Mtaguso wa Trento (uliofanyika kwa kwikwi kuanzia mwaka 1545 hadi 1563), unahesabiwa na Kanisa Katoliki kuwa mtaguso mkuu wa kumi na tisa.

Mtaguso ukifanyika katika kanisa kuu la Trento.

Miaka hiyo maaskofu wa Kanisa Katoliki walikutana Trento, Italia Kaskazini, wakajadiliana juu ya mafundisho na hali ya Kanisa, wakachukua hatua za kuimarisha imani na kuondoa matatizo.

Huo Mtaguso, ulioitishwa kizazi kimoja baada ya matengenezo ya Martin Luther, ulianza kabla ya vita vya Schmalkald (1546-1547) ukamalizika baada ya amani ya Augsburg (1555).

Mwishoni mwa kikao cha tatu ilionekana wazi kuwa umoja wa Kanisa la magharibi umekwisha. Haikuwezekana kufuta farakano lililotokea tayari.

Mtaguso huo, uliochukua muda mrefu kuliko yote ya historia, ulieneza urekebisho wa Kanisa na kuchukua msimamo kuhusu mafundisho ya Waprotestanti waliojitokeza katika hiyo karne ya 16.

Historia hariri

Utangulizi hariri

Mtu wa kwanza kulilia mtaguso ambao uamue kati yake na papa alikuwa Martin Luther (1517): huko Ujerumani ombi lake liliungwa mkono na wengi, pamoja na Kaisari Karolo V aliyeuona kuwa njia ya kurekebisha Kanisa lakini pia ya kujiimarisha kimamlaka. Ndiyo sababu kuu iliyomfanya Papa Klementi VII (1523-1534), aliyesimama upande wa Ufaransa, kukataa kabisa kuuitisha.

 
Mchoro wa Sebastiano Ricci, Papa Paulo III ana ono la Mtaguso wa Trento. 1687-1688, Piacenza, Museo Civico.

Wazo hilo lilipata nguvu tena chini ya mwandamizi wake, Papa Paulo III (1534-1549), ambaye mwaka 1536 aliitia kwanza Mantova halafu Vicenza maaskofu na maabati wote, pamoja na wafalme wadogo wengi wa Dola takatifu la Kiroma (Ujerumani).

Baada ya juhudi mbalimbali kushindikana, mwaka 1542 uamuzi ulifikiwa wa kuitisha mtaguso huko Trento kwa sababu ni mji wa Italia lakini ulikuwa ndani ya mipaka ya dola hilo. Hatimaye (19 Novemba 1544) Papa aliweza kutoa hati ya kuitisha mtaguso inayoitwa Laetare Jerusalem.

Hati hiyo iliupatia mtaguso kazi tatu: kuponya utengano katika mafundisho, kurekebisha Kanisa na kurudisha amani kati ya watawala, ili kujihami dhidi ya uvamizi wa Waturuki Waislamu.

Vikao hariri

Mtaguso ulifunguliwa rasmi tarehe 13 Desemba 1545 katika kanisa kuu la Mt. Vigilio.

 
Mtaguso wa Trento katika kanisa la Santa Maria Maggiore (Museo Diocesano Tridentino).

Mwanzoni mtaguso ulikuwa na maaskofu wachache, karibu wote kutoka Italia, ukatawaliwa na wajumbe wa Papa. Kati ya makardinali wapya (Contarini, Sadoleto, Carafa, Fisher na huyo Pole) wengi walipenda urekebisho.

Zilijadiliwa na kupitishwa hasa dogma dhidi ya mafundisho ya Waprotestanti, kama vile kuhusu utakaso na wokovu. Pamoja na kupitisha tafsiri rasmi ya Biblia katika Kilatini iliyo maarufu kwa jina la Vulgata, kati ya maamuzi muhimu zaidi upo ule wa kudai maaskofu waishi katika majimbo yao ili kufanya uchungaji uliowapasa.

Baada ya mtaguso kuhamishiwa Bologna, Papa Paulo III aliusimamisha mnamo Septemba 1549.

Papa Julius III (1550-1555) aliuitisha tena kuanzia tarehe 1 Mei 1551 na zikatolewa hati juu ya sakramenti za Ekaristi, Kitubio na Mpako wa wagonjwa.

Polepole waliohudhuria waliongozeka, wakiwemo Waprotestanti wengi pia, wakidai wanateolojia wao wawe na haki ya kupiga kura na hati zilizokwishatolewa zifutwe. Ndipo ilipoonekana wazi kwamba tofauti katika imani ni kubwa mno.

Majeshi ya Kiprotestanti yalipokaribia Trento, Papa alikubali kusimamisha tena mtaguso tarehe 28 Aprili 1552.

Sehemu ya mwisho ya mtaguso baada ya kuitishwa ilichelewa kuanza hadi tarehe 18 Januari 1562, tena ilikabili matatizo mengi, lakini iliokolewa na kutawaliwana askofu wa Milano Karolo Borromeo, mpwa wa Papa Pius IV (1559-1565) aliyemalizia haraka mtaguso wakiwemo wajumbe 255.

Katika sehemu hiyo yalitolewa mafundisho rasmi kuhusu Misa, Daraja takatifu na Ndoa, Toharani, sala kwa watakatifu, heshima kwa masalia na rehema.

Pia Kanisa la Roma lilikubaliwa kama mama na mwalimu wa makanisa yote. Maaskofu wote walitakiwa kuahidi utiifu kwa Papa, ambaye peke yake ana haki ya kuitisha mtaguso mkuu. Kwa msingi huo, mtaguso ulimuachia Papa kuthibitisha maamuzi yote, naye alifanya hivyo bila ya kujali upinzani wa maofisa wake huko Roma.

Hivyo, mwishoni, maamuzi mbalimbali yaliachwa mikononi mwa Papa na ofisi zake, yakachukuliwa miaka iliyofuata; kati yake, urekebisho wa Breviari na Misale, kwa kusawazisha liturujia za majimbo ya magharibi (isipokuwa chache, kama ile ya Jimbo la Milano na ya Jimbo la Lyon) kulingana na mapokeo ya Roma. Halafu ikatolewa Katekisimu ya Trento na Orodha ya vitabu vilivyokatazwa (Index librorum prohibitorum).

Tathmini hariri

Mtaguso wenyewe uliamua kila kikao kitoe hati moja ya kidogma ili kufafanua rasmi imani ya Kanisa na nyingine ya kisheria ili kufanikisha urekebisho.

Kwa kiasi kikubwa Mtaguso huo ulisababishwa na haja ya kuitikia Matengenezo ya Kiprotestanti, lakini haukuhukumu watu wala jumuia maalumu, ila mafundisho yao. Hata hivyo kwa kawaida haukueleza imani kwa upana wote, bali zilitetea mafundisho yaliyokanushwa na Waprotestanti, zikisisitiza zaidi tofauti zilizokuwepo.

a) Msingi wa imani ni Biblia pamoja na mapokeo ya Kanisa. b) Kanisa peke yake lina mamlaka ya kueleza maana ya Biblia; Mkristo asijisomee bila mwongozo wa Kanisa. c) toleo la Biblia linalofaa zaidi ni lile linalotolewa na Kanisa Katoliki katika lugha ya Kilatini (lililoitwa "Vulgata" - pamoja na vitabu vya "Deuterokanoni" vilivyotengwa na Luther). d) Juu ya kuhesabiwa haki (jinsi ya kupata wokovu) ni kwamba mwanadamu hakubaliwi kwa sababu ya matendo yake mema bali kwa neema ya Mungu, lakini lazima ashiriki katika kupokea na kutumia neema hiyo. e) Sakramenti ziko saba.

Kwa kuwa dogma zilizotangazwa zililenga hasa kupinga Uprotestanti kama uzushi katika mambo kadhaa, zilichangia mazingira ya kubishana yaliyofanya Ukatoliki uonekane kama kinyume kabisa cha Uprotestanti. Katika kufanya hivyo, mtaguso ulilingana na maandishi mengi ya Kilutheri yaliyosisitiza tofauti na Ukatoliki. Hali hiyo iliendelea hadi Mtaguso II wa Vatikano (1962-1965).

Mtaguso wa Trento uliagiza pia marekebisho ya kichungaji, ukihamasisha utangazaji bora zaidi wa Neno la Mungu kupitia uanzishaji wa seminari kwa malezi ya mapadri (wote wawe na elimu kwa kufuata masomo huko na kwa kufuata utaratibu wa kusoma Biblia kila siku) na kupitia hotuba za lazima katika Misa za Dominika na sikukuu nyingine. Maaskofu na maparoko walidaiwa kuishi katika majimbo na parokia zao.

Ili kushirikisha vizuri zaidi imani, mtaguso ulipongeza juhudi zilizoanza wakati huo za kuandika katekisimu, kama ile ya Petro Kanisi, ukaagiza itungwe moja kwa Kanisa lote pamoja na vitabu vipya vya liturujia.

Mtaguso ulifuta maovu mbalimbali (kampeni za kuuza vyeti vya rehema, malipo ya maaskofu kwa Papa ili awathibitishie cheo, askofu kuwa na majimbo zaidi ya moja, kama ilivyofanyika zamani kwa sababu ya mapato) pamoja na kuongeza mamlaka ya maaskofu (hao walipewa kazi ya kufanya ziara hata katika parokia na shughuli za kichungaji za wale ambao awali hawakuwa chini yao). Ulipanga zifanyike sinodi za kikanda na za kijimbo.

Kwa jumla Mtaguso wa Trento ulishindwa kuwavuta Waprotestanti warudi, lakini uliendeleza urekebisho wa Kanisa Katoliki. Maazimio yake makuu yalibaki muhimu mpaka karne ya 20. Katika nchi zilizobaki chini ya Roma, Kanisa lilipata nguvu tena kwa kuimarisha mafundisho ya kale pamoja na kuondoa kasoro mbalimbali.

Tanbihi hariri

Marejeo hariri

  • Bühren, Ralf van: Kunst und Kirche im 20. Jahrhundert. Die Rezeption des Zweiten Vatikanischen Konzils (Konziliengeschichte, Reihe B: Untersuchungen), Paderborn 2008, ISBN 978-3-506-76388-4
  • O'Malley, John W., in The Sensuous in the Counter-Reformation Church, Eds: Marcia B. Hall, Tracy E. Cooper, 2013, Cambridge University Press, ISBN 978-1-107-01323-0, google books

Marejeo mengine hariri

  • John W. O'Malley: Trent: What Happened at the Council, Cambridge (Massachusetts), The Belknap Press of Harvard University Press, 2013, ISBN 978-0-674-06697-7
  • Hubert Jedin: Entstehung und Tragweite des Trienter Dekrets über die Bilderverehrung, in: Tübinger Theologische Quartalschrift 116, 1935, pp. 143–88, 404–29
  • Hubert Jedin: Geschichte des Konzils von Trient, 4 vol., Freiburg im Breisgau 1949–1975 (A History of the Council of Trent, 2 vol., London 1957 and 1961)
  • Hubert Jedin: Konziliengeschichte, Freiburg im Breisgau 1959
  • Mullett, Michael A. "The Council of Trent and the Catholic Reformation", in his The Catholic Reformation (London: Routledge, 1999, ISBN 0-415-18915-2, pbk.), p. 29-68. N.B.: The author also mentions the Council elsewhere in his book.
  • Schroeder, H. J., ed. and trans. The Canons and Decrees of the Council of Trent: English Translation, trans. [and introduced] by H. J. Schroeder. Rockford, Ill.: TAN Books and Publishers, 1978. N.B.: "The original 1941 edition contained [both] the Latin text and the English translation. This edition contains only the English translation...."; comprises only the Council's dogmatic decrees, excluding the purely disciplinary ones.

Viungo vya nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
  Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mtaguso wa Trento kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.