Mein Kampf (tamka main kampf; maana ya Kijerumani: Mapambano au mapigano yangu) ni kitabu kilichoandikwa na Adolf Hitler kabla ya kushika utawala wa Ujerumani. Alieleza humo mawazo yake juu ya siasa, historia na dunia kwa jumla.

Toleo la Kifaransa la "Mein Kampf".

Hitler aliandika kitabu cha kwanza cha Mein Kampf gerezani alipofungwa baada ya jaribio la kupindua serikali mwaka 1923. Alipoondoka aliongeza kitabu cha pili. Tangu mwaka 1930 sehemu zote mbili zilichapishwa pamoja kama kitabu kimoja.

Katika kitabu chake Hitler alieleza kwa upana mawazo yake mbalimbali.

Yaliyomo yalikuwa

  1. Alidai maungano ya Austria na Ujerumani
  2. Alieleza kwa upana uadui wake dhidi ya Wayahudi akidai waliendesha ubepari lakini pia kinyume chake yaani ukomunisti kwa shabaha ya kutawala dunia. Hapo ulikuwa msingi wa siasa yake iliyochocheza uadui dhidi ya kundi dogo alilodai kuwa sababu ya maovu yote.
  3. litangaza ujamaa au usoshalisti wa kitaifa badala ya ujamaa wa kimataifa akilenga tabaka kubwa la wafanyakazi wa viwandani;
  4. Alieleza utawala wa ukomunisti katika Urusi ulipaswa kuondolewa kwa vita
  5. Alidai ardhi mashariki mwa Ulaya ilihitajika kwa ajili ya Wajerumani ambao aliwaona walikosa nafasi waliostahili,
  6. Alikashifu demokrasia kama muundo wa serikali na dola akidai ya kwamba utamaduni asilia wa Wajerumani ni kuwa na kiongozi mwenye mamlaka yote

Kitabu kilitangazwa kama "biblia" ya harakati ya Manazi. Baada ya Hitler kuwa kiongozi wa serikali na dikteta kilichapishwa na kugawiwa na vyombo vya serikali; bwana na bibi arusi wote walipewa nakala. Kwa jumla kilitolewa zaidi ya mara milioni kumi.

Baada ya mwisho wa utawala wake mwaka 1945 kitabu kilipigwa marufuku katika Ujerumani hadi leo. Mtu anaruhusiwa kuwa nacho lakini hakuna ruhusa kukichapisha upya.