboga wanaokataa nyama kwenye msingi wa hifadhi ya mazingira; wanaona ufugaji wa wanyama kwa shabaha ya kuzalisha nyama kama chakula husababisha uharibifu mwingi wa mazingira; wanaona pia swali la haki ya kibinadamu wakiona kuongezeka kwa ulaji nyama unasababisha njaa kati ya maskini, maana mashamba mengi duniani hulenga kuzalisha lishe ya mifugo kwa kuichinja

Kati ya wala mboga kuna makundi tofauti; wengine wanatumia maziwa, asali na mayai kwa sababu matumizi ya vitu hivi hayajumlishi mateso na mauaji.

Wako pia wala mboga wakali zaidi wanaojiita Vegan ambao wanakataa chakula chochote chenye asili katika viumbehai.

Idadi kubwa ya wala mboga wako Uhindi, kwa jumla hukadiriwa kwamba asilimia 20 ya Wahindu wote hawali nyama. Kwa msingi huo upishi wa Kihindi una chaguo kubwa sana ya vyakula vitamu visivyo na nyama. Tangu karne ya 19 ulaji mboga umeanza kuenea pia kati ya watu wenye utamaduni wa Kizungu, lakini hadi sasa idadi yao bado iko chini ya asilimia 10 ya jamii za Ulaya au Marekani.

Hata hivyo, wasiwasi kuhusu ulaji nyama umesababisha kuongezeka kwa soko kwa vyakula visivyo na nyama.

Marejeo hariri

Viungo vya Nje hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya utamaduni bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Ulaji mboga kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.