Elimu kwa maana pana ni tendo au uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile wa mtu binafsi. Katika dhana ya kiufundi, elimu ni njia ambayo hutumiwa makusudi na jamii kupitisha maarifa, ujuzi na maadili kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine.

Darasa la chekechea nchini Afghanistan.
Darasa la shule ya msingi Meksiko.
Darasa la chuoni New York City.
Mwalimu akifundisha shule ya msingi

Walimu katika taasisi za elimu huratibisha elimu ya wanafunzi wao kupitia masomo kama vile ya kuandika, kusoma, kuhesabu (hisabati), sayansi na historia. Mbinu hii wakati mwingine huitwa masomo haswa tunaporejelea somo la aina fulani, kwa kawaida mbinu hii hutumiwa na maprofesa katika taasisi za masomo ya juu.

Kuna elimu maalumu kwa wale wanaohitaji ujuzi wa kitaaluma, kama vile wanaohitaji kuwa marubani. Juu ya hayo, kuna nafasi nyingi za elimu katika viwango vingine visivyo rasmi kama vile majumba ya ukumbusho, maktaba pamoja na mtandao na tajriba za maisha.

Wanachuo katika maabara, Saint Petersburg State Polytechnical University, Urusi

Haki ya kusoma imeweza kuelezwa kuwa haki ya msingi ya binadamu katika kifungu cha pili cha itifaki ya kwanza ya maagano ya haki za binadamu barani Ulaya kuanzia mwaka wa 1952 ambapo wanachama wote wanashurutishwa kuhakikisha elimu kwa wote. Katika kiwango cha kimataifa, Mapatano ya Umoja wa Mataifa ya haki za kiuchumi, za kijamii na za kiutamaduni katika mwaka wa 1966 yanahakikisha haki hii katika kifungu cha 13.

Mifumo ya elimu rasmi

Elimu ni dhana inayorejelea namna ambayo wanafunzi wanaweza kujifunza kitu:

  • Mwongozo hurejelea urahisishaji wa somo na hulenga kutambua shabaha zilizobuniwa na mwalimu au mbinu zingine za kufunza.
  • Kufunza hurejelea matendo halisi ya mwalimu yanayonuia kupasha elimu kwa wanafunzi.
  • Kujifunza hurejelea masomo yenye mtazamo unaolenga kuwapa wanafunzi elimu, ujuzi na uwezo unaoweza kutumika punde tu wakamilishapo kipindi cha masomo.

Elimu ya msingi

 
Shule ya msingi ya wazi. Mwalimu (kuhani) na darasa nje ya jiji la Bukarest, mwaka 1842.

Masomo ya msingi huchukua kati ya miaka 5-7 ya kwanza ya elimu rasmi. Kwa jumla elimu ya juu hujumulisha miaka 6-8 ya masomo kuanzia mwaka wa tano au sita, lakini hutofautiana baina na kati ya nchi. Asilimia 70 ya watoto waliotimu umri wa kujiunga na shule hujiandikisha katika masomo ya msingi kote ulimwenguni na viwango hivi vinaongezeka.[1] Chini ya Elimu kwa mipango yote inaendeshwa na UNESCO, nchi nyingi wana nia ya kufanikisha zima uandikishaji katika elimu ya msingi ifikapo mwaka 2015, na katika nchi nyingi, ni lazima kwa watoto kupata elimu ya msingi.Chini ya mpango wa elimu kwa wote ulioanzishwa na Shirika la Elimu, Sayansi na utamaduni la Umoja Wa Mataifa (UNESCO), nchi nyingi zimejitolea.

Elimu ya sekondari (shule za upili)

 
Wasichana katika shule ya sekondari huko Iraq.

Katika mifumo ya kisasa ya elimu ulimwenguni, elimu ya shule za upili au sekondari huchukua kipindi cha pili cha elimu rasmi ambayo hutokea wakati wa ujana wa wanafunzi. Mfumo huu hutofautian na masomo ya msingi ambayo ni ya lazima, ni ya jumla na yanayofanana.

Yale ya shule za upili ni teule na ya hiari. Shule hizi hujulikana kama sekondari, shule za upili, shule za kati, vyuo au shule za ujuzi wa kitaalamu kulingana na kipindi au mfumo unaofuatwa. Maana ya dhana hizi hutofautiana kutoka mfumo mmoja hadi mwingine. Mpaka kamili kati ya elimu ya msingi na ya upili hutofautiana kutoka nchi moja hadi nyingine. Tofauti hizi zipo hata katika nchi lakini kwa kijumla hutokea kati ya mwaka wa saba na wa kumi wa kusoma.

Elimu ya sekondari hutokea katika umri wa ujana. Nchini Marekani na Kanada elimu ya msingi na sekondari kwa pamoja hurejelewa kama elimu ya K-12 na katika nchini ya Nyuzilandi, elimu hii hurejelewa kama elimu ya miaka 1-13. Azma ya elimu ya sekondari ni kutoa maarifa ya kawaida, kutayarisha wanafunzi kwa elimu ya juu au kuwafunza watu kazi moja kwa moja.

Elimu ya sekondari iliibuka nchini Marekani mwaka wa 1910 na ilisababishwa na kuwepo kwa biashara kubwa na maendeleo ya kiteknolojia viwandani. Ili kuafikia mahitaji ya kazi, shule za upili zilijengwa na mtaala uliolenga maarifa ya kazi za ofisi na za sulubu ukazinduliwa. Hii ilibainika kuwa njia ya manufaa kwa mwajiri kwani uimarishaji wa huduma za kibinadamu uliwafanya waajiriwa kuwa madhubuti kazini na kushusha gharama kwa waajiri huku waajiriwa wakinufaika na mishahara minono ikilinganishwa na waliokuwa na elimu ya msingi pekee.

Barani Ulaya, shule za sarufi au akademia zilikuwepo hata katika miaka ya 1500. Shule za umma au zile za kulipa karo au hata shule za ufadhili na wakfu zina historia ndefu zaidi.

Tunapaswa kujitahidi katika kuhamasisha elimu ya sekondari kwani huwezesha kufikia chuo kikuu.

Elimu ya juu

 
Chuo Kikuu cha Cambridge ni taasisi ya elimu ya juu.

Elimu ya juu, yaani ile ya baada ya shule ya upili au elimu ya awamu ya tatu, si ya lazima. Elimu hii kwa kawaida hujumulisha viwango vya shahada pamoja na elimu ya ujuzi wa kitaalamu.

Kwa jumla elimu ya juu hutolewa na vyuo na vyuo vikuu na huambatana na kutolewa kwa vyeti, stashahada za diploma na shahada za digrii kitaaluma.

Masomo ya juu hujumuisha elimu, utafiti na huduma za jamii na katika uwanja wa elimu, hujumulisha viwango vya shahada ya kwanza na nyingine za juu. Elimu ya juu aghalabu huhusu kufuzu katika kiwango cha shahada ya kwanza, ya uzamili na ya uzamifu.

Idadi kubwa ya watu katika nchi zilizoendelea (hadi kufikia asilimia 50) wameweza kupata elimu ya juu wakati fulani maishani mwao. Kwa hiyo, elimu ya juu ni muhimu kwa uchumi wa taifa, ni kiwanda cha pekee ambacho huzalisha wafanyakazi walioelimika.

Katika nchi maskini serikali zinatakiwa kuongeza mikopo kwa wanafunzi wa vyuoni ili waweze kupata elimu hiyo na kusonga mbele, kwa kuwa elimu ni ufunguo wa maisha.

Elimu ya watu wazima

Elimu ya ngumbaru au ya watu wazima imekuwa kawaida katika nchi nyingi. Elimu hii huchukua maumbo mengi yakiwemo elimu rasmi darasani, elimu ya binafsi na masomo ya mtandao. Idadi fulani ya kozi za kazi maalum kama vile elimu ya mifugo, masuala ya madawa, uwekezaji, uhasibu na kozi nyinginezo kwa sasa hupatikana mtandaoni.

Elimu mbadala

Elimu mbadala, ambayo pia hujulikana kama elimu isiyo rasmi, ni dhana yenye maana pana na inayoweza kutumiwa kurejelea aina zote za elimu zilizo nje ya elimu ya kawaida (kwa watu wote na viwango vyote vya elimu).

Hujumuisha si tu mitindo ya elimu inayokusudiwa wanafunzi wenye mahitaji ya pekee lakini pia mitindo inayolenga hadhira ya jumla na kutumia mitindo na falsafa badala ya elimu.

Elimu mbadala mara nyingi huwa matokeo ya mabadiliko katika elimu yaliyotokea katika misingi mbalimbali ya falsafa ambayo kwa kawaida ni tofauti na elimu ya jadi ya lazima. Mabadiliko mengine yana misingi ya kisasa, kiutafiti au kifalsafa, ilhali mengine ni miungano isiyo rasmi kati ya walimu na wanafunzi wasioridhika na masuala fulani ya elimu hiyo ya jadi.

Elimu mbadala hii ambayo ni pamoja na shule za tabia, shule badala, shule zinazojitegemea na masomo ya nyumbani hutofautiana pakubwa, lakini zote hutilia maanani umuhimu wa idadi ndogo ya wanafunzi darasani na mahusiano ya karibu kati ya wanafunzi na walimu. Vilevile husababisha hali ya umoja.

Elimu ya asili

Kuongezwa kwa ruwaza za elimu ya asili (mbinu na maudhui yake) ndani ya elimu badala katika eneo la mfumo wa elimu rasmi na elimu isiyo rasmi kumewakilisha kipengele muhimu kilichochangia ufanisi wa mfumo wa elimu asili kwa wanajamii asili walioamua kufuata njia hii; hii ikiwa ni pamoja na wanafunzi na walimu.

Kuingizwa kwa mbinu za asili kama vile kujua, kusoma, kuelekeza, kufunza na kusoma kama njia nzuri ya kuhakikisha kuwa wanafunzi/wanagenzi na walimu/waelekezi wanaweza kufaidika kutokana na elimu kwa njia ya kiasili iliyokuza, kutumia na kuendeleaza uhamasishaji wa tamaduni za kiasili.[2]

Kwa wanafunzi au wagenzi na walimu au waelekezi, kuwekwa pamoja kwa mbinu hizi mara nyingi huongeza fanaka, matarajio na matokeo ya elimu. Hili huafikiwa kwa kutoa elimu inayooana na taswira zao za asili, mazoea na mitiazamo yao ya ulimwengu. Kwa wanafunzi na walimu wasio wa asili, elimu ya aina hii ina athari ya kuongeza ufahamu wa tamaduni zao za kibinafsi na mazoea ya jumla ya umma na watu wanaowazunguka, hivyo basi kukuza heshima na kuthamini tamaduni za wanajamii hizo.

Katika elimu na mafunzo, kujumuishwa kwa maarifa ya kiasili, tamaduni, maono, mitazamo na dhana katika mitaala, vifaa vya kuelekeza na vitabu vya kozi vina athari kubwa kama ile ya kujumuisha mbinu za asili katika elimu ambayo hunufaisha walimu na wanafunzi katika usambamba wa masomo, kufaulu na matokeo ya masomo hayo. Ambayo hunufaisha walimu na wanafunzi katika usambamba wa masomo, kufaulu na matokeo ya masomo hayo. Walimu na wanafunzi wa kisasa wana heshima, hamasa na maridhio kwa jamii na watu wa kienyeji kutokana na elimu husishi wanayopata.[3]

Mfano mkuu unaoonyesha mbinu na maudhui ya asili yanaweza kukuza matokeo yaliyotajwa hapo juu undhihirika katika elimu ya juu nchini Kanada. Kwa sababu ya sheria fulani, dhamira ya kuongeza mafanikio kwa wanafunzi wa elimu asili na kukuza maadili ya jamii ya kitamanduni, kuingizwa kwa mbinu na maudhui ya asili katika elimu huonwa kuwa jukumu na wajibu wa serikali na taasisi za elimu zenye mamlaka.[4]

Mchakato

Mitaala

Somo la taaluma ni tawi la elimu ambalo hufunzwa kirasmi katika vyuo vikuu ama kupitia njia zingine kama hizo. Kwa kawaida, kila somo huwa na masomo mengine ama matawi na mipaka ya kuyabainisha mara nyingi huwa si dhahiri na na mara nyingine husababisha utata. Mifano ya masomo ya kitaaluma yenye upana ni kama vile sayansi asilia, hesabu, sayansi ya komputa, sayansi za jamii, sayansi za binadamu na sayansi za matumizi.[5]

Mitindo ya kujifunza

Kuna utafiti uliofanywa kuhusu mitindo ya kusoma katika miongo miwili iliyopita. Dunn na Dunn [6] walilenga kutambua vichangamshi husishi vinavyofanya masomo yavutie na namna ya kutawala mazingira ya shule. Baadaye Joseph RenzulLi [7] alipendekeza mikAkati tofautitofauti ya kufunza. Howard Gardner[8] alitambua talanta ama vipaji vya mtu binafsi katika nadharia zake za akili nyingi. Kwa misingi ya kazi za C. G. Jung “Kielezi Aina cha Myers Briggs” na “kitenga tabia cha Keisresy” [9]vililenga kuelewa jinsi nafsi za watu huathiri uhusiano wa mtu binafsi na zinavyoathiri maelewano ya watu katika mazingira ya kujifunza. Kazi za David Kolib na Anthony Gregorc “jinsi ya kusawiri”[10] ” hufuata mfano kama huu lakini uliorahisishwa.

Kwa wakati huu, kugawika kwa elimu katika mitindo tofautitofauti hukubalika na wengi. Huenda ikawa kuwa mitindo[11] ya kujifunza ndiyo ya kawaida:[12]

  • Kuona: Masomo yenye misingi ya kutazama kwa makini na kuona kile kinachosomwa.
  • Kusikiza: Kusoma kwa misingi ya kusikiliza maelezo/habari.
  • Masomo husishi: Kusoma kwa misingi ya kutumia mikono na vitendo husishi.

Imedaiwa kuwa kulingana na mtindo wa kujifunza unaopendelewa, mbinu tofautitofauti za kufunza huwa na matokeo ya viwango tofauti.[13] Umuhimu wa nadharia hii ni kuwa kunakofaa, inapaswa kutumia mbinu mbalimbali za kufunza zinazojumulisha mitindo yote mitatu ya kufunza ili wanafunzi tofautitofauti wapate fursa ya kujifunza kwa njia inayowafaa.[14] Guy Claxton ametilia shaka mitindo ya kujifunza kama vile VAK kwani kwa kiasi fulani mitindo hii ina mazoea ya kupachika watoto majina hivyo basi kuwazuia kujifunza.[15]

Kujifunza

Kujifunza ni kutaka kujua juu ya jambo fulani ambalo hukulijua kabla. Hata jambo zuri kuhusu kujifunza ni kwamba hakuna mtu yeyote mwenye uwezo wa kukiweka mbali nawe kitu hicho ambacho umejifunza.

Walimu wanapaswa kuelewa somo vilivyo ili kuwasilisha umuhimu wake kwa wanafunzi. Shabaha hapa ni kuunda misingi ya ujuzi kamili ambayo wanafunzi wanaweza kutumia kujijenga zaidi kwani wamewekwa wazi kwa matukio mbalimbali ya maisha. Walimu wazuri huweza kutafsiri habari kama hukadiria vizuri, hutumia mazoea na hekima hadi kwa elimu husika ambayo mwanafunzi anaweza kuelewa, kuhifadhi na kupititishia wengine.

Utafiti kutoka Marekani unatoa maoni kuwa ubora wa walimu ndio kigezo kinachoathiri mafanikio ya wanafunzi, na kuwa nchi zinazopata alama za juu katika mtihani au majaribio ya kimataifa zimeweka sera chungu nzima zinazohakikisha kuwa walimu wanaoajiriwa ndio bora. [16]

Teknolojia

 
Tarakilishi mpakato zikitolewa kwa watoto wa Haiti.

Teknolojia ni kigezo muhimu katika elimu. Tarakilishi na simu za rununu zinatumiwa katika nchi zilizoendelea kuimarisha elimu iliyothibitishwa na kukuza njia mpya za elimu kama vile elimu ya mtandao (masomo ya mbali). Wanafunzi hupata fursa ya kuchagua wanachotaka kusoma.

Kuenea kwa tarakilishi pia kunamaanisha kuongezeka kwa programu za kompyuta na kuongeza habari mtandaoni. Teknolojia hutoa vifaa muhimu vinavohitaji ujuzi mpya na uelewa wa wanafunzi zikiwemo njia nyingi za mawasiliano, na huleta njia mpya za kuhusisha wanafunzi kama vile mazingira ya kujifunza.

Teknolojia inatumiwa si tu katika wajibu wa kutawala katika elimu bali pia katika kuwaelekeza wanafunzi. Matumizi ya teknolojia kama vile virusha maandishi (power point) na ubao mweupe hutumiwa kunasa akili za wanafunzi darasani. Teknolojia vilevile hutumiwa kuwatahini wanafunzi. Mfano mzuri ni mfumo wa kuvutia hadhira (ARS),ambao huruhusu majibu ya mitihani moja kwa moja pamoja na majadiliano darasani.

Teknolojia pia imekuwa mojawapo wa maktaba katika elimu ambamo vitabu, ripoti za utafiti, tansifu n.k. huchapishwa. Tovuti zinazochapishwa vitabu, ripoti na tansifu zimekuwa za manufaa kwa wasomi. Zinawapa uwezo wa kupata vitabu maalum kwa ujumbe fulani tofauti na maktaba za kizama ambazo humlazimu mtu kusoma kwa urefu na upana kupata ule ujumbe. Tofuati hizi hufuata mpangilio, nyingine zikiruhusu watumizi kupakua vitabu bila malipo, nyingine zina malipo ya muda, ilhali nyingine hulazimu mtu kununua kile kitabu anachokihitaji.[17]

Teknolojia za habari na mawasiliano (ICT) ni "seti ya vifaa na rasilimali mbalimbali zinazotumiwa kuwasiliana, kuunda, kueneza na kuongoza habari."[18] Teknolojia hizi ni pamoja na kompyuta, mtandao, teknolojia za kusambaza habari (redio na televisheni) na simu (kuongea na pia kwa ujumbe wa maandishi). Kuna mvuto unaoongezeka kuhusu namna tarakilishi na mtandao vinavyoweza kuimarisha elimu katika viwango vyote, yaani mseto wa elimu rasmi na ile isiyo rasmi.[19]

Teknolojia za habari na mawasiliano za awali, kama vile redio na televisheni, zimetumiwa kwa zaidi ya miaka 40 kwa elimu wazi na ile ya mbali, hata hivyo kupiga chapa ndiyo njia nafuu zaidi, inapatikana kwa urahisi, na hivyo basi ni mbinu iliyotawala katika nchi zilizoendelea na zile zinazoendelea.[20]

Matumizi ya tarakilishi na mtandao (ikiwa vinatumika) bado ni changa katika nchi zinazoendelea, na hii ni kwa sababu miundo msingi ni michache na ghali. Kwa kawaida teknolojia kadhaa hutumiwa kwa pamoja bali si mbinu pekee ya kupokelewa. Kwa mfano, Kothmel Community Radio Internet hutumia matangazo ya redio na kompyuta pamoja na teknolojia ya mtandao, na hivyo hurahisisha kugawa habari na kutoa nafasi za elimu katika kijiji fulani Sri Lanka.[21]

Chuo Kikuu cha Uingereza (UKOU) kilichoanzishwa mwaka wa 1969 kama taasisi ya elimu ya kwanza ulimwenguni kujitolea kutoa elimu ya wazi na ya mbali, bado hutegemea vifaa vilivyopigwa chapa na kuongezea redio, runinga na kompyuta.[22] Vivyo hivyo, Chuo Kikuu cha Indira Gandhi nchini India huweka pamoja matumizi ya chapa, sauti zilizorekodiwa, video, redio, televisheni na teknolojia ya vielezo vya kusikiza mkutano.[23]

Dhana ya “masomo yanayosaidiwa na kompyuta” (CAL) limetumiwa kwa wingi kuelezea teknolojia katika masomo.

Nadharia ya elimu

Nadharia ya elimu ni nadharia ya azma, matumizi na ufafanuzi wa elimu na kusoma. Historia yake inatokana na wataalamu wa elimu kutoka Ugiriki kuanzia karne ya 18. Katika karne ya 20 mbinu za kusoma zimetumia nadharia katika kufunza, kutathmini na katika sheria za elimu ambazo hupatikana katika vitengo mbalimbali kama ifuatavyo:

Uchumi

Sababu zimetolewa kuwa kiasi cha juu cha elimu ni muhimu kwa nchi ili kuwezesha ukuaji haraka wa uchumi.[24] Uchunguzi unaotegemea nadharia huunga mkono nadharia za kutabiri kuwa nchi maskini zinapaswa kukua haraka kuliko nchi tajiri kwani nchi hizi zinaweza kutumia teknolojia mpya kabisa ambayo imeshajaribiwa na nchi tajiri.

Hata hivyo, kuhamisha teknolojia kunahitaji viongozi wenye maarifa na wahandisi wenye uwezo wa kutumia mashine mpya ama mazoezi ya uzalishaji yaliyokopwa ili kuziba mpaka kwa miigo. Hivyo basi, uwezo wa nchi wa kujifunza kutoka kwa nchi kiongozi ni jukumu la wafanyakazi wa nchi hiyo.[25]

Utafiti wa hivi karibuni wa vitambulishi vya kujumuisha ukuaji wa kiuchumi umesisitiza umuhimu wa vyuo asili vya uchumi[26] na majukumu ya ujuzi tambuzi.[27]

Katika kiwango cha mtu binafsi, kuna maandishi yenye uhusiano na kazi ya Jacob Mincer, [28] ya jinsi mapato yanahusiana na elimu na rasilimali ya mtu binafsi. Kazi hii imetia motisha idadi kubwa ya utafiti lakini pia inaelekea kuleta mabishano kwa kiasi fulani. Ubishi mkubwa unahusu jinsi ya kufasiri matokeo ya kusoma.[29]

Wataalamu wa uchumi Samwel Bowels na Herbert Ginits walitoa maoni kwamba kulikuwa na ubishi asili katika elimu nchini Marekani kati ya shabaha ya demokrasia shirikishi yenye usawa na faida ya mapato ya kibepari yaliyodokeza hali ya kutokuwa na usawa.[30]

Historia ya elimu

 
Mchoro wa Chuo Kikuu cha Bologna, Italia.

Historia ya elimu ilianza miaka mingi iliyopita, kwa kuwa elimu kama sayansi haiwezi kutengwa na utamaduni wowote wa elimu iliyokuwepo awali. Wakubwa waliwafunza wadogo wao juu ya jamii kwa kutumia maarifa na ujuzi waliohitaji kufahamu na mwishowe kupitisha.

Mabadiliko ya utamaduni na binadamu kama spishi yalitegemea mazoea ya kupitisha elimu. Katika jamii ambazo hazikujua kusoma, hili liliafikiwa kupitia mdomo na kuiga. Kusimuliana hadithi kuliendelezwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Lugha ya mazungumzo iliendelea na kuwa ishara na herufi. Kina na upana wa elimu au maarifa ulioweza kuhifadhiwa na kupitishwa uliongezeka zaidi na zaidi. Wakati ambapo tamaduni zilianza kupanua elimu zaidi ya ujuzi wa kawaida wa mawasiliano, biashara, ukusanyaji chakula, tunu na desturi za kidini na kadhalika, mwishowe elimu rasmi na masomo vilifuatia. Kisomo kwa maana hii kilikuwa kimeshaanza nchini Misri kati ya 3000 na 500 KK.

Siku hizi aina fulani ya elimu ni jambo la lazima kwa watu wote katika nchi nyingi. Kwa sababu ya ongezeko la watu na kuenea kwa elimu ya lazima, Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) limepiga hesabu ya kwamba miaka 30 ijayo, watu wengi zaidi ulimwenguni watapata elimu rasmi katika historia ya binadamu.[31]

Falsafa ya elimu

 
Kitabu cha John Locke "Baadhi ya Mawazo Kuhusu Elimu" kiliandikwa mwaka 1693 na bado huonyesha vipaumbele vya elimu ya jadi katika Nchi za Magharibi.

Falsafa ya elimu ni utafiti wa kifalsafa juu ya kusudi, utaratibu na ubora wa elimu kwa kuchunguza ufafanuzi, malengo na maana ya elimu kwa jumla au ya mtazamo mmojawapo juu yake.

Falsafa ya elimu kwa kawaida huonwa kama tawi la falsafa na la elimu.

Falsafa ya elimu mara nyingi hubaki ndani ya falsafa na elimu, ilhali ni falsafa matumizi, iliyotokana na nyanja za zamani za falsafa (ontolojia, maadili, epistemolojia) na njia (kisia, taswira na tafiti), mbinu na mtaala, nadharia, kwa kutaja tu chache.

Saikolojia ya elimu

 
Utafiti nchini Marekani ulionyesha kwamba watoto wa familia zenye kipato cha chini, kwa kuhudhuria madarasa madogo miaka 3 au zaidi ya utotoni, walifaulu zaidi kuhitimu masomo ya juu baadaye. [32]

Saikolojia ya elimu ni uchunguzi wa jinsi watu hujifunza katika mandhari ya elimu, ufaafu wa maingiliano ya elimu, saikolojia ya kufunza na saikolojia jamii za shule. Ingawa maneno “saikolojia ya kielimu” na “saikolojia ya shule“ mara nyingi hutumiwa kwa kubadilishana, watafiti na wananadharia wanaweza kutambuliwa kama wanasaikolojia wa elimu, ilhali weledi wanaopatikana shuleni au mandhari yanayoana na shule hujulikana kama wanasaikolojia wa shule. Saikolojia ya elimu inajishughulisha na utaratibu wa kutoa elimu kwa watu na umma kwa jumla na umma mdogo, kama vile watoto wenye vipaji na wale wenye ulemavu.

Saikolojia ya elimu inaweza kueleweka kwa sehemu kupitia masomo mengine. Saikolojia ya elimu vilevile huarifiwa na saikolojia, ikileta uhusiano baina ya utabibu na biolojia. Saikolojia ya elimu pia huarifu masafa mapana ya masomo maalum yakiwemo mpango wa mafunzo. Teknolojia ya elimu, mtaala uliokuzwa, masomo yaliyopangwa, masomo maalumu, sayansi tambuzi na sayansi masomo. Katika vyuo vikuu, idara za elimu ya saikolojia zimehifadhiwa katika vitivo vya elimu. Hii ni kwa sababu ya uwezekano wa ukosefu wa uwakilishaji wa maudhui ya saikolojia ya elimu katika utangulizi wa vitabu vya saikolojia.

Sosholojia ya elimu

Sosholojia ya elimu ni somo linalohusu jinsi taasisi za kijamii na kani huathiri michakato na matokeo ya elimu, na kinyume chake. Kwa wengi, elimu hueleweka kama mbinu ya kushinda vizuizi, kufanikisha usawa na kupata amani na hadhi kwa wote (Sargent 1994). Wanafunzi wanaweza kutiwa motisha na hamu ya maendeleo na uboreshaji. Elimu hutambuliwa kama mahali ambapo watoto huweza kujikuza kulingana na mahitaji yao ya pekee.[33] Jukumu la elimu linaweza kuwa ni kukuza mtu binafsi hadi kilele. Uelewa wa shabaha na mbinu za michakato ya utangamano wa kielimu hutofautiana kulingana na dhana ya sosholojia iliyotumika.

Maendeleo ya elimu

 
Ramani ya dunia ikionyesha Viwango vya Elimu (kulingana na Ripoti ya Maendeleo ya Binadamu 2007/2008)
     0.950 kwenda juu      0.900–0.949      0.850–0.899      0.800–0.849      0.750–0.799      0.700–0.749      0.650–0.699      0.600–0.649      0.550–0.599      0.500–0.549      0.450–0.499      0.400–0.449      0.350–0.399      chini ya 0.350      hakuna takwimu

Katika nchi zinazoendelea idadi na uzito wa shida zilizoko kwa kawaida ni kubwa. Watu wa vijijini wakati mwingine huwa hawana habari kuhusu umuhimu wa elimu. Hata hivyo, nchi nyingine zina wizara ya elimu na katika masomo mengi, kama vile kujifunza lugha za kigeni, kiwango cha elimu kimo juu kuliko katika nchi zilizoendelea. Kwa mfano, katika nchi zinazoendelea ni kawaida kupata wanafunzi wakizungumza lugha nyingi za kigeni kwa usanifu mkubwa, ilhali jambo hili ni nadra katika nchi zilizoendelea ambapo idadi kubwa ya watu huzungumza lugha moja.

Vilevile kuna shinikizo la kiuchumi kutoka kwa wazazi ambao hupendelea watoto wao wapate pesa kwa muda mfupi kuliko faida za elimu ya muda mrefu. Utafiti wa hivi karibuni kuhusu ajira ya watoto na umasikini zimependekeza kuwa familia zilizokumbwa na umasikini zinapofikia kiwango fulani cha kukidhi mahitaji yao ya kimsingi, wazazi huwarejesha watoto wao shuleni. Hii imethibitshwa kuwa kweli mara tu kizingiti kinapovukwa. Hata kama uwezekano wa thamani ya kiuchumi ya ajira ya watoto inaongezeka baada yao kurudishwa shuleni.

 
Urusi ina wahitimu wengi kuliko nchi nyingine yoyote katika Ulaya.

Ukosefu wa vyuo vikuu bora na kiwango cha chini cha kukubalika katika vyuo hivi ni dhahiri katika nchi zilizo na idadi kubwa ya watu. Baadhi za nchi zina mitaala mikuu inayoweza kubadilika kwa urahisi, inayofanana na yenye miundo zaidi.

  • Kutokana na utandawazi shinikizo kwa wanafunzi katika shughuli za mtaala zimeongezeka
  • Kuondolewa kwa asili mia fulani ya wanfunzi kwa ajili ya uboreshaji wa masomo (kwa kawaida hufanywa shuleni baada ya daraja la kumi)

India inakuza teknolojia na mtandao. India ilizindua EDUSAT, elimu ya setilaiti ambayo inaweza kuwafikia wengi kwa gharama ya chini. Kuna pia mpango ulioanzishwa na shirika la OLPC, kundi lililotokana na maabara ya MIT lililoungwa mkono na mashirika makuu ili kukuza kompyuta ya kupakata ambayo ingeghalimu $100, ili kuwezesha kuwasilisha elimu ya programu ya kompyuta. Kompyuta hizi zimesambaa kote kufikia mwaka wa 2009. Kompyuta hizi zinauzwa au kutolewa kama msaada. Hii itawezesha nchi zinazoendelea kuwapa watoto wao elimu kwa kutumia mitambo.

Barani Afrika, shirika la NEPAD limezindua programu ya masomo ya mtandao inayotoa vifaa vya kompyuta na masomo ya mtandao kwa shule zote za msingi na upili kwa kipindi cha miaka kumi. Vikundi vya binafsi kama vile Wamormoni, wanajikakamua kuwapa watu fursa ya kupokea elimu katika nchi zinazoendelea kupitia miradi kama vile Perpetual Educational Fund. Mradi wa maendeleo kimataifa inayofahamika kama nabuur.com, com iliyoanza kwa msaada wa rais wa Marekani Bill Clinton, hutumia mtandao kuwezesha ushirikiano wa watu binafsi kuzungumzia maswala ya maendeleo ya jamii.

Umataifishaji

Elimu inaendelea kuwa jambo la kimataifa. Si vifaa vyake tu vinavyoendelea kuathiriwa na mazingira ya kimataifa yenye ukwasi bali pia mabadiliko ya wanafunzi katika viwango vyote yanayochangia kuendesha jukumu hili muhimu. Kwa mfano kule Uropa, programu ya Socratis Erusmus imechechemua mabadilishano kati ya vyuo vikuu vya Uropa. Vile vile, Shirika la Soros hutoa fursa nyingi kwa wanafunzi kutoka Asia ya kati na Uropa mashariki. Wasomi wengi hudai kwamba ingawa mfumo fulani unaweza kuzingatiwa kuwa bora au mbaya kuliko mwingine, kuzoea aina tofauti ya elimu mara nyingi huonwa kuwa elementi muhimu ya kuzoea masomo ya kimataifa.[34]

Dini na elimu

Makala kuu: Elimu ya kidini

Elimu katika dini ya Uislamu ni muhimu kwa wake na waume, haswa kwa watoto wadogo. Kinyume na dhana ya kawaida, kutafuta aina zote za maarifa, yawe ya kitaaluma, ya kidini au ya kidunia yanaruhusiwa kwa watu wa umri wowote. Hata hivyo, masomo ya umri mdogo huonwa kuipa akili fursa ya kumakinika bila kuathiriwa na shida na majukumu ya maisha ya utu uzima.[35]

Tazama pia

Marejeo

  1. UNESCO, elimu kwa wote Ufuatiliaji Report 2008, Net Enrollment Rate katika elimu ya msingi
  2. Se Merriam et al. Kujifunza kwa watu wazima: A Comprehensive Guide (San Francisco: Jossey-Bass, 2007). Sharan Miriam, Rosemary Caffarella na Lisa Baumgartner wameandika kuwa tunahitaji kuangalia kwa karibu ndani ya mipaka yetu wenyewe, wenyeji wa marekani kwa mfano….. ili kupata mifumo haswa ya fikra na imani zikiwa ndani ya thamani za tamaduni tofauti na mifumo ya epistemilojia ambayo inaweza kutumiwa kupanua uelewa wetu juu ya elimu ya ngumbaru.(uk 218). Merriam wanaendelea kueleza kuwa, azma nyingine ya kupata ufahamu juu ya mifumo mingine ya maarifa, ni faida ambayo maarifa yatakuwa nayo kuathiri utendakazi wetu na wanafunzi walio na mtizamo tofauti isipokuwa ile ya kimagharibi. Antone na Gamlin (2004) kwa mfano wanatoa sababu kuwa programu za kujua kusoma na kuandika za watu asili lazima ziwe zaidi ya kusoma, kuhesabu na kuandika ambako hulenga kufikia ajira kuu' (uk 26). Kwa hakika elimu halisi inahusu kuhifadhi mtazamo maalum na kudumisha tamaduni tofauti na za lazima. Kujua kusoma na kuandika kunahusu kuashiria tena na kutafsiri tena uzoefu uliopita, na kwa wakati huo kuheshimu maadili ya jadi. Uwezo wa kusoma na kuandika kuhusu “kuishi” maadili haya kwa wakati wa sasa. Uwezo huu wa kusoma na wa kuandika unahusu kuwa na maono ya siku za usoni. Asili ya uwezo wa kusoma na kuandika itakuzwa na kupata maelezo katika yote yanayofanywa. Hivyo, programu za asili ya kuweza kusoma na kuandika zinafaa kulenga mtazamo pana unaotambua njia za kipekee ambazo watu asili huwakilisha uzoefu na maarifa yao.(uk 26). Mara kwa mara Merriam na wenzake pia hurejelea mahitaji haya ya “Kutanua uelewa wa elimu ya ngumbaru” kwa kupitia enzi ya utamaduni nyeti nadharia zinazohusiana na mwingiliano wa ndani kati ya masomo na muktadha wa jamii. Kwa kawaida hutazamwa kwa muktadha wa maadili yanayotofautiana, imani, uzoefu, taswira na mazingira yanayowiana na njia za kale na mbinu asili pamoja na fikra za kibinafsi na za kijumla. Kwa mfano katika majadiliano yao, majaribio ya kusoma, waandishi wanatoa maoni kuwa, katika kukubali ujuzi na masomo kutoka kwa uzoefu kama tukio la kitamaduni, taswira … na wasomi wa kisasa huwa muhimu. Kati ya matokeo ya fikra muhimu kuhusu utambuzi kutoka kwa mwegemeo wa utamaduni ni uhakiki ambao umeendelezwa kuhusu nadharia ya elimu ya kale na uzoefu … Muhimu kati ya hizi changanuzi ni changamoto kwa fikra asili kuwa kusoma ni jambo linalofanyika ndani ya mtu binafsi. Kwa hakika, kusoma hujumuisha maingiliano ya wanafunzi na mazingira ya jamii wanamokulia.(uk 180).
  3. ^Tazama kwa ujumla R.A Malatest na wenzake . Best Practices katika Kuongeza Aboriginal Post-sekondari Enrollment Rates (Kanada: Baraza la Mawaziri wa Elimu, Kanada, 2002) na Dr Pamela Toulouse, Kusaidia Aboriginal Student Success: Self-Esteem na Identity, A Hai Mafundisho strategin (Presentation mikononi katika Utafiti wa Elimu Ontario 2007 Kongamano) [1]
  4. Katika mkoa wa Manitoba nchini Kanada kwa mfano, juhudi za pamoja kati ya serikali na taasisi za elimu (vyuo na vyuo vikuu) kumesababisha utekelezaji wa programu 13 za Access. Programu hizi hutilia maanani mbinu na maudhui ya kale katika upokezi wa elimu ya juu; na pia huwapa wanafunzi misaada mbalimbali ya tamaduni nyeti (kama vile wazee na washauri) ili kuzidisha mafanikio katika elimu ya juu. Watetezi wa programu hizi mara nyingi husisitiza kuwa kati ya miaka ya 2001/2002 na 2005/2006 (data iliyopatikana ya hivi karibuni) jumla ya wanafunzi 800 walihitimu kutoka kwa programu hizi na vyeti na asilimia 70.8 ya wanafunzi waliojiandikisha katika miaka hii walikuwa wa usuli wa asili. Takwimu hizi zimetolewa kutoka kur. 141-143 za Manitoba Council on Post-Secondary Education Statistical Compendium for the Academic Years Ending in 2006 [2] halmashauri ya Manitoba kuhusu elimu ya juu. Kulingana na watetezi hawa, kuwekwa pamoja kwa mitindo asili ya elimu ndani ya programu hizo zinazolenga wanafunzi asili, ni kipengele muhimu kinachochangia kukamilika kwa elimu ya juu ya wanafunzi asili waliokisiwa kuwa 566 ambao hawangetarajiwa kuhitimu kiwango hiki cha mafanikio.
  5. Examples of subjects. Curriculumonline.gov.uk. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-08-21. Iliwekwa mnamo 2009-04-20. Archived 21 Agosti 2008 at the Wayback Machine.
  6. Dunn and Dunn. Learningstyles.net. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-02-03. Iliwekwa mnamo 2009-04-20.
  7. Biographer of Renzulli. Indiana.edu. Iliwekwa mnamo 2009-04-20.
  8. Thomas Armstrong's website Archived 21 Machi 2009 at the Wayback Machine. detailing Multiple Intelligences
  9. Keirsey web-site. Keirsey.com. Iliwekwa mnamo 2009-04-20.
  10. Type Delineator description. Algonquincollege.com. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-03-01. Iliwekwa mnamo 2009-04-20.
  11. Swassing, RH, Barbe, WB, & Milone, MN (1979). The Swassing-Barbe Mfumo Index: Zaner-Bloser mfumo Kit. Columbus, OH: Zaner-Bloser.
  12. Priscilla Theroux (2004-04-26). Varied Learning Modes. Members.shaw.ca. Iliwekwa mnamo 2009-04-20.
  13. Barbe, WB, & Swassing, RH, pamoja MN Milone. (1979). Kufundisha kupitia mfumo uwezo: Dhana na mazoea. Columbus, OH: Zaner-Bloser.
  14. Learning mfumo maelezo kutoka Learning Curve website. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-04-04. Iliwekwa mnamo 2009-12-07.
  15. Guy Claxton speaking on What's The Point of School?. dystalk.com. Iliwekwa mnamo 2009-04-23.
  16. / Jinsi duniani mifumo shule bora hutoka topg. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-08-24. Iliwekwa mnamo 2009-12-07.
  17. Citationsy (2018-11-29). How to Download Research Papers and Scientific Articles for free (en). The Citationsy Blog. Iliwekwa mnamo 2018-12-05T07:44:12Z.
  18. Blurton, Craig. New Directions of ICT-Use in Education (PDF). Iliwekwa mnamo 2007-02-06.
  19. IKT katika Elimu
  20. Potashnik, M. and Capper, J.. Distance Education:Growth and Diversity (PDF). Jalada kutoka ya awali juu ya 2000-09-19. Iliwekwa mnamo 2007-02-06.
  21. Taghioff, Daniel. Seeds of Consensus—The Potential Role for Information and Communication Technologies in Development.. Jalada kutoka ya awali juu ya 2003-10-12. Iliwekwa mnamo 2003-10-12.
  22. Open University wa Uingereza Official website
  23. Indira Gandhi Taifa Open University Official website
  24. Hanushek, Uchumi Matokeo na Shule ya Quality
  25. UCLA Economics Qur'ani 183 kutoka Profesa Boustan
  26. Daron Acemoglu, Simon Johnson, na James A. Robinson, "The kikoloni Chimbuko la Comparative Maendeleo: An Empirical Investigation." American Economic Review 91, no.5 (Desemba 2001) :1369-1401.
  27. Eric A. Hanushek, na Ludger Woessmann, "Jukumu la cognitive ujuzi katika maendeleo ya kiuchumi." Journal of Economic Literature 46, no.3 (Septemba 2008) :607-608.
  28. Yakobo Mincer, "Mgawanyo wa kazi kipato: utafiti na kumbukumbu maalumu kwa mtaji mbinu." Journal of Economic Fasihi 8, no.1 (Machi 1970) :1-26.
  29. Angalia, kwa mfano, Daudi Kadi, "Causal elimu juu ya athari za mapato," katika uchumi Handbook wa kazi, mwisho na Ashenfelter na Daudi Orley Card. Amsterdam: Kaskazini-Holland, 1999:1801-1863; James J. Heckman, Lance J. Lochner, na Petra E. Todd., "Earnings utendaji, viwango vya tiba kurudi na madhara: The Mincer equation na nje," katika Handbook ya ya Uchumi wa Elimu, mwisho na Eric A. Hanushek na Finis Welch. Amsterdam: Kaskazini Holland, 2006:307-458.
  30. Samuel Bowles na Herbert Gintis, Elimu katika kibepari Marekani: Educational Mageuzi na utata wa Kiuchumi Life (Basic Books, 1976)
  31. Robinson, K.: Shule Kill Creation. TED Talks, 2006, Monterrey, CA, USA.
  32. Finn, JD, Gerber, SB, Boyd - Zaharias, J. (2005). Small madarasa katika darasa mapema, mafanikio ya kielimu, na kufuzu kutoka high school. Journal of Educational Psychology, 97, 214-233.
  33. Schofield, K. (1999). "The Malengo ya Elimu", Queensland State Elimu: 2010, [Juu] URL: www.aspa.asn.au / Papers / eqfinalc.PDF [Accessed 2002, 28 Oktoba]
  34. Dubois, HFW, Padovano, G., & Stew, G. (2006) Kuboresha muuguzi kimataifa mafunzo: an American-Kiitaliano kesi masomo. Kimataifa Nursing Review, 53 (2): 110-116.
  35. Inter-Islam> ZZ> Elimu <http://www.inter-islam.org/AZ/E/E.htm#Education[dead link]>.

Viungo vya nje

Jua habari zaidi kuhusu Education kwa kutafuta kupitia mradi wa Wikipedia Sister
  Uchambuzi wa kamusi kutoka Wikamusi
  Vitabu kutoka Wikitabu
  Dondoo kutoka Wikidondoa
  Matini za vyanzo kutoka Wikichanzo
  Picha na media kutoka Commons
  Habari kutoka Wikihabari
  Vyanzo vya elimu kutoka Wikichuo