Kalenda ya Juliasi

Kalenda ya Juliasi ni kalenda iliyoanzishwa katika Dola la Roma kwa amri ya Julius Caesar mnamo mwaka 46 KK Ilichukua nafasi ya kalenda ya Kirumi iliyotangulia.

Kalenda ya Juliasi ilibadilishwa na kalenda ya Gregori kuanzia karne ya 16 BK lakini ilikuwa kalenda rasmi katika nchi mbalimbali kama Urusi hadi karne ya 20. Mpaka leo ni kalenda ya liturgia katika Kanisa la Kiorthodoksi.

Matengenezo ya mwaka 46 KK hariri

Juliasi Kaisari alikuwa mtawala wa Kirumi aliyeamua kubadilisha kalenda ya kale iliyokuwa ya aina ya kalenda ya mwezi. Majira yalikosa tarehe kamili katika kalenda hiyo, hali iliyosababisha matatizo ya kiutawala, hasa kwa sababu tarehe ya malipo ya kodi ilitakiwa kuwa baada ya mavuno, wakati wakulima walipokuwa na uwezo wa kulipa.

Hivyo Caesar alimwajiri mtaalamu Mmisri Sosigenes atunge kalenda mpya inayofuata mzunguko wa jua. Kalenda hiyo iliitwa kwa heshima yake Kalenda ya Juliasi. Ilikuwa na miezi 12 yenye siku 30 au 31 isipokuwa mmoja mfupi wenye siku 28 ambao ni mwezi wa Februari ili kukamilisha siku 365 za mzunguko wa kandokando ya jua. Vipindi hivyo viliendela kuitwa "mwezi/miezi" ingawa havikufuata tena mwendo wa mwezi wenyewe. Kwa sababu muda wa mwaka wa jua ulijulikana kuwa na siku 365 1/4, kila mwaka wa nne siku ya nyongeza iliingizwa kama siku ya 29 ya mwezi wa Februari.

Mwaka 46 KK wenyewe ulirefushwa kwa ajili ya sahihisho lile ukawa na siku 445 ambao Warumi waliukumbuka kama "mwaka uliochanganyikiwa".

Majina na hesabu ya miezi hariri

Sosigenes alitumia majina ya miezi ya kalenda ya kale yanayoendela kutumika hadi leo. Isipokuwa mwaka 44 KK baada ya kifo cha Caesar mwezi wa "Quintilis" ulipewa jina la marehemu ukaitwa "Julius" ndiyo Julai kwa Kiswahili. Mtawala mkubwa aliyefuata baada ya Julius Caesar alikuwa Augusto (anayehesabiwa kuwa Kaisari wa kwanza wa Kirumi) na mwezi wa Sextilis ulipewa jina kwa heshima yake: ni mwezi wa Agosti kwa Kiswahili. Hata watawala wengine walijaribu kupachika majina yao kwenye mwezi fulani lakini ni majina ya Kaisari Juliusi na Augusto pekee yaliyodumu.

Miezi ya Septemba hadi Desemba inatunza kumbukumbu ya kwamba ilikuwa miezi ya saba hadi kumi katika kalenda ya kale ya kirumi.

Jina la mwezi - Nambari ya Kilatini

Septemba - septem (7)

Oktoba - octo (8)

Novemba - novem (9)

Desemba - decem (10)

Lakini hapakuwa na mapatano kuhusu mwanzo wa mwaka ni mwezi gani. Maeneo mbalimbali yalitumia mwanzo tofauti. Ni tangu karne ya 13 BK tu kwamba 1 Januari ilianza kukubaliwa polepole kuwa mwanzo wa mwaka katika nchi za Ulaya.

Kasoro za Kalenda ya Juliasi hariri

Kalenda ya Juliasi ilikuwa na kasoro ambayo haikujulikana mwanzoni. Muda kamili wa mwaka wa jua si siku 365 1/4. Hivyo mwaka wa kalenda ya Juliasi ulipita muda kamili ya mwaka wa jua kwa dakika 11 na sekunde 14.

Hadi karne ya 14 BK tofauti hiyo ilikuwa imefikia tayari jumla ya siku 7. Hayo yalionekana hasa wakati wa Pasaka ambayo haikufuata tena utaratibu uliowekwa na Mtaguso wa kwanza wa Nisea.

Kwa sababu hiyo Mtaguso wa Trento wa Kanisa Katoliki uliamua kusahihisha kalenda. Ni Papa Gregori XIII aliyeita wataalamu waliofanya makadirio mapya.

Tangu mwaka 1582 kalenda ya Gregori ilipoanzishwa ikawa leo kalenda ya kimataifa.