Nicolas-Louis de Lacaille

Nicolas-Louis de Lacaille (tamka nikola lu-i de lakaiy, Rumigny, departement Ardennes, 15 Machi 1713 - Paris, 21 Machi 1762) alikuwa mwanaastronomia wa Ufaransa aliyetunga makundinyota 14 kati ya makundinyota 88 ya kisasa, zote kwenye Nusutufe ya kusini ya Dunia.

Picha ya Lacaille.

Lacaille alisoma theolojia Katoliki lakini baadaye alikazia elimu ya hisabati na astronomia. Mwaka 1746 alikuwa profesa wa hisabati na hapo alishughulika masahihisho ya orodha za nyota.

Mwaka 1750 alisafiri hadi Afrika Kusini na hapo alikaa miaka minne kwenye Rasi ya Tumaini Jema alitaka kutazama hasa Mwezi na sayari za Zuhura na Mirihi. Alipima pia nyota nyingi za anga ya kusini ambazo hazikueleweka kwa wanaastronomia wa Ulaya na hapo aliorodhesha nyota karibu 10,000.

Alipanga majina ya Bayer kwa kundinyota ya Argo na kuigawa baadaye kwa makundinyota tatu mpya za Shetri, Mkuku na Tanga.