Klaudio Ptolemaio

(Elekezwa kutoka Ptolemy)

Kuhusu wafalme wa Misri walioitwa Ptolemaio angalia Nasaba ya Waptolemaio

Ptolemaio alivyoonyeshwa kama mfalme wa sayansi pamoja na mama mwakilishi wa astronomia katika kitabu cha Ujerumani mnamo mwaka 1503

Klaudio Ptolemaio (kwa Kigiriki Κλαύδιος Πτολεμαῖος, Klaúdios Ptolemaíos; 100 – mnamo 170 BK) alikuwa mtaalamu wa hisabati, jiografia na astronomia kutoka nchini Misri.

Kiutamaduni alikuwa Mgiriki aliyeishi mjini Aleksandria wakati Misri ilikuwa jimbo la Dola la Roma. Hakuna habari za hakika kuhusu maisha yake.

Ptolemaio ni maarufu kwa vitabu vyake vilivyohifadhiwa alipotoa hitimisho ya elimu ya siku zake. Vitabu hivyo vilitafsiriwa kwa Kilatini na Kiarabu vikawa msingi wa elimu hadi mwisho wa Zama za Kati kwa Wakristo wa Ulaya na pia kwa Waislamu wa Mashariki ya Kati.

Astronomia

 
Ptolemaio aliona Dunia katika kitovu cha ulimwengu

Katika kitabu chake cha Almagest alieleza jinsi Wagiriki walivyoona ulimwengu. Walidhani Dunia iko kwenye kitovu cha ulimwengu. Magimba mengine ya angani yaani Mwezi, Jua na sayari tano zilizojulikana ziliizunguka kwa njia za mizingo yenye umbo la duara. Mizingo hii ilidhaniwa kama tufe za kioo. Tufe la nje kabisa lilikuwa tufe la nyota. Ili kupatanisha mwendo wa sayari na miendo yao jinsi ilivyotazamwa angani ilikuwa lazima kuwaza pia miendo mingine ya sayari ya kuzunguka tena katika duara ndogo wakati wa kufuata njia zao kwenye mzingo katika tufe husika.

Picha hii ya muundo wa ulimwengu ilitazamiwa kuwa kweli hadi mafundisho mapya ya Koperniko na Galileo yaliyoanza kusambaa kuanzia mwaka 1543.

 
Dunia ya Ptolemaio - ramani iliyochorwa Italia kwenye karne ya 15 kufuatana na maandiko yake

Jiografia

Kitabu kingine kilichohifadhiwa na kuwa na athari kubwa kilikuwa "Jiografia" yake. Humo alikusanya data kuhusu mahali palipojulikana katika Dola la Roma wakati wake.

Ptolemaio alijua tayari ya kwamba Dunia ina umbo la tufe. Alitambua pia ya kwamba habari zake zilihusu takriban robo moja ya uso wa Dunia na robo tatu hazikujulikana kwake.

Habari alizokuwa nazo zilianza upande wa magharibi kwenye Visiwa vya Kanari katika Bahari Atlantiki zikaelekea hadi katikati ya China, kwa jumla nyuzi 180. Upande wa kaskazini alikuwa na habari kuhusu Visiwa vya Shetland (kaskazini kwa Britania) hadi pwani ya Afrika ya Mashariki upande wa kusini.

Hisabati

Kati ya kazi zake za kihisabati kuna uhakiki mmoja tu uliohifadhiwa kupitia taarifa za wataalamu wengine: hii ni Uhakiki wa Ptolemaio juu ya uhusiano kati ya pande nne za pembenne na ulalo wake kama kona za pembenne hulala juu ya duara.

Viungo vya nje

 
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
 
Wikiquote ina mkusanyiko wa dondoo kuhusu:

Matoleo ya maandiko yake

Juu ya Ptolemaio

      . http://www.u.arizona.edu/~aversa/scholastic/Dictionary%20of%20Scientific%20Biography/Ptolemy%20(Toomer).pdf. Archived 14 Machi 2012 at the Wayback Machine.

Maelezo mengine

Picha

  Makala hii kuhusu mwanasayansi fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Klaudio Ptolemaio kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.