Wanyaturu (au Waturu; wao hupendelea kuitwa Arimi, yaani watu wa Rimi [1]) ni kabila la watu wa Tanzania wanaoishi hasa katika Mkoa wa Singida.

Shujaa wa Kinyaturu

Lugha yao ni Kinyaturu, ambayo kwa sehemu ina matamshi ya Kibantu, ingawa ina fonimu nyingi za Kikushi. Hii inaweza kuwa kwa sababu ya muingiliano wa karibu na majirani zao Wanyatunzu (watu wa kaskazini magharibi) na Wanyiramba wa maeneo ya jirani ambao ni Bantu asili.

Wana utani na Wanyiramba na Wairaqw.

Asilimia kubwa ya Wanyaturu wa sasa ni weupe: hii ni kutokana na miingiliano yao na Waarabu na kupelekea kuzaliwa machotara wengi.

Wanyaturu wengi ni Waislamu na Wakristo, kwa jumla ni wachamungu kwani ni watu wanaojua kuishika dini vizuri na kupenda ibada.

Wanyaturu wanajua sana kulinda ardhi yao kwani ni vigumu Mnyaturu kuuza ardhi yake kwa mtu ambaye si Mnyaturu.

Historia

Asili ya kabila hilo inasemekana ni nchi ya Ethiopia ambako kunasadikiwa kuwa na watu wanaotumia lugha ambayo kwa asilimia kubwa inafanana na Kinyaturu. Hudhaniwa pia kuwa Wanyaturu na Wakushi wa Ethiopia asili yao ni moja.

Walipoingia eneo la Tanganyika walichangamana na Wanyatunzu pamoja na Wasukuma, ndiyo maana mila na tamaduni zao zinashabihiana kwa kiasi kikubwa, hivi kwamba ni vigumu kumpambanua Mnyaturu na Wanyatunzu. Mpaka miaka ya 1980 Wanyaturu wengi sura na nywele zao, hasa kina mama, zilishabihiana sana na watu wa jamii ya Waoromo wa Ethiopia, na walipenda sana kujiita ni Wahabeshi. Hii ni kutokana na kuwafahamu watu wa jamii ya Kihabeshi.

Idadi na mgawanyiko

Mwaka 1993 walikuwa 556,000 [1].

Ndani ya kabila hilo, kuna makundi matatu:

  • Vahi (Wahi), ambao ni zaidi ya nusu ya Wanyaturu wote, na kuwa wenyeji wa mji wa Singida: hao wanaishi kuanzia Singida mjini hadi karibu na wilaya ya Manyoni;
  • Airwana (Wilwana) wanaishi kaskazini kwa ziwa Singida;[2]
  • Anyiŋanyi (Wanyinganyi) wanaishi maeneo ya Mnying'anyi;maeneo hayo ni kama vijiji vya Mgori, Pohama na maeneo yazungukayo sehemu hizo. Ni kundi dogo zaidi na lile linalozidi kupotea kwa kasi ukilinganisha na mengine. Kwa ujumla Wanyaturu halisi wanaojua lugha yao halisi wanazidi kupotea kutokana na kuchanganya matamshi ya Kiswahili na Kinyaturu chenyewe.

Kuna historia pia ya koo mbalimbali kama Unyanjoka ambao waliongoza sehemu za Wilwana. Ukoo wa Unyanjoka unaanzia Ikhangao na Ndaang'ongo, Ilongero hadi Mtinko na Mpambaa.

Unyambwa ni sehemu iliyoko Singida na inasemekana ni ukoo mkubwa sana wenye mababu wakubwa wawili: Ghambona na Hante. Ukoo huo hauvumi sana kutokana na watoto wa wazee hao kuhama Unyambwa na kwenda Iguguno, ambako lakini hawakukaa sana, wakahama tena na kuelekea hasa mikoa jirani kama Shinyanga, Tabora na Mwanza. Ni ukoo wenye watoto wengi wa kike kuliko wa kiume, na dini yao kubwa ni Uislamu.

Tanbihi

  1. Pengine jina "Wanyaturu" linapoteza historia yao kwani liliundwa na Wazungu
  2. Unaweza kubadilisha hapa kuhusu Airwana kuwa si wengi karibu nusu ya Wanyaturu wote kwa ukianzia pale mjini Singida ukielekea Kusini hadi sehemu za Issuna hadi Itigi na Manyoni hadi Kintinku hawa ni Vahi tu, bado sijasema sehemu za Ihanja hadi Muhintiri na sehemu za Mang'onyi na Misughaa ni vahi au wahi kwa hiyo robo tatu ya wanyaturu ni wahi yaani vahi waweza kufanya utafiti na utagundua ukweli huo. wairwana wana maeneo kuelekea Kaskazini ambayo ni sehemu ndogo sana kieneo na inapakana na Wanyiramba ukifika sehemu za Iguguno.
  Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wanyaturu kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.