Attila (406-453), alikuwa kiongozi wa Wahunni kutoka mwaka 434 hadi alipofariki mnamo 453. Alisimamia himaya iliyounganisha makabila mbalimbali kama vile Waostrogoti, Waalani, Wabulgari na wengineo katika Ulaya ya Kati na ya Mashariki.

Himaya ya Wahuni katika Ulaya wakati wa Attila

Attila alipigana katika vita nyingi na majirani. Madola makubwa yaliyokuwa majirani yake yalikuwa Uajemi, Roma ya Mashariki na Roma ya Magharibi. Wakati ule Dola la Roma lilikuwa bado na umoja fulani lakini hali halisi kulikuwa na serikali tofauti mashariki na magharibi.

Attila alirithi uongozi wa Wahunni pamoja na kaka yake Bleda baada ya kifo cha baba yao Rugila mnamo mwaka 434. Rugila aliwahi kufaulu kuunganisha Wahunni wote. Bleda na Attila walitisha Waroma wa Mashariki na serikali ya Bizanti ilikubali kuwalipa ruzuku wa pauni 700 za dhahabu kila mwaka.

Hapo kaka hao waliongoza jeshi lao kushambulia Uajemi lakini walishindwa.

Mwaka 440 walionekana tena kwenye mpaka wa Dola la Roma wakaushambulia kwa nguvu mwaka 443. Walishindwa kuvunja kuta za Bizanti lakini serikali ya Roma ya Mashariki iliona vema kuwalipa kwa amani kiasi cha pauni 2000 za dhahabu kwa mwaka.

Baada ya ushindi huo Bleda alikufa mnamo 445. Waandishi wengine wa kale walisema Attila alimwua.

Vita kadhaa na Roma ya Mashariki vilifuata.

Mwaka 450 Attila aliangalia hali ya Gallia (leo: Ufaransa), jimbo la Roma ya Magharibi. Inasemekana dada wa Kaizari Valentinian III aliozwa huko dhidi ya mapenzi yake akamwandikia Attila barua na kuomba msaada wake. Kwa namna yoyote jeshi la Attila lilielekea Gallia. Gallia ilitawaliwa na gavana Mroma Aetius aliyekusanya jeshi la askari Waroma wachache aliokuwa nao pamoja na askari kutoka makabila ya Kigermanik katika Gallia waliowahi kuingia katika harakati za uhamaji wa mataifa mazima ambako makabila ya Wagermanik walielekea magharibi na kusini na kuingia katika Dola la Roma. Jeshi hilo la Kiroma-Kigermanik lilikutana na jeshi la Attila mwaka 451 kwenye uwanja wa Katalauni[1] Hapa alikutana na jeshi la Kiroma akashindwa[2].

Kutoka Ufaransa Attila alivamia Italia ya kaskazini akarudi katika ikulu yake iliyopatikana katika maeneo ya Hungaria ya leo. Mwaka 453 aliamua kumwoa binti lakini alikufa kwenye sherehe ya arusi.

Baada ya kifo chake makabila ya Kigermanik yaliyowahi kuwa chini yake yaliasi. Katika mapigano Wahunni walishindwa. Baada ya kushindwa tena katika mapigano na Roma ya Mashariki umoja wa Wahunni uliporomoka kabisa. Walipotea na baada ya muda mdogo hawakutajwa tena katika maandiko ya kale, isipokuwa katika kumbukumbu ya vita zao za awali.

Marejeo hariri

  1. Wataalamu wanatafuta mahali pake katika Ufaransa ya Magharibi, ama karibu na mji wa Troyes au karibu na Châlons-en-Champagne.
  2. Article on Britannica.

Kujisomea hariri

Viungo vya Nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu: