Zuhura (alama: ♀; pia: Ng'andu; kwa Kiingereza Venus) ni sayari ya pili katika mfumo wa jua na sayari zake. Kati ya sayari zote za jua ndiyo inayofanana zaidi na dunia yetu.

Zuhura ikionekana kama nyota ya kwanza wakati wa jioni kando ya mwezi.
Venus - August 4 2016.png

Jina la sayari

Sayari hii ina majina mawili kwa Kiswahili: Zuhura, kwa matamshi mengine pia "Zuhra", ni jina leye asili ya Kiarabu زُهَرَة zuhara lenye maana asilia ya "mwenye kung'aa".

Ng'andu ni jina lenye asili ya Kibantu.

Tabia za sayari

Kwenye anga la usiku inang'aa kushinda nyota zote isipokuwa mwezi. Kutokana na nguvu ya mwanga wake inaonekana mapema kati ya nyota za kwanza zinazoonekana jioni; vilevile huwa inaonekana kama nyota ya mwisho wakati wa pambazuko.

Zuhura ina umbali wa kati ya kilomita milioni 107.5-108.9 kutoka jua. Umbali kutoka dunia yetu hutegemea na mahali pa dunia na Zuhura kwenye mizingo yao ya kuzunguka jua: uko kati ya kilomita milioni 38.3-260.9.

Ukubwa wake na pia kemia yake zinafanana sana na dunia ikiwa kipenyo chake ni km 12,103.6 kwenye ikweta.

Haina mwezi wowote.

Mwaka wa Zuhura (ambao ni muda wa kutimiza obiti moja wa kuzunguka dunia) una siku 224.7 za kidunia.

Siku ya Zuhura (ambayo ni muda wa dura moja ya sayari yenyewe) ina siku 243 za kidunia.

Zuhura ni sayari yenye mzunguko kufuatana na mwendo wa saa.

Hali ya hewa ni ya joto sana, kwa wastani sentigredi 500. Hewa yake ni hasa ya kabonidaioksaidi[1] inayosababisha mawingu mengi yanayozuia sura yake isionekane kwa darubini. Kutokana na halijoto kali hakuna maji.

Utafiti

Warusi na Wamarekani walifaulu kupeleka vipimaanga mbalimbali hadi Zuhura, vingine vilipita na kupima hewa, vingine vilifika kwenye sura ya sayari na kutuma picha za mazingira hadi kuharibika kutokana na joto kali.

Uso wa sayari umefanyiwa utafiti kwa msaada wa rada kutoka vipimaanga Magellan na Pioneer-Venus. Kutokana na matokeo yake ramani ya kwanza ilitokea. Sehemu kubwa ya sayari ni tambarare yenye vilima na mabonde yasiyo marefu. Kutokana na joto kubwa (mnamo 500°C) hakuna maji wala bahari.

 
Ramani hii ya Zuhura imepatikana kutokana na vipimo vya rada; rangi ya buluu huonyehsa maeneo yaliyo karibu na uwiano wa wastani wa sayari;

Kuna sehemu mbili ambako nyanda za juu zinapanda juu ya uwiano wa kawaida na hizi zilifananishwa na kontinenti za Dunia. Karibu na ikweta ya Zuhura iko sehemu inayoitwa "Aphrodite Terra" yenye ukubwa kama Amerika Kusini. Kwenye upande wa mashariki kuna safu za milima na mabonde makubwa pamoja na volkeno. Sehemu ya pili huitwa "Ishtar Terra" yenye ukubwa sawa na Australia kwenye Dunia. Hapa kuna milima ya Maxwell yenye urefu wa mita 10.800 juu ya uwiano wa wastani.

Tanbihi

  1. "Atmosphere of Venus". The Encyclopedia of Astrobiology, Astronomy, and Spaceflght. Iliangaliwa Agosti 2018. Jalada kutoka ya awali juu ya 2019-04-02. Iliwekwa mnamo 2018-08-28.

Viungo vya nje

Wikimedia Commons ina media kuhusu:

Kuhusu ramani za Zuhura

  Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Zuhura kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.
Mradi wa Astronomia Makala hii imewahi kukaguliwa na kuboreshwa kwenye warsha ya pamoja ya Jenga Wikipedia ya Kiswahili, Wikimedia Community User Group Tanzania na ASSAT. Imepewa hali ya ulinzi. Tunaomba mapendekezo yote ya usahihisho na nyongeza zipelekwe kwanza kwenye ukurasa wa majadiliano