Hispania Mpya (Kihisp. Virreynato de Nueva España) ilikuwa eneo la kikoloni la Hispania katika Amerika ya Kaskazini, Amerika ya Kati na sehemu za visiwa vya Asia kuanzia mwaka 1535 hadi 1821. Lilijumlisha nchi za leo za Mexiko, Belize, Guatemala, El Salvador, Honduras, Nikaragua, Costa Rica, visiwa vya Karibi, Ufilipino na visiwa mbalimbali katika Pasifiki pamoja na maeneo yaliyo leo majimbo ya kusini ya Marekani (majimbo ya Kalifornia, Nevada, Utah, Colorado, Wyoming, Arizona, New Mexico, Texas na Florida). Hata Venezuela ilikuwa sehemu yake hadi kuhamishwa Granada mpya mnamo 1717.

Maeneo ya Hispania Mpya (bila sehemu za Pasifiki na Asia) mnamo mwaka 1919
Bendera ya Hispania iliyotumiwa katika Hispania Mpya

Maeneo haya mapana yalikuwa chini ya usimamizi wa gavana mkuu mwenye cheo cha "mfalme mdogo" ("virrey" yaani mfalme mdogo au makamu wa mfalme) aliyekaa mjini Mexico City.

Maeneo yake yaligawiwa kwa majimbo yaliyoongozwa na magavana wa pekee.

Hispania ilipaswa kuachia Uingereza visiwa vya Bay Islands (1643), Jamaika (iliyoitwa awali Santiago - hadi 1655) , Visiwa vya Kaiman (1670), Trinidad (1797) na Belize (1798). Nusu ya magharibi ya Hispaniola ilikuwa koloni ya Haiti ya Ufaransa mwaka 1697.

Tangu uhuru wa koloni za Uingereza katika Amerika ya kaskazini zilizounda Muungano wa Madola ya Amerika (yaani Marekani) mawazo ya kujitenga na Hispania yalianza kusambaa hata katika Mexiko.

Uhuru wa Mexiko ulitokea mwaka 1821 na kuanzia sasa zilikuwa sehemu za Kuba, Puerto rico na Ufilipino pekee zilizobaki chini ya Hispania hadi Vita ya Marekani dhidi Hispania mwaka 1898 iliyomaliza utawala wa Hispania katika Amerika na Asia.

Tazama pia hariri

Marejeo hariri