Dizasta Vina

Mwanamuziki, mwandishi wa nyimbo na mtayarishaji wa muziki kutoka Tanzania

Edger Vicent Mwaipeta (anafahamika zaidi kwa jina la kisanii kama Dizasta Vina; amezaliwa 17 Februari 1993) ni msanii wa muziki wa Hip Hop na mtayarishaji wa muziki kutoka Mbeya, Tanzania.[1] [2]

Dizasta Vina
Dizasta Vina akiwa Stejini—Septemba 2018, Dar es Salaam,Tanzania.
Taarifa za awali
Jina la kuzaliwaEdger Vicent Mwaipeta
Pia anajulikana kamaFundi Vina, The Black Maradona, Professor Tungo
Amezaliwa17 Februari 1993 (1993-02-17) (umri 31)
Iringa, Tanzania
ChimbukoMbeya, Tanzania
Aina ya muzikiHip hop
Kazi yakeRapa, Mtunzi, Mshairi, Mtayarishaji wa rekodi
AlaSauti, Kinanda
Miaka ya kazi2012 - sasa
StudioPanorama Authentik
Ameshirikiana naBaraka the Prince, G Nako, One The Incredible, Nikki Mbishi, Nash MC, JCB wa Watengwa

Ni msanii ambaye muundo wa mashairi yake unajumuisha usimuliaji wa matukio na hadithi za maisha halisi ya jamii aliyotokea. Tungo zake zinasifika kwa kuelimisha na kugusa mausula ya kijamii kama vile malezi, maradhi, siasa, umasikini, elimu, haki na usawa, uraibu wa madawa ya kulevya na masuala mengine ndani na nje ya jamii na taifa lake na ulimwengu mzima kwa jumla.[3]

Alianza kurap mnamo mwaka wa 2007 kwa kushiriki katika mashindano mbalimbali ikiwa ni pamoja na SM Straight Music Freestyle Battle mwaka wa 2010 mkoani Iringa. Mashindano haya yalimjenga kisanaa na baadaye alijiunga na Tamaduni Muzik kupitia shindano la utafutaji wa vipaji. Mnamo mwaka wa 2012 alianza kupata umaarufu kwenye tasnia ya muziki nchini Tanzania, baada ya kutoa wimbo uliokwenda kwa jina la "Harder".[4]

Mnamo mwaka wa 2017, alitoa kandamseto yake ya kwanza "The Wonderboy Mixtape". Aliachia nyimbo kadhaa na kufanikiwa kutoa albamu yake ya kwanza "JESUSta" mwaka wa 2018. Mnamo tarehe 27 Desemba 2020, alitoa albamu yake ya pili "The Verteller".[5] Kando na kutoa nyimbo, Dizasta amekuwa akifanya utayarishaji wa nyimbo zake, hii ni baada ya kuamua kukaa chini na kuanza kusoma namna ya kutayarisha muziki na kufanya uhandisi wa sauti.

Maisha ya awali na elimu hariri

Dizasta Vina ni mtoto wa pili kuzaliwa katika familia yake na ni mwanaume pekee akiwa na dada zake wawili, alizaliwa mnamo tarehe 17 Februari 1993. Ingawa kiasili ni Mnyakyusa kutoka Mbeya (mkoa uliopo Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania) alizaliwa mkoa wa Iringa kabla ya wazazi wake kuhamia Dar es Salaam ambako alianza masomo yake ya awali.

Elimu yake ya msingi aliipata katika shule ya msingi ya "Kimanga" iliyopo wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam aliandikishwa katika shule hiyo mnamo mwaka wa 2000. Mwaka wa 2007 alijiunga na elimu ya sekondari katika shule binafsi ya "White Lake High School" iliyopo eneo la Changanyikeni jijini Dar es Salaam kisha kumaliza masomo ya sekondari katika shule ya "Southern Highlands Secondary School" iliyopo Soweto jijini Mbeya — mnamo mwaka wa 2O1O. Aliendelea na kidato cha tano katika shule ya "Kigoma High School" mkoani Kigoma ambapo alisoma kwa muda wa miezi minne tu kabla ya kumalizia masomo yake ya elimu ya sekondari katika shule ya "Mbeya High School". Dizasta alijiunga na masomo ya elimu ya juu mwaka wa 2013 katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) kilichopo jijini Dar es Salaam na kusoma shahada ya kwanza ya uhasibu.

Kazi ya muziki hariri

 
Dizasta vina katika Pozi — 2019.

Dizasta Vina amezaliwa katika familia inayopenda muziki na alianza kufuatilia muziki tangu akiwa na umri mdogo. Msukumo wa kuupenda muziki aliupata kutoka kwa familia yake. Mama yake alikuwa mwimbaji wa kwaya kanisani na pia kwa vipindi tofauti dada zake walijiunga na uimbaji wa kwaya. Wakati anakua, Vina alijulikana mtaani kwa kukariri nyimbo za wanamuziki mashuhuri nchini Tanzania kama vile Professor Jay, Afande Sele, Juma Nature, na Solo Thang. Wakati fulani, watu walikuwa wakimpa pesa ili awaimbie baadhi ya nyimbo zilizotamba wakati huo. Alianza kutamani kuwa mchanaji baada ya kusikiliza albamu ya "Machozi Jasho na Damu" ya Professor Jay.

Dizasta vina alianza rasmi kujishughulisha na masuala ya muziki mnamo mwaka wa 2007 kwa kushiriki katika mashindano mbalimbali ya kurap ikiwa ni pamoja na SM Straight Music Freestyle Battle mwaka wa 2010 mkoani Iringa. Mashindano kama haya yalimjengea msingi wa kuwa mwanamuziki na kumpa hamasa ya kujifunza zaidi kuhusu misingi ya utamaduni wa hip hop.

Mnamo mwaka wa 2011 alikutana na mtayarishaji wa muziki, Duke Touchez. Duke alimpa mwongozo wa jinsi ya kujiunga na Tamaduni Muzik ambayo kwa kipindi hicho ilikuwa inatafuta vipaji vipya kwa ajili ya "Tamaduni Foundation". Dizasta alishiriki shindano ya kuchana lililofanyika wakati wa tamasha la kuachia santuri tano kwa mpigo ("African Son" ya Stereo, "Sauti ya Jogoo" ya Nikki Mbishi, "Mzimu wa Shaaban Robert" ya Nash MC, "Underground Legendary" ya Duke Touchez na "Mathematrix" ya Songa na Ghetto Ambassador).[6] Baada ya shindano hilo alifanikiwa kujiunga rasmi na Tamaduni Muzik. Alianza kupata umaarufu mnamo mwaka wa 2012, alipotoa wimbo wake wa kwanza 'Harder'.[7]

Mwaka wa 2013, Dizasta alitoa wimbo ulioitwa "Tega sikio", kisha akatoa "Goli la ushindi", "Nyumba Ndogo" na "Sister". Dizasta alishirikishwa kwenye albamu ya "Underground Project" ya mtayarishaji wa muziki anayefahamika kwa jina la AK 47, kwenye wimbo uliokwenda kwa jina la "Heavyweight" alishirikiana na mwanamuziki wa kike, Tifa Flows. Mwaka huo huo alishirikishwa katika albamu ya "Upande wa pili wa sarafu" ya mtayarishaji wa muziki Abby Mp, kazi ya kilinge ya Duke Touchez, albamu ya "Kiutu Uzima" ya msanii Kadgo, Kandamseto ya "Slow Jams" ya mtayarishaji wa muziki - Innocent Mujwahuki, "Tamaduni Foundation" ya Ngwesa na "Representing Africa Popote" ya One the Incredible.

Dizasta akiwa anaendelea na masomo ya chuo kikuu alijifunza mambo madogo madogo ya kuwa mwanamuziki wa kujitegemea. Kufikia mwaka wa 2015, Vina alikuwa maarufu nchini Tanzania baada ya kutoa wimbo wa ‘Kijogoo’ na ‘Siku Nikifa’. Mwaka 2017 alitoa kandamseto yake ya kwanza iliyokwenda kwa jina la "The Wonderboy Mixtape".[8] Kandamseto hii ilivuta usikivu wa wadau wengi wa muziki na alianza kuzungumziwa kupitia media mbalimbali kama mmoja wa wasanii bora wa kizazi kipya na mtunzi mahiri wa nyimbo za masimulizi.[9] Mnamo 14 Februari 2018, Dizasta alipata mwaliko kwenye "Dakika 10 za Maangamizi" kipindi kidogo ndani ya kipindi cha Planet Bongo cha East Africa Radio. Iliripotiwa kuwa kipindi chake cha mitindo huru ni mojawapo ya kipindi bora zaidi kwenye mfululizo wa kipindi hicho.[10]

2018: Jesusta hariri

Desemba mwaka wa 2018, Dizasta Vina alitoa albamu yake ya kwanza iliyoitwa "Jesusta". Albamu hiyo yenye nyimbo 20 imeshirikisha wasanii wengine ikiwa ni pamoja na Nikki Mbishi, Shaolin Senetor, Bokonya, Kinya, Motra the Future, Boshoo na Jeff Mduma. Albamu ilivuta hisia za wapenzi wengi wa muziki wa hip hop kote nchini na ilijumuisha nyimbo maarufu kama: "The Lost One", "Nobody is Safe", " Kanisa"[11], na "Hatia". Wimbo wa "Kikaoni" ambao aliutayarisha mwenyewe uliingia katika chati za vituo kadhaa vya redio jijini Dar es Salaam na kote Tanzania.[12]

2020:The Verteller hariri

Makala kuu: The Verteller

"The Verteller" albamu ya pili ya Dizasta Vina ilitolewa tarehe 27 Desemba 2020 ilitolewa kupitia Panorama Authentik na utayarishaji wake ulishughulikiwa na Ringle Beatz (ambaye pia amesimama kama mtayarishaji mkuu), Cjmoker na Jcob.

Dizasta alirekodi albamu hii kati ya mwaka 2019 na 2020. The Verteller ina jumla ya nyimbo 20 kama mtangulizi wake na imeshirikisha wasanii wengine kutoka nchini Tanzania ikiwa ni pamoja na Tk Nendeze, Adam ShuleKongwe, Bokonya, Wakiafrika, Nasra Sayeed na Dash. Albamu ilipokelewa vyema na mashabiki na wapenzi wa muziki. Nyimbo kama "Ndoano", " The Confession of a Mad Man", "Wimbo usio bora", " Kesho" na "Muscular Feminist" zilimletea umaarufu zaidi wa kitaifa na ufuasi mkubwa wa mashabiki.[13]

Mzozo hariri

Mnamo Januari 2023 uliibuka mzozo kati ya Dizasta Vina na Rapcha. Mzozo ulianza kutokana na wimbo wa Rapcha "Story Nyingine", ambapo Rapcha aliwazungumzia wasanii kadhaa kwenye wimbo huu ikiwa ni pamoja na Babu Tale, Young Lunya na Dizasta Vina.[14] Januari 9, 2023, Dizasta alimjibu kwa kutoa wimbo unaoitwa "Best Friend". Mzozo wao uliendelea baada ya Januari 12, 2023, Rapcha kutoa wimbo wa "Nyuclear Story" ambao moja kwa moja ulimlenga dizasta vina. Siku nne mbele, Januari 17, 2023, Dizasta Vina alimjibu tena Rapcha kwa kutoa wimbo wa "Tribulation", Rapcha hakuja na jibu.[15]

Kutayarisha muziki hariri

 
Dizasta Vina akiwa katika studio za Panorama Authentik jijini Dar es Salaam, Tanzania— mnamo tarehe 17 Februari, 2018.

Miaka ya karibuni, Dizasta amekuwa akitayarisha muziki wake mwenyewe, hii ni baada ya kuamua kukaa chini na kuanza kusoma jinsi ya kutayarisha muziki na kufanya uhandisi wa sauti. Baadhi ya nyimbo zake mashuhuri alizotayarisha mwenyewe ni pamoja na "Fallen Angel" iliyotoka tarehe 23 Julai 2016, "Kanisa" iliyotoka 13 Novemba 2016 na "The Lost One" iliyotoka Aprili 2017.

Uwezo wake mkubwa kama mtayarishaji ulianza kuonekana kupitia mfululizo wa nyimbo zake kama vile "Hatia", "Nobody is Safe", "Hatia II", na "Hatia III" na "Kikaoni", kibao kilicho jizolea umaarufu mkubwa kwa wapenzi wa utamaduni wa handakini kutokana na kugusa maisha ya familia na ndoa. Katika albamu ya " The Verteller" alishiriki kutayarisha wimbo wa "Tatoo Ya Asili", "A Confession of a Mad Teacher","A Confession of a Mad Son", "Ndoano", "Maabara" na "Kifo.

Anakubali kuwa amepata utaalamu na mbinu nyingi zaidi za kutayarisha muziki kutokana na kufanya kazi na watayarishaji wengine wa muziki wa Kitanzania kama Duke Touchez, Ray Teknohama na Ringle Beatz. Dizasta anaamini kuwa na taaluma ya kutayarisha muziki wake mwenyewe kuna faida kubwa kwani kunafanya afikie hisia halisi za wimbo tofauti na pale anapotafuta na kujenga mahusiano ya kimuziki na mtayarishaji mwingine.

Dizasta Vina na Tamaduni Muzik hariri

Tamaduni ni lebo ambayo Dizasta Vina alifanya nayo kazi baada ya uwezo na uelewa wake kuhusu utamaduni wa hip hop kumvutia Duke Touchez ambaye alifanikisha Dizasta kujiunga na "Tamaduni Foundation" akiwa na wasanii kama One the Incredible, Nikki Mbishi, Boshoo na wengineo. Kupitia Tamaduni Muzik waliweza kubadilisha na kutimiza nguzo karibia zote za hip hop zinavyotaka. Maoni ya Dizasta Vina kuhusu Tamaduni Muzik ni kwamba ndio wao waliobadilisha mtazamo na mwelekeo mzima wa muziki wa hip hop ya Tanzania. Kupitia wao, tuliweza kuona kutolewa kwa albamu kwa sana hata kwa wasanii wachanga, kutoa kandamseto, kurudisha maonesho ya hip hop kukusanya wasanii “Kilingeni” huko Msasani Club.

Diskografia hariri

Hii ni orodha ya albamu za muziki alizotoa Dizasta Vina.

Na. Jina la albamu Mwaka Maelezo
1. THE WONDERBOY Mixtape 2017 Kandamseto ya kwanza kutoka kwa Dizasta Vina.
2. Jesusta 2018 Albamu rasmi ya kwanza kutoka kwa Dizasta Vina.
3. The Verteller 2020 Albamu ya pili kutoka kwa Dizasta Vina.

Viungo vya nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
  1. Frank Lachman (2024-03-25). "Dizasta Vina: The Legendary Tanzanian Hip Hop Artist who is redefining the genre with his rare and unique rhymes" (kwa en-US). Iliwekwa mnamo 2024-03-27. 
  2. "Dizasta Vina". Music In Africa (kwa Kiingereza). 2022-11-10. Iliwekwa mnamo 2023-01-19. 
  3. "Fid Q ataja Top 5 ya rapa wake bora Tanzania | East Africa Television". www.eatv.tv (kwa Kiingereza). 2023-11-29. Iliwekwa mnamo 2024-01-29. 
  4. "Dizasta Vina Biography, Music Career, Awards, Relationships and Net Worth ⚜ Latest music news online". mdundo.com (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-07-28. 
  5. "Micshariki Africa" (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-07-28. 
  6. Tamadunimuzik (2012-08-11). ":::::::::TAMADUNIMUZIK::::::::::: UZINDUZI WA SANTURI 5 KWA PAMOJA". Iliwekwa mnamo 2022-07-28. 
  7. "Dizasta Vina: Zawadi nyingine kwa wapenda HipHop Tanzania". JamiiForums (kwa en-US). Iliwekwa mnamo 2022-07-28. 
  8. Frank Lachman (2024-03-25). "Dizasta Vina: The Legendary Tanzanian Hip Hop Artist who is redefining the genre with his rare and unique rhymes" (kwa en-US). Iliwekwa mnamo 2024-03-27. 
  9. "Dizasta Vina anaweza akawa ndio best rapper Tanzania". JamiiForums (kwa en-US). Iliwekwa mnamo 2022-07-28. 
  10. Dakika 10 Za Maangamizi- Dizasta Vina | Planet Bongo I (kwa sw-TZ), iliwekwa mnamo 2022-07-28 
  11. "Micshariki Africa" (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-10-20. 
  12. "Audiomack | Free Music Sharing and Discovery". audiomack.com (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-07-28. 
  13. Simulizi na sauti SNS (2024-03-25). "More deadly than the male: Clara Cleitus Luvanga – A story of a baller from Njombe" (kwa en-US). Iliwekwa mnamo 2024-03-27. 
  14. "The beauty and ugliness of beefing to Bongo Flava showbiz". The Citizen (kwa Kiingereza). 2023-01-20. Iliwekwa mnamo 2024-04-02. 
  15. "Rapcha Amjibu Dizasta Vina Kwenye Nyu'clear Freestyle ⚜ Latest music news online". mdundo.com (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2024-04-02.