Kroisos

(Elekezwa kutoka Croesus)

Kroisos (kwa Kigir. Κροῖσος, Kilat. Croesus) alikuwa mfalme wa Lydia aliyetawala kuanzia mwaka 585 KK hivi hadi aliposhindwa na mfalme wa Uajemi, Koreshi Mkuu, mnamo mwaka 547 KK.[1] Lydia ilikuwa nchi ya Ugiriki ya Kale kwenye maeneo ya magharibi ya Asia Ndogo yaani Uturuki ya leo.

Picha kwenye chungu cha kale inamwonesha Kroisos kwenye kuni atakapoendelea kuchomwa kufuatana na mapokeo ya Herodoti.

Kroisos alikuwa maarufu kwa utajiri wake mkubwa. Chanzo cha utajiri wake kilikuwa dhahabu iliyochimbwa katika milki yake pamoja na kodi ya miji ya biashara na malipo ya miji ya Kigiriki iliyoshindwa naye kwa vita. Waandishi Herodoti na Pausanias walitaja kwamba zawadi zake zilitunzwa kwenye hekalu la Delphi. [2] [3]

Mipaka ya Lydia chini ya Mfalme Kroisos
Sarafu ya dhahabu ya Kroisos, Lydia, mnamo 550 KK.

Croesus anasifiwa kwa kutoa sarafu za kwanza za dhahabu zilizosanifishwa kwa usafi sanifu na uzito maalumu kama pesa rasmi.[4] [5]

Katika tamaduni za Kigiriki na Kiajemi jina la Kroisos likawa kisawe cha mtu tajiri. Kwa lugha za Ulaya kama Kiingereza, semi kama vile "tajiri kama Croesus" au "tajiri kuliko Croesus" hutumiwa hadi leo kuonyesha utajiri mkubwa.

Wakati wa utawala wake milki ya Uajemi chini ya mfalme Koreshi II ilipanusha mipaka yake ndani ya Asia Ndogo na Kroisos aliona hatari kwa utawala wake. Hivyo aliamua kutumia utajiri wake kuajiri jeshi la mamluki na kushambulia Waajemi. Kabla ya kuvuka mto Hadys uliokuwa mpaka wa milki, alituma wajumbe kwa Pythia wa Delfi aliyekuwa mwaguzi mashuhuri katika Ugiriki ya Kale na kutafuta utabiri kuhusu vita aliyopanga. Jibu la Pythia lilikuwa "Ukivuka mto Hadys utaharibu milki kubwa", alilopokea kama utabiri wa ushindi wake. Lakini alishindwa katika vita na Koreshi II na milki iliyoharibika ilikuwa milki yake mwenyewe.[6]

Hatima ya Croesus baada ya ushindi wa Waajemi dhidi ya Lydia haijulikani: Herodoti pamoja na waandishi wengine waliandika kwamba ama Kroisos alijaribu kujiua, au kwamba alihukumiwa na kuchomwa na Waajemi akiwa hai. Wengine waliandika kwamba aliendelea kuishi na kuwa mshauri wa mshindi Koreshi. Xenofoni alidai pia kwamba Koreshi alimweka Kroisos kama mshauri wake, ilhali mwandishi mwingine wa kale aliandika kwamba Koreshi alimteua kuwa gavana wa eneo huko Umedi. [7]

Baada ya kumshinda Kroisos, Koreshi aliiga matumizi ya dhahabu kama sarafu kuu ya ufalme wa Uajemi. [8]

Marejeo hariri

  1. Wallace, Robert W. (2016). "Redating Croesus: Herodotean Chronologies, and the Dates of the Earliest Coinages". The Journal of Hellenic Studies 136: 168–181. JSTOR 44157500. doi:10.1017/S0075426916000124. Retrieved 14 November 2021.  Unknown parameter |s2cid= ignored (help)
  2. Among them a lion of gold, which had tumbled from its perch upon a stack of ingots when the temple at Delphi burned but was preserved and displayed in the Treasury of the Corinthians, where Pausanias saw it (Pausanias 10.5.13). The temple burned in the archonship of Erxicleides, 548–47 BC.
  3. Evans, J. A. S. (1978). "What Happened to Croesus?". The Classical Journal 74 (1): 34–40. JSTOR 3296933. Retrieved 11 May 2022. 
  4. Herodotus, I, p. 80
  5. An Encyclopedia of World History, (Houghton Mifflin Company Boston, 1952), chap. II. "Ancient History", p. 37
  6. Poulsen, Frederik (1920): Delphi. London 1920, uk. 27; online hapa
  7. Kevin Leloux, La Lydie d'Alyatte et Crésus: Un royaume à la croisée des cités grecques et des monarchies orientales. Recherches sur son organisation interne et sa politique extérieure, University of Liège: https://orbi.uliege.be/bitstream/2268/220928/2/The%cc%80se%20entie%cc%80re%20vol%20II.pdf Archived 2022-10-09 at ghostarchive.org [Error: unknown archive URL]
  8. Mallowan, Max (1968). Gershevitch, Ilya, ed. The Cambridge History of Iran (in English). Cambridge University Press. pp. 392–419. ISBN 978-0-521-20091-2. 

Viungo vya nje hariri